“Yeye Anampa Nguvu Mtu Aliyechoka”
1 Sisi wote tunachoka mara kwa mara. Si kazi yetu tu inayotuchokesha au utendaji mwingine wa kimwili lakini tunachokeshwa pia na matatizo tunayokutana nayo katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Tukiwa watumishi wa Yehova, namna gani tunapata nguvu za kiroho zenye kuhitajiwa ili tusiregee katika kazi yetu ya kuhubiri? Tunapata nguvu hizo kwa kumtegemea yule aliye “hodari katika nguvu,” yaani Yehova. (Isa. 40:26) Anajua mahitaji yetu na anapenda kutusaidia kwelikweli.—1 Pet. 5:7.
2 Mipango ya Yehova ya Kutusaidia: Yehova anatutia nguvu kupitia roho yake takatifu, nguvu ileile aliyotumia ili kuumba ulimwengu. Tunapochoka, roho ya Mungu inatusaidia ‘kupata nguvu mpya.’ (Isa. 40:31) Jiulize mwenyewe hivi: “Ni wakati gani niliposali kwa mara ya mwisho, nikiomba roho takatifu initie nguvu ili nitimize madaraka yangu ya Kikristo?”—Luka 11:11-13.
3 Kwa kusoma kila siku na kufikiri sana juu ya Neno la Mungu lililoongozwa kwa roho na kwa kujifunza kwa ukawaida vitabu vyetu vya Kikristo, tutakuwa kama ‘mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, unaotoa matunda yake kwa wakati wake na ambao majani yake hayakauki.’—Zab. 1:2, 3.
4 Yehova anatumia pia waamini wenzetu, ambao wanaweza kuwa ‘msaada wenye kututia nguvu.’ (Kol. 4:10, 11) Wanatutia nguvu kwenye mikutano ya kutaniko kupitia mazungumzo yao yenye kujenga, maelezo yao na hotuba zao. (Mdo. 15:32) Zaidi sana wazee Wakristo wanatoa msaada wa kiroho na vitia-moyo vyenye kutia nguvu.—Isa. 32:1, 2.
5 Kazi ya Kuhubiri: Ikiwa unajisikia mwenye kuchoka, usiache kuhubiri! Tofauti na kazi zingine nyingi, kuhubiri kwa ukawaida kunatutia nguvu kwelikweli. (Mt. 11:28-30) Kuhubiri habari njema kunatusaidia tuendelee kufikiria Ufalme wa Mungu na tuendelee kukumbuka uzima wa milele na matumaini mazuri tunayongojea.
6 Kuna mambo mengi ya kufanya kabla ya kuharibiwa kwa ulimwengu huu mwovu. Tuna kila sababu ya kushikamana na kazi yetu ya kuhubiri, “tukitegemea nguvu ambazo Mungu anatoa.” (1 Pet. 4:11) Kwa msaada wa Mungu tutamaliza kazi yetu, kwa kuwa Yehova “anampa nguvu mtu aliyechoka.”—Isa. 40:29.