Tegemea Yehova ili Upate Nguvu
1 Kwa sababu nyingi, tunahitaji kumtegemea Yehova. Kuhubiri habari njema “katika dunia yote inayokaliwa” ni mgawo mgumu. (Mt. 24:14) Sikuzote, tunapigana na mwili wetu usiokamilika. (Rom. 7:21-23) Zaidi ya hayo, “tunashindana mwereka . . . dhidi ya watawala [wenye nguvu kupita zile za kibinadamu] wa ulimwengu wa giza hili.” (Efe. 6:11, 12) Kwa wazi, tunahitaji msaada. Tunawezaje kupata nguvu kutoka kwa Yehova?
2 Kupitia Sala: Yehova hutoa kwa ukarimu roho takatifu yake yenye nguvu kwa watumishi wake wanaoiomba. (Luka 11:13) Je, unakosa uhakika katika uwezo wako wa kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba, barabarani, au kwa njia ya simu? Je, unaogopa kutoa ushahidi kivivi hivi? Je, kutojali kwa watu katika eneo kumepunguza bidii yako? Namna gani ikiwa unapatwa na mikazo ya kufanya jambo lisilopatana na imani yako au uaminifu wako? Tegemea Yehova. Sali ili upate nguvu.—Flp. 4:13.
3 Kupitia Funzo la Kibinafsi: Kama vile tu tunavyopata nguvu kwa kula chakula cha kimwili, tunatiwa nguvu kiroho kwa kujilisha kikawaida Neno la Mungu na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 4:4; 24:45) Alipoulizwa kile kilichompa nguvu ya kuvumilia kufungwa gerezani akiwa peke yake bila Biblia huko China, Stanley Jones alisema: “Tunaweza kusimama imara katika imani. Bila shaka, tunapaswa kujifunza kwanza. Hatuna nguvu ya ndani ikiwa hatujifunzi.”
4 Kwa Kuhudhuria Mikutano: Kwenye mkutano mmoja wa Kikristo katika karne ya kwanza, Yudasi na Sila “wa[li]watia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwatia nguvu.” (Mdo. 15:32) Vivyo hivyo leo, yale tunayosikia kwenye mikutano huongeza kina cha uthamini wetu kuelekea Yehova, hujenga imani yetu, na hutuchochea kwa ajili ya huduma. Mikutano hutukutanisha kwa ukawaida na ‘wafanyakazi wenzetu kwa ajili ya ufalme wa Mungu,’ wenzetu ambao ni “msaada wenye kutia nguvu” kwetu.—Kol. 4:11.
5 Tunahitaji msaada katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushugulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Kuhusu wale wanaopata nguvu kutoka kwa Yehova, tunahakikishiwa: “Watapanda juu na mabawa kama tai; watapiga mbio na hawatachoka; watatembea, wala hawatazimia roho.”—Isa. 40:31.