Tieni Wakati wa Kujiburudisha pa Nafasi Yake Yenye Kufaa
1 Katika siku hizi ngumu, sisi sote tunahitaji kubadili mwendo wakati kwa wakati. Kiasi fulani cha burudisho ni chenye kufaa. Hata hivyo, wakati mwingi sana unaopitishwa katika kujiburudisha, vitumbuizo, na mazungumzo katika vikundi unaweza kupunguza uangalifu wa mtu kwa kiasi cha kutumia wakati mdogo zaidi na zaidi katika mambo ya kiroho. Tunapaswa kutia wakati wa kujiburudisha pa nafasi yake yenye kufaa. (Mt. 5:3) Hilo linawezekanaje? Kwa kufuata shauri linalopatikana kwenye Waefeso 5:15-17.
2 Weka Mipaka: Paulo aliandika kwamba Wakristo wanapaswa ‘kufuliza kuangalia sana’ jinsi wanavyoishi maisha yao kwa hekima. Kiasi na kujizuiza vinahitajiwa ili kufanya wakati wa kujiburudisha usipite ule unaohitajiwa. Ni vizuri kufikiria kwa uangalifu jinsi tunavyotumia wakati tunapokuwa hatufanyi kazi. Burudisho linapaswa kutimiza kusudi fulani lenye manufaa badala ya kutufanya tuhisi kwamba tumepoteza wakati wetu au kutuacha tukiwa wenye kuchoka sana. Ikiwa tunabaki tukijisikia kuwa wasio na thamani, wasiotosheka, na wenye hatia kwa kiasi fulani baada ya kushiriki utendaji fulani, hilo linaonyesha kwamba tunapaswa kufanya marekebisho katika matumizi yetu ya wakati.
3 Iweni Wenye Akili: Paulo alitoa shauri kuhusu ‘kujinunulia wakati unaofaa’ kwa ajili ya mambo ya maana zaidi maishani, si kuwa “wenye kukosa akili.” Wakristo waliojiweka wakfu hawawezi kuruhusu maisha yao yawe ya kujiburudisha tu. Ingawa pumziko na viburudisho vinaweza kututia nguvu kimwili, chanzo cha nguvu ya kiroho ni kani ya Mungu ya utendaji. (Isa. 40:29-31) Tunapokea roho yake kuhusiana na utendaji mbalimbali wa kitheokrasi—kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano ya kutaniko, kushiriki katika utumishi wa shambani—si kupitia burudisho.
4 Weka Mambo ya Kutanguliza: Paulo aliagiza Wakristo ‘waendelee kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.’ (Efe. 5:15-17) Yesu alifundisha kwamba utendaji wetu mbalimbali unapaswa kuweka Ufalme wa Mungu kuwa jambo la kutanguliza maishani mwetu. (Mt. 6:33) Ni jambo la lazima tufanye kwanza mambo yatakayotuwezesha kuishi kulingana na wakfu wetu kwa Yehova. Baadaye, wakati wa kujiburudisha unaweza kutiwa pa nafasi yake yenye kufaa. Wakati jambo hilo linapofanywa, litakuwa na uvutano wenye kufaa, nasi tutalifurahia zaidi.—Mhu. 5:12.