‘Wanaume Walio Zawadi’ Wanachunga kwa Shauku Kundi la Mungu
1 Yehova amefanya uandalizi wenye upendo kama nini kupitia Mwana wake kwa kutoa ‘zawadi zikiwa wanaume’! (Efe. 4:8, 11, 12) Wanaume hao wana madaraka mengi, kutia ndani kuchunga kundi la Mungu kwa namna yenye kutenda na yenye shauku. (1 Pet. 5:2, 3) Sisi sote tunafaidika na uandalizi huo unaohitajiwa sana. Ikiwa wengine wanapambana na matatizo, ikiwa ni wapya katika kushirikiana na kutaniko, ikiwa wana udhaifu fulani-fulani, au ikiwa wamekwenda kombo, wanaume hao wanapendezwa kibinafsi na hali njema ya kiroho ya wote.—Flp. 2:4; 1 Thes. 5:12-14.
2 Wakati matukio ya ulimwengu yenye kuvuruga akili yanapotokeza woga fulani, wachungaji hao wa chini huonekana kuwa “kama pahali pa kujificha na upepo, na pahali pa kufunikana na mvua.” Tunapochoka au tunapolemewa, na tunapohisi uhitaji wa kufarijiwa, wanatuburudisha, “kama mito ya maji katika pahali pakavu” au “kama kivuli cha mwamba mukubwa katika inchi ya kiu.”—Isa. 32:2.
3 Tutie Moyo Wale Wasiotenda: Wazee wanafanya jitihada ya pekee ili kutia moyo wale ambao wamekuwa wasio kawaida au wasiotenda, wakiwasaidia wawe tena wakishiriki kwa ukawaida katika utendaji wote wa kutaniko. Ziara za uchungaji zenye upendo zimesaidia wengi wahudhurie mikutano ya kutaniko kwa ukawaida na kujengwa tena kiroho hivi kwamba wao ni wenye kushiriki tena katika huduma ya shambani. Jitihada hizo zote kwa upande wa wazee zinaonyesha hangaiko lenye upendo la Yehova na uongozi wenye kutenda wa Yesu Kristo. Yesu aliweka mfano wa kuhangaikia yeyote wa kondoo zake ambaye huenda amekwenda kombo au ambaye amepotea.—Mt. 18:12-14; Yn. 10:16, 27-29.
4 Wachungaji hao wa chini hutafuta alama zinazoonyesha kwamba huenda watu fulani wakawa wenye kuyumbayumba kiroho. Wale wote wanaoonyesha alama ya kuvunjika moyo, wanaokosa ukawaida katika kuhudhuria mikutano, au wanaopunguza mwendo katika utumishi wa shambani yaelekea wanahitaji msaada wa kiroho. Wazee wana nia ya kusaidia yeyote anayeanza kuonyesha mwelekeo unaoongoza kwenye mavazi na kujipamba kwa kilimwengu au ambaye anasitawisha mtazamo wa kulaumu-laumu kutaniko. Wakiwa wenye kupendezwa kwelikweli na wenye shauku nyororo, waangalizi wenye kujali wako tayari ‘kutoa nafsi zao wenyewe’ katika jitihada za kusaidia mtu kama huyo awashe tena upendo wake kuelekea Yehova.—1 Thes. 2:8.
5 Wakati uliopita, Wakristo fulani waliojiweka wakfu walipoteza ushirikiano na kutaniko, wakaanguka katika hali ya kutotenda kiroho kwa sababu wamekuwa wenye kulemewa na matatizo ya kiafya, vizuizi vya kiuchumi, au mikazo ya kifamilia. Bila kulaumu, wazee hutoa kwa wema uhakikisho kwamba Yehova anajali kondoo wake wote na kwamba atawategemeza kupitia nyakati ngumu. (Zab. 55:22; 1 Pet. 5:7) Wachungaji wa kundi walio macho wanaweza kusaidia kondoo waone kwamba ikiwa ‘wanamkaribia Mungu, yeye atawakaribia,’ akiwatolea faraja na kiburudisho.—Yak. 4:8; Zab. 23:3, 4.
6 Tuthamini Wale Walio Dhaifu: Wachungaji wa chini wenye upendo wanahangaikia pia wale ambao wanaweza kusahauliwa. Kila kutaniko lina washiriki fulani walio dhaifu, wasiotoka katika hospitali za kutunzia wasiojiweza, au wenye udhaifu mwingine fulani. Kwa namna yenye kueleweka, ushiriki wao katika kutangaza ujumbe wa Ufalme unakuwa wenye mipaka kwa sababu ya hali zao. Labda wanapata nafasi ya kutoa ushahidi tu wakati wanapokuwa pamoja na wageni, na wagonjwa wengine, au na wale wanaotoa matunzo. Hata hivyo, lolote wanaloweza kufanya linaonwa kuwa mchango wenye thamani katika kazi ya kuhubiri kwa ujumla. (Mt. 25:15) Hata ikiwa wanatoa ushahidi kwa dakika 15 tu, hilo linapaswa kuripotiwa, nao wataendelea kuhesabiwa kuwa wahubiri wa Ufalme walio kawaida.
7 Wale ‘zawadi zikiwa wanaume’ wanajua hasa mahitaji ya kiroho ya ndugu zao wakati huu wa mwaka—majira ya Ukumbusho. Ni wakati wenye kufaa kama nini kwa wazee kufanya jitihada ya pekee ili kusaidia wale ambao wamekwenda kombo wapate tena furaha na amani ya akili vinavyotokana na ushirika wenye shauku katika kutaniko! Tunashangilia wakati tunapoona watu kama hao “ambao katika imani ni jamaa zetu” wakihudhuria mikutano ya kutaniko na kwenda katika huduma ili kuhakikisha tena kwamba wana imani katika dhabihu ya ukombozi.—Gal. 6:10; Luka 15:4-7; Yn. 10:11, 14.