Kuhubiri Katika Ulimwengu
Wenye Kubadilika-Badilika
1 Mambo yanaweza kubadilika kwa uharaka sana. Katika usiku mmoja, msiba wa kiasili, tatizo la kiuchumi, msukosuko wa kisiasa, au msiba uliotangazwa sana unaweza kuwa kichwa cha mazungumzo. Hata hivyo, kwa uharaka huohuo, watu wanaweza kugeuzia uangalifu wao mahali pengine. (Mdo. 17:21; 1 Kor. 7:31) Katika ulimwengu huu wenye kubadilika-badilika, tunawezaje kuvuta uangalifu wa watu ili tushiriki nao ujumbe wa Ufalme?
2 Tambua Mahangaiko ya Wengine: Njia moja ya kuvuta uangalifu wa watu ni kwa kutaja matukio ya kisasa. Akihimiza wasikilizaji wake wafikiri sana kuhusu msimamo wao pamoja na Mungu, kwenye pindi moja Yesu alisema kuhusu misiba ya wakati uliotoka kupita iliyokuwa akilini mwao. (Luka 13:1-5) Katika njia hiyohiyo, tunapotoa habari njema, ni vizuri tutaje habari inayovuma au suala la kwetu ambalo linagusa maisha za watu wa eneo letu. Hata hivyo, tunapozungumzia mambo hayo, tunapaswa kuwa waangalifu ili tusichukue msimamo wowote katika mambo ya kisiasa au ya kijamii.—Yn. 17:16.
3 Tunawezaje kujua yale ambayo watu wanafikiria sasa? Labda njia bora zaidi ni kuuliza tu ulizo na baadaye kusikiliza. (Mt. 12:34) Kupendezwa na watu kutatuchochea tufahamu maoni ya wengine na kuuliza habari zaidi kwa busara. Maneno yanayosemwa na mwenye nyumba bila kuyafikiria kimbele yanaweza kufunua hangaiko la watu wengi katika eneo na yanaweza kufungua njia ya kutoa ushahidi.
4 Kutayarisha Utoaji: Katika kujitayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani katika ulimwengu wenye kubadilika-badilika, tunaweza kutumia kitabu Kutoa Sababu. Mapendekezo yenye kusaidia kuhusu jinsi ya kuingiza matukio ya kisasa katika utoaji wetu yanatolewa kwenye ukurasa wa 12-13, chini ya kichwa “Uhalifu/Kutopatwa na Madhara” na “Matukio ya Sasa.” Habari za kufanana na hizo zinaweza kupatikana katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Septemba 2000, ukurasa wa 8. Unapotayarisha utoaji wako, hakikisha kwamba unatia ndani andiko linalofaa.
5 Tunapokuwa waangalifu kwa mahangaiko yenye kubadilika-badilika ya watu wa eneo letu, tunapaswa kupatanisha utoaji wetu wa habari njema na hali hizo. Katika njia hiyo, tunazungumza na watu kuhusu yale yanayogusa sana maisha zao. Kwa kufanya hivyo, tunasaidia wengine wengi wajue Yule asiyebadilika katika sifa zake na viwango vyake.—Yak. 1:17.