Sifuni Yehova kwa Kutoa Ushahidi wa Vivi Hivi
1 Watumishi waaminifu wa Yehova hutafuta nafasi za kumsifu yeye kila siku. (Zab. 96:2, 3; Ebr. 13:15) Njia moja ambayo kwa hiyo tunaweza kufanya hivyo ni kwa kutoa ushahidi wa vivi hivi. Waabudu wengi wa Yehova leo ni wenye shukrani kwamba mtu fulani aliwajulisha ujumbe wa Ufalme kwa kuwatolea ushahidi wa vivi hivi.
2 Kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa mtu mmoja mara nyingi kunafungulia wengine njia ya kusikia ujumbe wa Ufalme. Kwa mfano, mazungumzo ya Yesu na mwanamke Msamaria kwenye kisima cha Yakobo yalifanya wengine wengi wapendezwe na habari njema. (Yn. 4:6-30, 39-42) Paulo na Sila walipokuwa gerezani katika Filipi, walitoa ushahidi kwa mlinzi wa gereza, na nyumba nzima ya mwanamume huyo ikakubali kweli.—Mdo. 16:25-34.
3 Nafasi Zilizopo: Ni nafasi gani ulizo nazo za kutoa ushahidi wa vivi hivi? Watu fulani hufanya hivyo wanapofanya ununuzi dukani, wanaposafiri katika vyombo vya kusafirishia watu wote, au wanapongojea wakutane na mganga. Wengine wanaweza kutoa ushahidi wakati wa mapumziko kazini au shuleni. Kuwa tu na kimoja cha vichapo vyetu vya kibiblia kikionekana wazi kunaweza kuchochea wengine waulize kuhusu imani zetu.—1 Pet. 3:15.
4 Jinsi ya Kuanza: Binti mmoja wa miaka saba mwenye haya alisikia kwenye mkutano kwamba ni jambo la maana sana kwa wote kuhubiri. Hivyo, alipoenda kufanya ununuzi dukani pamoja na mama yake, alitia broshua mbili katika mfuko wake. Mama yake alipokuwa akitoa hesabu kwenye meza ya kuuzia vitu, binti huyo akatoa broshua kwa mwanamke mmoja, ambaye aliikubali kwa fadhili. Alipoulizwa jinsi alivyopata moyo mkuu wa kumkaribia mwanamke huyo, binti yule mwenye haya akajibu: “Nilisema tu, Tayari, Simama, Kwenda! Na nikaenda!”
5 Ili kutoa ushahidi wa vivi hivi, sote tunahitaji roho kama ile ya yule binti mdogo. Ni nini linaloweza kutusaidia? Sali ili upate moyo mkuu wa kusema bila woga. (1 Thes. 2:2) Tayarisha ulizo au maelezo kuhusu habari yenye kupendeza ambayo unaweza kutumia ili kuanzisha mazungumzo. Kisha, uwe na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zako.—Luka 12:11, 12.
6 Kutoa ushahidi wa vivi hivi kwa watu tunaokutana nao kila siku kunamletea Yehova sifa na kunatupatia furaha. Kunaweza kusaidia mtu aanze kutembea katika njia inayoongoza kwenye uzima wa milele.