Tuwe Wenye Bidii Katika “Kutoa Ushahidi Kamili”
1 Kama Yesu na watumishi wengine waaminifu wa zamani, mtume Paulo alikuwa mhubiri wa habari njema mwenye bidii, ‘akitoa ushahidi kamili’ katika hali yoyote ile. Hata alipofungiwa nyumbani, alikuwa “akiwapokea kwa fadhili wote wale walioingia ndani kwake, akiwahubiri ufalme wa Mungu na kufundisha mambo yahusuyo Bwana Yesu Kristo kwa uhuru wa usemi ulio mkubwa zaidi sana.”—Mdo. 28:16-31.
2 Sisi pia tunaweza kuwa wenye bidii katika “kutoa ushahidi kamili” wakati wote. Hilo linatia ndani kutoa ushahidi kwa watu tunaokutana nao katika safari yetu ya kwenda na kutoka kwenye Kusanyiko la Wilaya “Mtukuzeni Mungu” na tunapokuwa katika jiji ambako kusanyiko litafanyiwa.—Mdo. 28:23; Zab. 145:10-13.
3 Je, Ni Ushahidi Unaotolewa Bila Kupangwa au wa Vivi Hivi? Je, kuna tofauti? Ndiyo. Kitu kisichopangwa kinatukia kwa bahati tu au bila kukusudia, kana kwamba hakikufikiriwa au ni cha maana ndogo. Ufafanuzi huo bila shaka haufai kwa huduma yetu. Kama ilivyokuwa kweli kuhusu Paulo, kutukuza Mungu kwa kutoa ushahidi ni kwa maana kwetu, na tunapaswa kukusudia kutoa ushahidi mahali popote inapofaa wakati wa safari zetu. Hata hivyo, namna tunavyokaribia wengine inaweza kufafanuliwa sawasawa kuwa ya vivi hivi—ni kusema, yenye utulivu, yenye urafiki, na ya hali ya kawaida. Njia hiyo inaweza kuzaa matunda mazuri.
4 Tujitayarishe Kutoa Ushahidi: Paulo alilazimika kutokeza nafasi za kutoa ushahidi alipofungiwa nyumbani huko Roma. Kutoka makao yake, alichukua hatua ya kualika nyumbani mwake wakuu wa Kiyahudi wa mahali hapo. (Mdo. 28:17) Hata ingawa kulikuwako kutaniko la Kikristo huko Roma, Paulo alipata habari kwamba jamii ya Kiyahudi katika jiji hilo ilikuwa na habari ndogo ya moja kwa moja kuhusu imani ya Kikristo. (Mdo. 28:22; Rom. 1:7) Hakujizuiza “kutoa ushahidi kamili” kuhusu Yesu Kristo na Ufalme wa Mungu.
5 Fikiria kimbele watu wote utakaokutana nao katika safari zako walio na ujuzi mdogo sana kuhusu Mashahidi wa Yehova. Huenda wasijue hata kwamba tunatolea watu mafunzo ya Biblia ya nyumbani bila kuomba malipo. Uwe macho kuhusu nafasi za kutoa ushahidi kwa wale unaokutana nao unaposafiri, unapokatiza safari ili kupumzika, unapotwaa mafuta ya gari, unapofanya ununuzi dukani, unapokaa katika hoteli, unapokula katika mikahawa, unapotumia vyombo vya kusafirishia watu wote, na kadhalika. Panga kimbele yale unayoweza kusema ili kuanzisha mazungumzo na kutoa ushahidi mfupi. Labda siku zilizo mbele unaweza kufanya mazoezi kwa kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa majirani wako, washiriki wa familia yako, wafanyakazi wenzako, na watu wengine unaojuana nao.
6 Utahitaji kiasi cha kutosha cha vichapo vya kutumia unapotoa ushahidi wa vivi hivi. Vichapo gani? Unaweza kutumia trakti yoyote. Ikiwa trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? inapatikana, kazia mafungu matano ya kwanza, ambako sababu mbalimbali za kusoma Biblia zinatolewa. Onyesha kuponi kwenye ukurasa wa mwisho kwa ajili ya kuomba funzo la Biblia la bila malipo. Unapopata mtu anayesikiliza, mtolee broshua Anataka. Kwa kufikiria kimbele kukutana na watu wanaosema lugha nyingine, chukua trakti, broshua, na magazeti katika lugha zinazosemwa katika majimbo mengine. Ikiwa unasafiri kwa gari, huenda ukawa na uwezo wa kuchukua vichapo vingine vichache vya msingi kwa ajili ya wale wanaoonyesha kupendezwa kikweli na ujumbe wa Ufalme.
7 Fikiria Sura Yako na Mwenendo Wako: Tunapaswa kuhakikisha kwamba mwenendo wetu na pia mavazi yetu na kujipamba kwetu hakutawapa wengine mawazo mabaya au kuwafanya ‘waseme vibaya’ kuhusu tengenezo la Yehova. (Mdo. 28:22) Hilo halitumiki tu tunapohudhuria kusanyiko bali pia tunaposafiri na wakati wa mapumziko. Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 2002, ukurasa wa 18, fungu la 14, unaonya: “Hatupaswi kuvalia mavazi ya kujionyesha, ya kiajabu-ajabu, yanayochochea nyege, yanayofunua uchi, au ya mitindo inayopita kiasi. Kwa kuongezea, tunapaswa kuvalia kwa njia ya ‘kumstahi Mungu.’ Hilo ni jambo linalotufanya tutafakari, sivyo? Hatupaswi kuvalia tu kwa njia inayofaa wakati tunapohudhuria mikutano na kuvalia ovyoovyo nyakati nyingine. Sikuzote mavazi yetu yanapaswa kuonyesha staha na heshima kwa kuwa sisi ni Wakristo na wahudumu wakati wote.”—1 Tim. 2:9, 10.
8 Tunapaswa kuvalia kwa kiasi na heshima. Ikiwa sura yetu na mwenendo wetu vinaonyesha wakati wote kwamba tunamwamini Mungu, hatutajisikia kamwe kuwa wenye kulazimika kujizuiza tusitoe ushahidi wa vivi hivi kwa sababu sura yetu ni isiyoweza kukubaliwa kwa mhudumu.—1 Pet. 3:15.
9 Kutoa Ushahidi wa Vivi Hivi Ni Kwenye Kuzaa Matunda: Mnamo miaka miwili ambayo katika hiyo Paulo alikuwa akifungiwa nyumbani huko Roma, aliona matokeo mazuri ya jitihada zake za kutoa ushahidi. Luka aliripoti kwamba “wengine wakaanza kuamini mambo yaliyosemwa.” (Mdo. 28:24) Paulo mwenyewe alikadiria matokeo ya ‘kutoa kwake ushahidi kamili’ alipoandika: “Mambo yangu yamegeuka kuwa kwa ajili ya kusonga mbele kwa habari njema badala ya kuwa vingine, hivi kwamba vifungo vyangu vimejulikana kwa watu wote kwa kushirikiana na Kristo miongoni mwa Walindaji wa Praetori wote na wale wengine wote; na walio wengi zaidi kati ya akina ndugu katika Bwana, wakihisi uhakika kwa sababu ya vifungo vyangu vya gereza, wanaonyesha moyo mkuu hata zaidi kulisema neno la Mungu bila hofu.”—Flp. 1:12-14.
10 Mwaka uliopita, baada ya kupitisha mchana kwenye kusanyiko la wilaya, mume mmoja na mke wake waliona jambo lenye kuzaa matunda walipotoa ushahidi wa vivi hivi kwa mwanamke aliyehudumia watu katika hoteli na aliyewauliza kuhusu kadi zao za vitambulisho kwa ajili ya kusanyiko. Wakamweleza kuhusu kusanyiko na pia kuhusu tumaini ambalo Biblia inatoa kuhusu wakati ujao wa wanadamu. Wakamtolea trakti Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? na kumweleza kuhusu mpango wa funzo la Biblia la bila malipo. Mwanamke huyo akasema kwamba alipenda mtu fulani amtembelee, akaandika jina lake na anwani yake kwenye ukurasa wa mwisho wa trakti, na akaomba mume na mke hao wachukue mipango. Ni mafanikio gani unayoweza kufurahia mwaka huu kwa kuwa mwenye bidii katika “kutoa ushahidi kamili”?
11 Endeleza Kikamili Habari Njema: Wazia jinsi Paulo alivyokuwa mwenye furaha aliposikia kwamba Wakristo wenzake walikuwa wakiiga mfano wake wenye bidii! Sisi sote na tufanye yote tuwezayo ili kuendeleza habari njema kwa kutoa ushahidi wa vivi hivi kuhusu imani zetu zinazotegemea Biblia tunapofaidika na kusanyiko la wilaya linalokaribia.
[Study Questions]
1, 2. Ni kitu gani kinachokuvutia kuhusu jinsi Paulo alivyoona kuhubiri habari njema, na tunawezaje kuiga mfano wake wa “kutoa ushahidi kamili”?
3. Tunawezaje kuepuka kufanya ushahidi wetu wa vivi hivi ugeuke kuwa tu jitihada isiyopangwa?
4. Ni kitu gani kilichomwezesha Paulo atoe ushahidi kwenye makao yake?
5, 6. Ni nafasi gani tunazoweza kuwa nazo za kutoa ushahidi wa vivi hivi, na tunawezaje kujitayarisha ili kufanya hivyo kwa matokeo?
7, 8. Ni onyo gani tunalopaswa kutii kuhusu sura yetu na mwenendo wetu tunaposafiri na wakati wa mapumziko?
9. Paulo alipata matokeo gani katika kutoa ushahidi huko Roma?
10. Mume mmoja na mke wake walipata mafanikio gani katika kutoa ushahidi mwaka uliopita?
11. Ni sifa gani tunazopaswa kusitawisha ili kuendeleza habari njema kwa “kutoa ushahidi kamili”?
[Picture on page 3]
Vichapo Vinavyohitajiwa Ili Kutoa Ushahidi wa Vivi Hivi
■ Je, Ungependa Kujua Mengi Zaidi Kuhusu Biblia? (trakti)
■ Mungu Anataka Nini Kwetu? (broshua)
■ Trakti katika lugha nyingine
■ Vichapo vingine vya msingi
[Picture on page 4]
Usiwasahau!
Kusahau nani? Wale wote wanaopendezwa waliohudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo au hotuba ya pekee. Je, tumewaalika waje kuhudhuria kusanyiko la wilaya la mwaka huu? Yaelekea wengi kati yao watahudhuria ikiwa wanatiwa moyo kwa fadhili. Wanapofurahia ushirika wenye kujenga kwenye kusanyiko na programu ya kiroho yenye kutia moyo, watavutwa wamkaribie zaidi Yehova na tengenezo lake. Kwa nini usiwaalike na kuona jinsi watakavyoitikia? Watolee habari zote wanazohitaji, kutia ndani tarehe za kusanyiko, maelezo kuhusu jinsi ya kupata mahali ambapo kusanyiko litafanyiwa, wakati ambapo vipindi vitakapoanza na kumalizika, na kuwaonyesha kimbele yale yaliyo kwenye programu kama yanavyopatikana kwenye ukurasa wa mwisho wa toleo la Juni 8, 2003, la Amkeni!