Je, Unajitahidi Kusoma na Kuandika?
1 Kujifunza kwa kusudi la kupata ujuzi sahihi kuhusu Mungu na makusudi yake kunaomba kuwa na kiasi fulani cha elimu, hata ikiwa kiasi hicho ni kidogo. Wengi wametambua kwamba kujua kusoma na kuandika ni ufunguo wa kushiriki vya kutosha katika ibada ya Yehova Mungu. (Ufu. 1:3) Wengi wamejifunza kusoma na kuandika kupitia masomo ya kujifunza kusoma na kuandika yanayopangwa katika mengi ya makutaniko yetu. Mahali ambapo inapatikana, broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika (ay-SW) ndiyo inayotumiwa katika masomo hayo. Hiyo imeonekana kuwa njia yenye matokeo ya kujifunza kusoma na kuandika katika kipindi kilicho kifupi kwa kiasi fulani.—1 Tim. 4:13; Mt. 24:45.
2 Jinsi ya Kupanga Masomo ya Kujifunza Kusoma na Kuandika: Zifuatazo ni sehemu chache zinazochukuliwa katika kijitabu hicho kuhusu jinsi ya kupanga masomo ya kujifunza kusoma na kuandika: “Kama tu vile katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, wahubiri waliobatizwa, na wale wasiobatizwa wanaweza kujiandikisha katika masomo ya kujifunza kusoma na kuandika. Ikiwa wazee wanaamua kwamba ni jambo la lazima kuunda darasa moja au zaidi ili kufundisha kusoma na kuandika, wangepaswa kuchagua mtu mwenye uwezo ili kuyaendesha. . . . Kwa kawaida, akina ndugu wangepaswa kutimiza daraka la kufundisha. Hata hivyo, ikiwa hakuna ndugu aliye na uwezo wa kuendesha darasa hilo, dada mwenye uwezo anaweza kupewa mgawo wa kufanya hivyo. . . . Wazee wanaweza kumwomba dada aongoze darasa la akina dada na/au darasa la wanaume na wanawake vijana wasiobatizwa. Kwa kuwa dada anachukua mahali pa ndugu katika daraka lake la kufundisha, yeye angepaswa kuvaa kitambaa kichwani. Mahali ambapo hilo linawezekana, lingekuwa jambo lenye mafaa ikiwa masomo yangeendeshwa mara mbili au tatu kwa juma kusudi wanafunzi wafanye maendeleo ya haraka. Kati ya masomo, mwanafunzi atagawiwa kazi ya kufanya nyumbani, ambayo mwalimu atasahihisha mwanzoni mwa somo linalofuata. Masomo yanapaswa kufanywa wakati wenye kufaa kwa wanafunzi wengi zaidi. Makutaniko fulani hugawa madarasa katika vikundi vidogo-vidogo na kutoa masomo kabla ya Funzo la Kitabu la Kutaniko. Mengine hutenganisha madarasa na kufundisha wakati Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inapoendeshwa. Wakati na mahali pa masomo ya kutaniko ya kujifunza kusoma na kuandika huamuliwa na baraza la wazee katika kutaniko.”
3 Muumba wetu, Yehova Mungu, ametuumba tukiwa na uwezo wa ajabu wa kusoma na kuandika. Hata hivyo, ufundi huo mbalimbali haupatikani bila jitihada. Thawabu kubwa zaidi ya kujifunza kusoma na kuandika ni kuwa na uwezo wa kuchukua Neno la Mungu na kutii agizo hili la kimungu: “Utawaza [“soma,” NW] ndani yake muchana na usiku.”—Yos. 1:8.