Mkazo wa wenzako na pendeleo lako la kuhubiri
1 Mkazo wa wenzetu ni uvutano wenye nguvu—uvutano mzuri au mbaya. Watumishi wenzetu wa Yehova huwa na uvutano mzuri unaotuchochea kwenye kazi zilizo bora. (Ebr. 10:24) Lakini, washiriki wa familia wasio Mashahidi, wafanyakazi wenzetu, wanashule wenzetu, majirani, au watu wengine tunaojuana nao wanaweza kutia mkazo juu yetu ili tufuate mwendo unaopingana na kanuni za Kikristo. Huenda wakasema “kwa kushushia heshima mwenendo [wetu] mwema kuhusiana na Kristo.” (1 Pet. 3:16) Tunawezaje kulinda azimio letu la kuendelea kuhubiri ingawa mkazo mbaya ambao tunaweza kukutana nao kutoka kwa wenzetu?
2 Washiriki wa Familia: Nyakati nyingine, mume na baba asiyekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova huenda asitake mke na watoto wake washiriki katika huduma ya peupe. Hali ilikuwa hivyo katika familia moja huko Mexico. Mke na watoto saba wa mwanamume mmoja walikuja katika kweli. Kwanza, mume huyo alipinga kwa sababu hakutaka familia yake ihubiri na kutolea watu vichapo vya kibiblia toka nyumba hadi nyumba. Aliona jambo hilo kuwa liliwashushia heshima. Hata hivyo, mke wake na watoto wake walibaki imara katika uamuzi wao wa kutumikia Yehova na kushiriki kikawaida katika huduma. Baada ya muda, mwanamume huyo akaanza kuona umaana wa kukubali mpango wa Mungu kuhusu kazi ya kuhubiri, naye pia akajiweka wakfu kwa Yehova. Ilichukua miaka 15 kusudi akubali kweli, lakini je, angepata kufanya hivyo wakati wowote ikiwa familia yake haingedumu katika pendeleo lao la kuhubiri?—Luka 1:74; 1 Kor. 7:16.
3 Wafanyakazi Wenzetu: Jitihada zako za kutoa ushahidi kwa wafanyakazi wenzako huenda zisipokewe vizuri na wengine. Dada mmoja alieleza kwamba wakati mazungumzo kuhusu mwisho wa ulimwengu yalipotokea katika ofisi, yeye alidhihakiwa kwa sababu alipendekeza kusoma Mathayo sura ya 24. Hata hivyo, siku chache baadaye, mmoja wa wafanyakazi wenzake alimwambia kwamba alikuwa amesoma sura hiyo na kwamba ilimgusa moyo. Aliachiwa kichapo, na mipango ikachukuliwa kwa ajili ya funzo la Biblia pamoja naye na mume wake. Funzo la kwanza lilidumu mpaka saa nane za usiku. Baada ya funzo la tatu, wakaanza kuhudhuria mikutano, na mapema baada ya hapo wakaacha matumizi ya tumbaku na kuanza kushiriki katika huduma. Je, jambo hilo lingetukia ikiwa dada yetu hangefanya jitihada yoyote ya kushiriki tumaini lake pamoja na wengine?
4 Wanashule Wenzako: Ni jambo la kawaida kwa vijana Mashahidi kupatwa na mkazo wa vijana wenzao shuleni, na kuogopa kwamba vijana wengine watawadharau kwa sababu ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Tineja mmoja Mkristo wa kike katika Shirikisho la Amerika alisema: “Nilikuwa na woga wa kutoa ushahidi kwa vijana wengine kwa sababu niliogopa watanicheka.” Kwa hiyo, aliepuka nafasi za kutoa ushahidi kwa wenzake shuleni na katika eneo. Unawezaje kukomaza nguvu ya kukabiliana kwa uhodari na mkazo wa wenzako? Mtumaini Yehova, ukitafuta upendeleo wake. (Mez. 29:25) Furahia uwezo wako wa kutumia Neno la Mungu katika huduma yako. (2 Tim. 2:15) Yule kijana wa kike ambaye tulitoka tu kutaja alianza kusali kwa Yehova, akimwomba amsaidie kukuza tamaa ya kuongea na wanashule wenzake. Akaanza kutoa ushahidi wa vivi-hivi shuleni, akapata matokeo mazuri, naye akaanza bila kukawia kuongea na kila mtu aliyejua. Akamalizia kwa kusema: “Vijana hao wanahitaji na wanataka tumaini la wakati ujao, naye Yehova anatutumia sisi ili kuwasaidia.”
5 Majirani: Huenda tukawa na majirani au watu wengine tunaojuana nao ambao huonyesha chuki fulani kutuelekea sisi kwa sababu ya kuwa kwetu Mashahidi wa Yehova na kwa sababu ya imani yetu. Ikiwa unaogopa yale wanayofikiri, jiulize: ‘Je, wanajua ile kweli inayoongoza kwenye uzima wa milele? Ninaweza kufanya nini ili kugusa moyo wao?’ Mwangalizi msafiri mmoja alieleza kwamba matokeo mazuri hupatikana wakati ushahidi unapotolewa kwa majirani kwa kiasi kidogo na cha kawaida. Omba sana Yehova akupe nguvu na hekima inayohitajiwa ili uendelee kutafuta watu wenye mioyo minyofu.—Flp. 4:13.
6 Kushindwa na mkazo usiofaa wa wenzetu huenda kukapendeza wapinzani, lakini je, kufanya hivyo kutakuwa kwa faida yao bora zaidi—au yetu? Yesu alipingwa na watu katika jamii yake mwenyewe. Alivumilia hata maneno makali kutoka kwa ndugu zake wa kambo. Lakini alijua kwamba angeweza kuwasaidia tu kwa kushikamana na mwendo ambao Mungu alikuwa ameweka kwa ajili yake. Hivyo, Yesu ‘alivumilia maongezi yaliyo kinyume ya namna hiyo yenye kufanywa na watenda-dhambi dhidi ya [faida zao] wenyewe.’ (Ebr. 12:2, 3) Tunapaswa kufanya hivyohivyo. Azimia kutumia vizuri zaidi pendeleo lako la kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Kwa kufanya hivyo, “utajiokoa wewe mwenyewe na wale wakusikilizao pia.”—1 Tim. 4:16.