“Kulishwa Maneno ya Imani”
1 Kufuatia maisha ya ujitoaji kimungu kunataka jitihada sana. (1 Tim. 4:7-10) Kwa nguvu zetu wenyewe, tayari tungekuwa wenye kuchoka na kujikwaa kwa kujaribu kufuata njia hiyo. (Isa. 40:29-31) Njia moja ambayo kwa hiyo tunaweza kupata nguvu kutoka kwa Yehova ni kwa “kulishwa maneno ya imani.”—1 Tim. 4:6.
2 Chakula cha Kiroho Chenye Kujenga: Kupitia Neno lake na kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yehova anatoa chakula cha kiroho chenye kujenga. (Mt. 24:45) Je, tunatimiza sehemu yetu ili kufaidika kutokana na chakula hicho? Je, tunasoma Biblia kila siku? Je, tumepanga wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi na kutafakari? (Zab. 1:2, 3) Kula kiroho vizuri kama hivyo kunatutia nguvu na kutulinda na matokeo yenye kudhoofisha ya ulimwengu wa Shetani. (1 Yoh. 5:19) Ikiwa tunajaza akili yetu na mambo mazuri na kuyatumia katika maisha zetu, Yehova atakuwa pamoja nasi.—Flp. 4:8, 9.
3 Yehova pia anatutia nguvu kwa njia ya mikutano ya kutaniko. (Ebr. 10:24, 25) Mafundisho ya kiroho na ushirikiano mzuri tunaopata kwenye mikusanyiko hiyo vinatutia nguvu kubaki imara ijapokuwa majaribu. (1 Pet. 5:9, 10) Msichana mmoja Mkristo alisema: “Mimi ninakwenda shuleni mchana wote mzima, nayo inanichosha sana. Lakini mikutano ni kama chemchemi ya maji katika jangwa, ambako mimi ninaburudishwa na kupata nguvu ya kupambana na siku nyingine shuleni.” Tunabarikiwa kabisa kwa sababu ya jitihada tunazofanya ili kuhudhuria mikutano.
4 Kutangaza Kweli: Yesu aliona kuwahubiria wengine kama vile chakula. Kufanya hivyo kulimtia nguvu. (Yoh. 4:32-34) Hali kadhalika, tunapozungumza na wengine kuhusu ahadi za ajabu za Mungu, tunajisikia kuwa tumepata nguvu mpya. Kuwa na mengi ya kufanya katika huduma pia kunafanya moyo wetu na akili yetu vikazie Ufalme na baraka zinazokuja karibuni. Jambo hilo ni lenye kutuburudisha kweli.—Mt. 11:28-30.
5 Sisi ni wenye pendeleo kabisa kwa kufaidika na chakula cha kiroho chenye kujenga ambacho Yehova anatolea watu wake leo. Na tuendelee kupiga vigelegele kwa shangwe ili kumsifu.—Isa. 65:13, 14.