Iweni Wenye Kuunganishwa Pamoja kwa Upatano
1 Je, unastaajabia mara nyingi jinsi mwili wa kibinadamu ulivyoumbwa kwa ufundi? (Zab. 139:14) Kila kiungo cha mwili kinatumika kwa upatano na viungo vingine. Neno la Mungu linafananisha kutaniko la Kikristo na mwili wenye viungo vyenye kutumika kwa upatano. Chini ya Kichwa, Kristo, washiriki wote wa kutaniko ni wenye ‘kuunganishwa pamoja kwa upatano na wenye kufanywa washirikiane kupitia kila kiungo ambacho hutoa kile kinachohitajiwa.’ (Efe. 4:16a) Hivyo, Yehova anaweza kutumia watu wake wenye umoja ili kutimiza mambo ya ajabu.
2 Washiriki wa kutaniko la karne ya kwanza walitenda “kwa umoja” katika kushughulikia mahitaji ya kiroho na ya kimwili ya kila mmoja. (Mdo. 2:44-47) Kwa msaada wa Yehova, walipambana na walishinda upinzani mkali kwa umoja. (Mdo. 4:24-31) Walitangaza ujumbe wa Ufalme popote walipokwenda, wakieneza habari njema katika ulimwengu uliojulikana wakati huo. (Kol. 1:23) Katika nyakati za kisasa, kutaniko la Kikristo limetimiza kwa umoja mambo hayo hayo kwa kiasi kikubwa hata zaidi. Ni mambo gani yanayochangia umoja huo?
3 Tunaunganishwa Kupitia Ufundishaji wa Kimungu: Ulimwenguni pote, tunaunganishwa kupitia ibada yetu. Hilo linawezekanaje? Tunatambua njia yenye kuonekana ya Yehova ya kutoa ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’ (Mt. 24:45) Tunathamini pia “zawadi zikiwa wanadamu” alizotoa ili kufundisha katika kutaniko. Kwa kuwa tunakubali kwa unyenyekevu maandalizi ya Yehova ya kutulisha kiroho, uelewevu wetu wa Neno la Mungu unaongezeka na unachochea ndani yetu tamaa tunayoshiriki sote ya kumwiga Yesu tukiwa wanafunzi wake. Tunapaswa kuendelea kujifunza Neno la Mungu, tukijitahidi kwa bidii “kuufikia umoja katika imani.” (Efe. 4:8, 11-13) Je, unachangia umoja wetu wa kiroho kwa kusoma Biblia kila siku?
4 Wenye Umoja Kupitia Ushirika wa Kikristo: Upendo unatuunganisha pamoja katika ushirikiano wa karibu kwenye mikutano ya Kikristo. Kwenye mikutano hiyo, ‘tunafikiriana.’ (Ebr. 10:24, 25) Hilo linahusisha kutazama zaidi ya sura ya nje na kupata kujua kikweli ndugu zetu, kuwaona kama vile Yehova anavyowaona, kuwa wenye thamani. (Hag. 2:7, NW, kielezi-chini.) Tunaposikiliza maneno yao ya imani, upendo wetu kwao unakomaa na umoja wetu unatiwa nguvu. Je, unajulikana kuwa mtu anayehudhuria kikawaida mikutano ya kutaniko?
5 Wafanyakazi Wenzetu Katika Shamba: Kuhubiri habari njema pamoja na waamini wenzetu kunatuunganisha katika kufanya mapenzi ya Mungu. Mtume Paulo alithamini ‘wafanyakazi wenzake kwa ajili ya ufalme wa Mungu.’ (Kol. 4:11) Kushiriki mambo yaliyoonwa, na kusaidiana tunapokuwa katika huduma kunatusaidia tutimize utume wetu wa Kikristo na kunatia nguvu kifungo chetu cha umoja.—Kol. 3:14.
6 Uvutano Wenye Kuunganisha wa Roho Takatifu: Tunapojitahidi kufanya mapenzi yake, Yehova anatupatia roho yake. Hiyo inatusaidia kupunguza hali za kutopatana na kukaa pamoja kwa umoja. (Zab. 133:1) Inatuchochea “kushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.” (Efe. 4:3) Kila mmoja wetu anaweza kuchangia upatano ulio kati ya watu wa Mungu kwa kuonyesha matunda ya roho katika kushughulikia wengine.—Gal. 5:22, 23.
7 Kutumikia pamoja kwa umoja chini ya ukichwa wa Kristo “hutokeza ukuzi wa mwili ili kujijenga huo wenyewe katika upendo.” (Efe. 4:16b) Kwa kuongezea, jambo hilo linamtukuza Yehova, “Mungu apaye amani.”—Rom. 16:20.