Unaweza Kutoa Ushahidi Wakati Haukupanga Kufanya hivyo!
1. (a) Inamaanisha nini kuhubiri wakati mutu hawakupanga kufanya hivyo? (b) Ni watu wangapi wanaohuzuria hapa leo ambao walijua kweli kwa mara ya kwanza kupitia njia hiyo?
1 Ni watu wangapi katika kutaniko lenu ambao walijua kweli kwa mara ya kwanza kupitia Shahidi ambaye alihubiri wakati hakupanga kufanya hivyo? Unaweza kushangazwa na jibu. Kutoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo kunatia ndani kuhubiria watu tunaokutana nao katika utendaji wetu wa kila siku—tunaposafiri, tunapotembelea watu wa jamaa yetu ao majirani, ao tunapokwenda kununua vitu, kwenye masomo, kwenye kazi, na mahali pengine. Katika kikundi kimoja cha Mashahidi wenye kubatizwa 200, watu 80 kati yao walitolewa ushahidi mara ya kwanza na shahidi aliyehubiri wakati hakupanga kufanya hivyo! Kwa hiyo, njia hiyo ya kuhubiri ni yenye matokeo sana.
2. Ni mifano gani iliyo katika Biblia ya watu waliotoa ushahidi bila kupanga kufanya hivyo?
2 Mara nyingi wahubiri katika karne ya kwanza walitoa ushahidi wakati hawakupanga kufanya hivyo. Kwa mfano, alipokuwa akisafiri kwenda Samaria, Yesu alimhubiria mwanamuke aliyeshota maji kwenye chemchemi ya Yakobo. (Yoh. 4:6-26) Filipo alianzisha mazungumzo na ofisa Mwetiopia wa makao ya kifalme aliyekuwa akisoma kitabu cha Isaya; Filipo alianzisha mazungumzo kwa kumuuliza: “Je, wewe kwa kweli unaelewa unayoyasoma?” (Mdo. 8:26-38) Alipokuwa gerezani katika Filipi, mtume Paulo alimhubiria mlinzi wa gereza. (Mdo. 16:23-34) Baadaye, akiwa katika nyumba ya wafungwa, Paulo ‘aliwakaribisha kwa fazili wale wote walioingia ndani kwake, akiwahubiria ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yanayohusu Bwana Yesu Kristo.’ (Mdo. 28:30, 31) Wewe pia unaweza kutoa ushahidi wakati haukupanga kufanya hivyo, hata ikiwa wewe ni mwenye haya. Namna gani?
3. Ni jambo gani linaloweza kutusaidia tushinde haya?
3 Jinsi ya Kuanza: Kwa wengi kati yetu ni vigumu kuanza mazungumzo na watu ambao hatujue. Inaweza kuwa hata vigumu kuhubiria watu tunaofahamiana nao ambao si Mashahidi. Hata hivyo, tutapata nguvu ya kuzungumza na watu, ikiwa tunafikiria sana kuhusu wema wa Yehova, kweli za maana sana ambazo ametolea watumishi wake, na kujua kwamba ulimwengu unapatikana katika hatari. (Yona 4:11; Zab. 40:5; Mt. 13:52) Zaidi ya hiyo, tunaweza kumwomba Yehova atusaidie, ‘tujipatie ujasiri.’ (1 The. 2:2) Mwanafunzi mmoja wa Gileadi alisema: “Mara nyingi nimeona kwamba sala inasaidia wakati ninakuwa na magumu ya kuzungumza na watu.” Ikiwa unasita kusema, fanya sala fupi ya moyoni.—Neh. 2:4.
4. Ni mradi gani tunaopaswa kujitilia kwanza, na kwa nini?
4 Kama inavyoitwa, namna hiyo ya kutoa ushahidi haiombi tuanze mazungumzo na utangulizi ao andiko fulani lililotayarishwa kimbele. Linaweza kuwa jambo lenye kusaidia kujuwa kwamba tunaweza kuanzisha mazungumzo hata ikiwa hatukupanga kufanya hivyo. Wahubiri wengi wanasema kwamba kufanya hivyo kunawapa uhakika wanaohitaji ili kuanzisha mwishowe mazungumzo kuhusu habari njema. Ikiwa mutu hapendi kuzungumza, si lazima kumkaza. Kwa heshima, kata mazungumzo na umuache.
5. Ni nini ilimsaidia dada mmoja mwenye haya kutoa ushahidi wakati hakupanga kufanya hivyo?
5 Alipokuwa akinunua vitu sokoni, dada mmoja mwenye haya alikuwa akianza kwa kumtazama mutu na kisha kucheka kidogo kwa urafiki. Ikiwa mutu naye anacheka, hivyo, anazungumza naye kwa kifupi. Ikiwa mutu anakubali kuzungumza, hilo linamtolea uhakika wa kuendelesha mazungumzo pamoja naye. Anasikiliza kwa uangalifu na kujaribu kuelewa sehemu gani ya habari njema itakayomvutia. Kwa kutumia njia hiyo, ametolea watu wengi vichapo vyetu na kuanzisha hata funzo la Biblia.
6. Namna gani tunaweza kuanzisha mazungumzo mahali fulani wakati hatukupanga kufanya hivyo?
6 Kuanzisha Mazungumzo: Tunaweza kusema nini ili kuanzisha mazungumzo? Yesu alipozungumza na mwanamke kwenye kisima, alianza tu kwa kumwomba maji. (Yoh. 4:7) Kwa hiyo, labda tunaweza kuanza mazungumzo kwa kumsalimu mutu kwa urafiki ao kumuuliza ulizo fulani. Mnapozungumza unaweza kupata nafasi ya kumtolea wazo fulani la Biblia na labda kupanda mbegu ya kweli. (Mhu. 11:6) Wahubiri fulani wamepata matokeo mazuri kwa kuzungumzia hali fulani yenye kupendeza ambayo ilimfanya mutu atafute kujua zaidi na kuwa tayari kuuliza. Kwa mfano, munapongojea mganga, unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kusema, “Nitafurahi wakati nitaishi bila kugonjwa.”
7. Namna gani kuwa watazamaji kunatusaidia tutoe ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo?
7 Kuwa pia watazamaji kutatusaidia tuanzishe mazungumzo. Tukimtazama mzazi aliye na watoto wenye kujiendesha kwa adabu, tunaweza kumpongeza mzazi huyo na kumuuliza, “Ni kitu gani kimekusaidia uwe na watoto walio na mwenendo mzuri?” Dada mmoja analinda akilini habari ambazo wengine wanazungumzia kwenye kazi na hivyo anawazungumzia habari zinazofaa zinazotegemea mambo yanayopendeza wafanyakazi wenzake. Alipojua kwamba mwanamke mmoja mahali anapotumika alijitayarisha kuolewa, alimtolea Amkeni! inayozungumzia jinsi ya kutayarisha ndoa. Hilo liliongoza kwenye mazungumzo ya Biblia baadaye.
8. Namna gani tunaweza kutumia vitabu vyetu ili kuanzisha mazungumzo?
8 Namna nyingine ya kuanzisha mazungumzo ni kusoma vitabu vyetu mahali ambapo wengine wanaweza kutuona. Ndugu mmoja anafungua Mnara wa Mlinzi ao Amkeni! kwenye habari moja yenye kuvutia na kuanza kuisoma. Ikiwa anaona kwamba mutu aliye pembeni yake anaangalia gazeti hilo, anamuuliza ulizo ao anatoa maelezo mafupi kuhusiana na habari hiyo. Mara nyingi kufanya hivyo kunamsaidia kuanzisha mazungumzo na kutoa ushahidi. Kuacha tu vitabu vyetu mahali ambapo vinaweza kuonwa na watu, hilo linaweza kuchochea wafanyakazi wenzetu ao wale tunaosoma nao watafute kujua mambo yaliyo ndani na kuuliza maulizo.
9, 10. (a) Namna gani tunaweza kutafuta nafasi za kutoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo? (b) Namna gani umeweza kufanya hivyo?
9 Tafuta Nafasi: Kwa kuwa kazi ya kuhubiri inaombwa kufanywa kwa haraka sasa, hatupaswi kupuuza kutoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo. Tunapaswa kutafuta nafasi za kutoa ushahidi katika utendaji wetu wa kila siku. Wazia kimbele kuhusu watu ambao unaweza kukutana nao, na ufikirie jinsi unaweza kuanzisha mazungumzo ya kirafiki pamoja nao. Uwe na Biblia katika mkono na vitabu vyetu ili uweze kuzungumza na wale wanaoonyesha kupendezwa.—1 Pet. 3:15.
10 Kwa kutumia akili, wahubiri wengi wamepata nafasi za kutoa ushahidi wakati hawakupanga kufanya hivyo. Dada mmoja anayeishi katika jengo lenye kulindwa sana anatumia mahali palipotengenezwa kwa ajili ya watu kupumzikia, ili kutia picha mbalimbali za mchezo wa mafumbo. Wakati watu wanasimama na kutoa maelezo kuhusu picha hizo nzuri, anapata nafasi ya kuanzisha mazungumzo na kuwaelezea kuhusu ahadi ya Biblia ya “mbingu mpya na dunia mpya.” (Ufu. 21:1-4) Unaweza kufikiria njia mbalimbali zinazoweza kukutolea nafasi za kutoa ushahidi wakati haukupanga kufanya hivyo?
11. Namna gani tunaweza kufuatia kupendezwa tunapotoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo?
11 Fuatia Kupendezwa: Ikiwa unapata mutu anayekusikiliza, jaribu kufuatia kupendezwa. Inapofaa, unaweza kumwambia mutu huyo hivi: “Nimefurahi sana kuzungumza nawe. Tutaonana namna gani ili tuendelee kuzungumza tena?” Wahubiri fulani wanamtolea mutu aliyependezwa adresi yao na namba yao ya telefone na kusema: “Nilifurahia mazungumzo yetu. Ikiwa unapenda kujua mengi kuhusu mambo tuliyozungumzia, unaweza kutumia adresi na namba hii ya telefone ili kunipata.” Ikiwa hauna namna ya kufuatia kupendezwa, fanya mpango ili kutaniko la eneo ambamo mutu huyo anaishi, lifuatie kupendezwa bila kukawia, jaza fomu (S-43) na kuituma kupitia kutaniko lenu.
12. (a) Kwa nini tuhesabu wakati tunaopitisha tukitoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo? (b) Ni matokeo gani mazuri ambayo wahubiri walipata kwa kutoa ushahidi wakati hawakupanga kufanya hivyo? (Ona kisanduku “Kutoa Ushahidi Wakati Hawakupanga Kufanya Hivyo Kulileta Matokeo Mazuri!”)
12 Tunapaswa kuhesabu wakati tuliopitisha katika namna hiyo ya kuhubiri. Kwa hiyo, hakikisha kwamba umeandika saa hizo, hata ikiwa ulifanya dakika chache tu. Fikiria jambo hili: Ikiwa kila mhubiri anatoa ushahidi wakati hakupanga kufanya hivyo, na kufanya dakika 5 kila siku, hilo lingeongeza zaidi ya saa milioni 17 kila mwezi!
13. Ni nini litatuchochea tutoe ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo?
13 Tuna sababu nzuri zaidi za kutoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo—Kumpenda Mungu na kupenda jirani. (Mt. 22:37-39) Kwa kuwa tunapendezwa sana na sifa za Yehova na makusudi yake, hilo linatuchochea tuseme kuhusu “utukufu wa fahali ya ufalme wake.” (Zab. 145:7, 10-12) Kuhangaikia kikweli majirani wetu kutatuchochea tutafute kila nafasi ili tuwatolee habari njema wakati ambapo kungali wakati. (Rom. 10:13, 14) Tukifanya mpango mbele ya wakati na kujitayarisha, sisi wote tunaweza kutoa ushahidi wakati hatukupanga kufanya hivyo na labda kupata furaha ya kusaidia mutu fulani mwenye moyo wa haki ajue ukweli.
[Wazo la fungu kwenye ukurasa wa 4]
Linaweza kuwa jambo lenye kusaidia ikiwa unajiwekea mradi wa kukutana na watu na kuanzisha mazungumzo pamoja nao
[Wazo la fungu kwenye ukurasa wa 5]
Kwa kutumia akili, wahubiri wengi wamepata nafasi za kutoa ushahidi wakati hawakupanga kufanya hivyo
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
Mapendekezo ili Kuanzisha Mazungumzo
◼ Omba Yehova akusaidie uanzishe mazungumzo
◼ Tafuta watu wanaoonekana kuwa na hali ya kirafiki na wasio haraka
◼ Tazama watu usoni, cheka kidogo, na uzungumzie jambo litakalowapendeza ninyi wawili
◼ Uwe msikilizaji mzuri
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Kutoa Ushahidi Wakati Hawakupanga Kufanya Hivyo Kulileta Matokeo Mazuri!
• Ndugu mmoja alipokuwa kwenye garage akingojea gari lake litengenezwe, aliwahubiria wale waliokuwa pembeni yake na kuwatolea mialiko ili waende kusikiliza hotuba ya watu wote. Kisha mwaka mmoja, alipokuwa kwenye mkusanyiko, ndugu asiyemjua alimsalimu kwa shauku. Alikuwa mmoja wa wale ambao alitolea mialiko alipokuwa kwenye garage kisha mwaka mmoja! Mutu huyo aliendaka kusikiliza hotuba ya watu wote na kuomba funzo la Biblia. Sasa yeye na muke wake wamekwisha kubatizwa.
• Dada mmoja aliyejifunza kweli kupitia mhubiri aliyetoa ushahidi wakati hakupanga kufanya hivyo, aliona watu aliokutana nao kupitia watoto wake watatu kuwa ndilo eneo lake. Mahali ambapo watoto wake watatu walikuwa wakisomea na kwenye mikutano kwa ajili ya wazazi, alikuwa akikutana pamoja na majirani wake huko na wazazi wengine, na hilo aliliona kuwa eneo lake. Anapojitambulisha, anatoa maelezo rahisi lakini yenye kugusa moyo kwamba ni Biblia iliyomsaidia sana ili kulea watoto wake, na kisha anazungumzia habari nyingine. Kwa kuwa amekwisha kuanzisha mazungumzo, linakuwa jambo rahisi kutumia Biblia katika mazungumzo yatakayofuata. Kwa kutumia njia hiyo, amewasaidia watu 12 wafikie ubatizo.
• Dada mmoja alipotembelewa na muuzisha bima (kama wafanyakazi wa Sonas), alitumia nafasi hiyo ili kutoa ushahidi. Dada akamuuliza ikiwa amekwisha kupata assurance ya afya nzuri, furaha, na uzima wa milele. Akakubali na kumuuliza dada huyo ni mpango gani wa assurance ambao alikuwa akizungumzia. Dada akamuonyesha ahadi za Biblia na kumtolea kitabu; mutu huyo alikisoma chote magaribi moja tu. Wakafanya mpango wa kujifunza Biblia. Akaanza kuhuzuria mikutano na baadaye akabatizwa.
• Alipokuwa katika safari ya ndege, dada mmoja alianzisha mazungumzo na mwanamuke aliyekaa pembeni yake na alianza kumtolea ushahidi. Walipofika, dada alimtolea mwanamuke huyo adresi yake na namba yake ya telefone na kumtia moyo kuomba funzo la Biblia wakati Mashahidi wa Yehova watakapomtembelea. Siku iliyofuata, Mashahidi wawili walimtembelea mwanamuke huyo nyumbani kwake. Akaanza kujifunza Biblia, akafanya maendeleo ya haraka, na kubatizwa, na bila kukawia yeye pia akaanza kuongoza mafunzo matatu ya Biblia.
• Ndugu mwenye umri wa miaka 100 aliyekuwa kipofu aliyekuwa akiishi katika nyumba ya kutunzia watu wazee, mara kwa mara anasema, “Tuna lazima ya Ufalme.” Hilo limefanya waganga na wagonjwa waulize maulizo; hivyo alipata nafasi ya kuwaelezea Ufalme ni nini. Mwanamuke mmoja anayetumika mahali hapo alimuuliza ndugu huyo jambo atakalofanya katika Paradiso. Alijibu, “Nitaona na kutembea tena na kuharibu kinga hii ya vilema.” Kwa kuwa ni kipofu, anamwomba mwanamke huyo amusomee magazeti. Wakati binti wa ndugu alikuja kumtembelea, mwanamke huyo alimwomba ruhusa ya kubeba magazeti hayo nyumbani. Mganga mmoja alimueleza hivi binti wa ndugu huyo, “Hapa katika nyumba ya kutunzia watu wazee, kichwa kikuu cha habari ni: ‘Tuna lazima ya Ufalme.’”
• Dada mmoja aliyekuwa akingojea kwenye mustari ili kuingia katika restaurant, alisikia kikundi cha watu waliozeeka waliokaa pembeni yake wakizungumzia mambo ya politike. Mmoja kati yao akasema kwamba serikali haiwezi kumaliza matatizo yetu. Dada huyo akasema moyoni mwake, ‘Sitapoteza nafasi hii.’ Akafanya sala fupi moyoni na akawakaribia. Kisha kujitambulisha, aliwaelezea kuhusu serikali itakayomaliza matatizo ya wanadamu yaani, Ufalme wa Mungu, na akawatolea broshua aliyokuwa nayo. Ndipo tu msimamizi wa restaurant akawakaribia. Dada akawaza kwamba atamufukuza. Tofauti na hilo, msimamizi huyo alimwambia dada kwamba alikuwa anasikiliza yale waliokuwa wakizungumza na kwamba angependa pia kupata broshua. Mfanyakazi mmoja mwanamuke alikuwa akiwasikiliza pia akakaribia akitiririkwa na machozi. Alikuwa akijifunza Biblia hapo mbele na alipenda kurudilia funzo lake.