Jitayarishe Kujifunza Unabii wa Isaya!
1 “Waabudu waaminifu waweza kuwa na uhakika kwamba Yehova . . . hatauruhusu ulimwengu wa Shetani uendelee kuwapo hata kwa siku moja zaidi kupita ilivyo haki.” Ni maneno yenye kutia moyo kama nini! Yalinukuliwa kutoka wapi? Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote. Je, unabii wa Isaya unatutolea sababu ya kufikia uamuzi huo wenye kutia moyo? Ndiyo! Katika kitabu hicho cha Biblia, kichwa cha wokovu kinakaziwa waziwazi na kwa nguvu. (Isa. 25:9) Kwa sababu hiyo, litakuwa jambo lenye kutia moyo sana kujifunza sehemu hiyo ya Neno la Mungu kwenye Funzo la Kitabu. Je, tutakuwako ili kuifurahia kila juma? Kwa nini tunapaswa kuwako?
2 Kwenye Isaya 30:20, Yehova anaitwa ‘Mfundishaji wetu Mtukufu.’ Kila Mkristo anapaswa kusikiliza wakati Yehova anaposema nasi kupitia kurasa za Neno lake na kupitia vichapo vyenye msingi juu ya Biblia, vichapo vinavyotolewa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45; Isa. 48:17, 18) Bila shaka, hilo ni kweli kuhusu kitabu Unabii wa Isaya I. Unawezaje kufaidika kikamili zaidi kutokana na kujifunza kitabu hicho?
3 Jitayarishe kwa Ajili ya Kushiriki: Weka kando wakati wa kutosha kila juma ili kujitayarisha kwa ajili ya funzo la kitabu. Soma habari iliyotolewa kuwa mgawo fungu kwa fungu. Tafakari juu ya kila moja la maulizo yaliyochapwa? Tia alama kwenye majibu katika kitabu chako. Maandiko yanayonukuliwa kutoka katika kitabu cha Isaya yanachapwa kwa herufi nzito nyeusi. Yasome kwa uangalifu. Kuhusu yale maandiko mengine yanayotajwa, tafuta hayo ili kuona jinsi yanavyohusiana na habari. Tafakari juu ya yale unayojifunza. Kisha, shiriki matokeo ya matayarisho yako pamoja na kikundi chako cha funzo la kitabu.
4 Yule ndugu anayeongoza funzo la kitabu anapaswa kusaidia wahudhuriaji wote wafanye matumizi mazuri ya Biblia na kufahamu thamani yenye kutumika ya habari inayozungumziwa. Ikiwa unaombwa kujibu wa kwanza, toa jibu jepesi na la moja kwa moja. Ikiwa mtu fulani amekwisha kufanya hivyo, unaweza kuchanganua nukta inayozungumziwa. Labda unaweza kuonyesha jinsi andiko la msingi linavyotegemeza kichwa cha habari. Jaribu kutoa maelezo katika maneno yako wenyewe, na ufurahie kushiriki katika mazungumzo.
5 Acheni tuchunguze pamoja kwa hamu ule ujumbe wenye thamani katika kitabu cha Isaya. Ujumbe huo utatutia moyo tuishi kila siku tukitazamia kwa furaha wokovu wa Yehova!—Isa. 30:18.