Kisanduku Cha Maulizo
◼ Tunapaswa kulinda jambo gani akilini tunapotumia simu za mikononi?
Vyombo hivyo vinaweza kutuwezesha tupashane habari na wengine karibu mahali popote tunapopatikana. Ijapokuwa jambo hilo huenda likawa lenye mafaa, tunapaswa kuwa waangalifu tusiruhusu matumizi ya simu za mikononi pa wakati usiofaa yapunguze umaana wa huduma yetu au wa mikutano ya Kikristo. Jambo hilo linaweza kutokeaje?
Fikiria matokeo yanaweza kuwa nini ikiwa simu yetu ya mkononi inalia tunapokuwa tukishiriki katika huduma ya shambani tukitoa ushahidi. Mwenye nyumba atafikiri nini? Tutamwacha akiwa na maoni gani ikiwa tunasimamisha mazungumzo ili kujibu kwenye simu? Hatungependa kufanya jambo lolote ili kuzuia wengine wasisikilize ujumbe wa Ufalme. (2 Kor. 6:3) Kwa hiyo, ikiwa tunachukua simu ya mkononi, tunapaswa kuizima ili isitukatize au kukatiza wengine tunaposhiriki katika huduma ya shambani.
Namna gani tunapongojea wakati wengine wanapotoa ushahidi? Ikiwa tumepanga kipindi fulani cha wakati kwa ajili ya utumishi wa shambani, je, hatungalipaswa kukaza uangalifu wetu juu ya kazi hiyo? Ili kuheshimu utumishi wetu mtakatifu, tafadhali shughulikia mambo ya kibinafsi yasiyo ya lazima au faida za marafiki zako wakati mwingine. (Rom. 12:7) Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba hatuwezi kutumia simu ili kutoa ushahidi zaidi au kufanya mapatano kwa ajili ya kutoa ushahidi.
Ni lazima tuwe waangalifu hasa kuhusu kutumia simu za mikononi tunapoendesha gari, kwa kuwa utafiti fulani unaonyesha kwamba kufanya hivyo kunaongeza kwa kiasi kikubwa hatari ya kutukia kwa aksidenti. Tunapaswa kuheshimu kabisa sheria yoyote inayokataza matumizi ya simu za mikononi tunapoendesha gari.
Tunakuja kwenye mikutano ya Kikristo, mikusanyiko, na makusanyiko ili kumwabudu Yehova na kufundishwa naye. Je, kuthamini utakatifu wa matukio hayo hakungalipaswa kutuchochea tuzime simu za mikononi ili zisitukengeushe sisi au kuwakengeusha wengine? Ikiwa kuna jambo la haraka linalohitaji uangalifu wetu wa papo hapo, tunapaswa kulishughulikia nje ya mahali pa mkutano. Kwa upande mwingine, tunapaswa kushughulikia mambo ya kibinafsi na ya kimwili wakati mwingine tofauti na ule uliochaguliwa kwa ajili ya ibada.—1 Kor. 10:24.
Acheni jinsi tunavyotumia simu za mikononi na chombo kingine chochote cha kielektroniki ionyeshe kwamba tunafikiria wengine na kwamba tunathamini sana mambo ya kiroho.