Kisanduku Cha Maulizo
◼ Ni kiwango gani tunachopaswa kufuata kuhusu mavazi na kujipamba tunapotembelea makao ya Betheli na majengo ya ofisi za tawi?
Tunapotembelea Betheli, iwe kwamba ni kwa kusudi la kuona jinsi jengo hilo lilivyo au kuongea na washiriki wa familia ya Betheli, “mavazi yetu, kujipamba kwetu na mwenendo wetu umepasa uwe namna ileile tunayotazamiwa kuwa tunapohudhuria mikutano ya ibada kwenye Jumba la Ufalme.” (om-SW 131) Hata hivyo, imeonekana kwamba wanapotembelea ofisi za tawi, ndugu na dada fulani wanaelekea kupita kiasi kwa kuvaa kwa namna isiyojali. Hilo si jambo lenye kufaa tunapotembelea majengo hayo. Sura yetu inapaswa kuwa yenye kutengenezwa vizuri na yenye kiasi, ikionyesha adabu na heshima inayostahili watumishi wa Yehova Mungu.—1 Tim. 2:9, 10.
Hilo ni jambo la maana hasa tunapotembelea makao ya Betheli na majengo ya ofisi za tawi, kwa sababu yanavuta uangalifu wa watazamaji wengi wasio Mashahidi. Huenda watazamaji hao wakawa na maoni mbalimbali kuhusu watu wa Mungu na tengenezo lake kwa msingi wa yale wanayoona. Ni jambo lenye kufaa kuzungumza na wanafunzi wa Biblia na wengine wanaoweza kutembelea makao hayo ili kuwakumbusha umaana wa kuwa waangalifu kuhusu mavazi na kujipamba kunakofaa. Familia ya Betheli itashukuru mkifanya hivyo.
Tukiwa wahudumu Wakristo, tunapaswa kuwa waangalifu ili sura yetu isitoe sababu yoyote ya kukwaza. (2 Kor. 6:3, 4) Badala ya hivyo, kupitia utaratibu wetu wenye kufaa, acheni sikuzote ‘turembe fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote’.—Tito 2:10.