Je, Unaweza Kutumikia Mahali Ambapo Kuna Uhitaji Mkubwa Zaidi?
1 Je, umekwisha kufikiria kuhamia mahali ambapo kuna uhitaji wa watangazaji wa Ufalme wengi zaidi? Ikiwa unaalikwa ‘kuvuka ili usaidie,’ je, utaitikia kama alivyofanya mtume Paulo? (Mdo. 16:9, 10) Katika makutaniko mengi, kuna uhitaji wa familia zenye kukomaa kiroho, mapainia ili kusaidia kutembelea eneo lote, au wazee na watumishi wa huduma ili kusaidia kuchukua uongozi. Huenda eneo likaundwa na miji midogo-midogo yenye kujitenga ambayo inatawanyika katika eneo kubwa la vijijini. Jumba la Ufalme la karibu zaidi huenda likawa kwenye umbali wa kilometa nyingi. Kazi ya kimwili huenda ikawa ndogo. Hali ya hewa huenda isiwe nzuri sikuzote. Je, utakuwa na nia tayari ya kukubali magumu hayo? Inawezekanaje kufanikisha jambo hilo?
2 Imani na Tumaini Vinahitajiwa: Chini ya mwongozo wa Mungu, Abramu aliacha mji wa nyumbani kwake wa Uru na kusafiri kilometa 1,000 kwenda Harani pamoja na mke wake, mtoto wa ndugu yake, na baba yake mzee-mzee, Tera. (Mwa. 11:31, 32; Neh. 9:7) Baada ya Tera kufa, Yehova aliamuru Abramu, akiwa sasa na umri wa miaka 75, aache Harani na washiriki wa familia yake ili asafiri kwenda nchi ambayo Mungu angemwonyesha. Abramu, Sarai, na Loti “wakatoka.” (Mwa. 12:1, 4, 5) Ni kweli kwamba Abramu hakuhama ili kutumikia mahali ambapo kulikuwa uhitaji mkubwa zaidi wa wahudumu. Lakini kuhama kwake kuliomba jambo fulani. Jambo gani?
3 Iliomba Abramu awe na imani na tumaini ili ajaribu kufanya jambo hilo. Mawazo yake na namna yake ya maisha vilipaswa kubadilika. Alipaswa kuacha usalama uliotokana na washiriki wa familia yake. Lakini alitumaini kwamba Yehova angemtunza, yeye na familia yake. Wengi leo wameonyesha kwamba wanamtumaini Yehova kwa njia hiyohiyo.
4 Migawo ya Muda Mfupi: Je, umekwisha kufurahia baraka tele zinazotokana na kutumika eneo lisilotolewa kuwa mgawo kwa mtu yeyote? Mwaka uliopita, katika zile nchi 48 zenye kupakana [za Shirikisho la Amerika], wahubiri 5,699 walitembelea maeneo 163 kati ya yale 174 yasiyotolewa kuwa mgawo kwa mtu yeyote. Wahubiri wengine 5,676 walisaidia makutaniko 380 kutembelea eneo lisilotumikwa mara nyingi. Kwa wengine, hilo lilimaanisha kusafiri miendo mirefu. Je, jambo hilo lilistahili kufanyiwa jitihada?
5 Ndugu mmoja kutoka Kalifornia ambaye alienda Utah aliandika: “Mara ya kwanza nilipoombwa kuongoza kikundi katika eneo lisilotumikwa mara nyingi, nilikuwa mwenye kusita. Lakini niliamua kukubali mgawo huo. Si kwamba tu sijapata kamwe kujutia jambo hilo lakini pia lilibadili maisha yangu. Ninamshukuru Yehova kila siku kwa pendeleo la kushiriki katika safari hii.” Ndugu mmoja kutoka Florida ambaye alienda Tennessee alisema kwamba hilo ndilo lilikuwa jambo la kukumbukwa zaidi katika ile miaka yake 20 katika kweli! Kijana mmoja mwenye umri wa miaka kati ya 13 na 19 kutoka Connecticut aliyekwenda Magharibi mwa Virginia alisema: “Hilo ndilo jambo bora zaidi nililojionea katika maisha yangu!” Wahubiri walio wengi hukubali kwamba kutumikia hata kwa muda mfupi mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi kumefanya uthamini wao kuelekea huduma uwe wenye kina kirefu. Ongea na wale ambao wamefanya jambo hilo. Utatambua kwamba waliinuliwa kiroho, na inaelekea kwamba watafanya hilo tena ikiwa wanatolewa nafasi.
6 Kukubali mgawo wa muda mfupi wa kutumikia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi kunatimiza kusudi lingine. Wale wanaofanya hivyo wanaweza kupata habari zenye mafaa zitakazowasaidia ‘wapige hesabu ya gharama” ya kuhamia sehemu nyingine ya nchi.—Luka 14:28.
7 Kuhamia Mahali Ambapo Uhitaji Ni Mkubwa Zaidi: Yehova anaazimia kufanya habari njema itangazwe “katika dunia yote inayokaliwa” kabla ya mwisho kuja. (Mt. 24:14) Ukijua hilo na ikiwa una uwezo, je, utakuwa tayari kuhamia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi? Kuna uhitaji katika maeneo mengi.
8 Je, wewe umeacha kazi kwa sababu ya umri? Je, una mshahara wa kawaida? Ikiwa sivyo, je, unaweza kupanga kufanya kazi yako mwenyewe? Je, una uwezo wa kupata riziki mahali popote unapopatikana? Ikiwa hauwezi kuhama, je, unaweza kusaidia mshiriki wa familia atumikie mahali pengine?
9 Ikiwa baada ya kufikiri katika sala unaona kwamba unaweza kupambana na magumu ya kuhamia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi, zungumza na familia yako na wazee katika kutaniko lenu kuhusu jambo hilo. Kisha, tayarisha barua na kuitoa kwa wazee kusudi watie ndani maelezo na mapendekezo yao kabla ya kuituma kwenye ofisi ya tawi.
10 Ni mambo gani unayopaswa kutia ndani ya barua yako? Umri wako, tarehe yako ya ubatizo, madaraka yako katika kutaniko, hali yako kuhusiana na ndoa, na ikiwa una watoto wachanga. Toa jina la mahali unapopendelea kutumikia, kulingana na mahitaji yako mwenyewe. Kwa mfano, je, unaweza kuishi mahali penye joto na unyevu? Je, unaweza kuishi katika maeneo yenye kuinuka sana? Je, unazungumza lugha fulani za kigeni?
11 Je, wewe ni mwenye bidii na mwenye kuchukua hatua? Je, hali zako zinakuruhusu kutumikia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi? Ikiwa ndiyo, basi tazama jinsi Yehova anavyomwaga baraka tele juu ya wale wanaomtumaini kadiri wanavyoonyesha roho ya kujinyima!—Zab. 34:8; Mal. 3:10.