Kisanduku Cha Maulizo
◼ Tunapaswa kuvaa namna gani tunapotembelea majengo yenye kutumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova?
Ulimwenguni pote, Majumba ya Ufalme, Majumba ya Mikusanyiko, Betheli, na majengo ya tawi ni nafasi za pekee zenye kutumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Majengo hayo ni ya kawaida, safi, na yenye kutunzwa vizuri; na hivyo yanaonyesha heshima. Ni tofauti sana na jinsi tunavyoona mara nyingi katika ulimwengu wa Shetani. Ikiwa tunatembelea nafasi zinazotumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova, tunapaswa pia kutambuliwa kuwa watu wa Yehova, wanaofanya mapenzi yake.
Tukiwa Wakristo, “tunajipendekeza kuwa wahudumu wa Mungu” katika kila njia, kutia ndani namna yetu ya kuvaa na kujipamba kunakofaa na kwenye mpangilio muzuri. (2 Kor. 6:3, 4) Tunatazamiwa pia kuendelea kuwa na mwenendo unaofaa. Nyakati zote, kuvaa na kujipamba kwetu kunapaswa kuonyesha adabu na heshima inayostahili watumishi wa Yehova Mungu. Jambo hilo linastahili zaidi sana tunapotembelea majengo ya makao makuu huko New York na majengo ya tawi ulimwenguni pote.
Kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova kinazungumza kuhusu umaana wa kuvaa na kujipamba kunakofaa, kikitoa maelezo kuhusu uhitaji wa usafi wa kimwili, kuvaa kwa kiasi na kujipamba vizuri tunapoenda kwenye mahubiri na tunapohuzuria mikutano ya Kikristo. Kisha, kwenye ukurasa wa 139, fungu la 1, kinaeleza hivi: “Kumbuka, jina Betheli linamaanisha ‘Nyumba ya Mungu.’ Kwa hiyo, tunapaswa kuvalia, kujipamba, na kujiendesha kama tunavyofanya tunapohuzuria mikutano ya ibada katika Jumba la Ufalme.” Wahubiri wa Ufalme wanapaswa kufuata kanuni hii ya juu wanapotembelea Betheli, iwe wanaishi karibu karibu na Betheli ao wanatoka mbali. Kwa njia hiyo, mtu mwenye kutembelea Betheli anaonyesha shukrani na heshima yenye kufaa.—Zab. 29:2.
Mvalio wetu unapaswa kututambulisha kuwa wale “wanaodai kumheshimu Mungu.” (1 Tim. 2:10) Mvalio wenye kufaa na kujipamba vizuri vinaweza kusaidia wengine wawe na maoni mazuri kuhusu ibada ya kweli ya Yehova. Hata hivyo, imeonekana kwamba ndugu na dada fulani, wanapotembelea majengo yenye kutumiwa kwa ajili ya utumishi wa Yehova, wanavaa mavazi yenye kupita kiasi bila kujali, ya ovyoovyo, ao yenye kuonyesha sehemu fulani za mwili. Mavazi ya namna hiyo hayafai Wakristo kwa wakati wowote. Katika jambo hilo, kama vile katika sehemu zingine zote za maisha yetu ya Kikristo, tunataka kuheshimu kanuni za juu zinazofanya watu wa Mungu wawe tofauti na wale wa ulimwengu, wakifanya mambo yote kwa utukufu wa Mungu.—Rom. 12:2; 1 Kor. 10:31.
Kwa hiyo, unapotembelea makao makuu na majengo ya tawi huko New York ao majengo mengine ya tawi, iwe ulipanga safari yako kwa kusudi hilo ao uko katika mapumziko kwenye maeneo mengine yanayotembelewa na watu, unapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, mavazi yangu na kujipamba kwangu ni vyenye kiasi, safi na vyenye kuonyesha heshima kwa ajili ya majengo nitakayotembelea? Je, vinaonyesha heshima kwa Mungu ninayeabudu? Je, wengine watakengeushwa ao kuumizwa kwa sababu ya mvalio na kujipamba kwangu?’ Kupitia mvalio na kujipamba kwetu, siku zote na ‘tulipambe fundisho la Mwokozi wetu, Mungu, katika mambo yote’!—Tito 2:10.