Onyesha Shukrani Yako
1 Ijapokuwa tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” tunazo sababu nyingi za kuwa wenye shukrani kwa Yehova. (2 Tim. 3:1) Tuko wenye shukrani hasa kwa sababu ya zawadi yenye thamani ya kumtoa Mwana wake kwa ajili yetu. (Yoh. 3:16) Zaidi ya hiyo, ijapokuwa wale walio katika dini ya uongo wana njaa ya kiroho, sisi tunafurahia chakula kingi cha kiroho. (Isa. 65:13) Sisi ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote na tunapewa pendeleo la pekee la kushiriki katika mpanuko wenye kusisimua wa ibada ya kweli. (Isa. 2:3, 4; 60:4-10, 22) Tunawezaje kuonyesha shukrani yetu kwa Yehova kwa ajili ya baraka anazomwaga juu yetu?—Kol. 3:15, 17.
2 Utumishi Wenye Furaha na Unaofanywa kwa Moyo Wote: Alipokuwa akizungumzia utoaji wa vitu vya kimwili, mtume Paulo aliandika: “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Kor. 9:7) Kanuni hii inatumika pia kuhusu utumishi wetu kwa Mungu. Shukrani inaonyeshwa katika shauku yetu kuelekea kweli, katika furaha yetu kwenye mikutano ya Kikristo, katika bidii yetu katika huduma ya shambani, na katika furaha tuliyo nayo katika kutimiza mapenzi ya Mungu.—Zab. 107:21, 22; 119:14; 122:1; Rom. 12:8, 11.
3 Katika Israeli ya kale, kuhusu matoleo fulani, ile Sheria haikuonyesha wazi kiasi cha kutoa. Kila mwabudu angeweza kuonyesha shukrani yake kwa kutoa “kulingana na baraka za Yehova Mungu” alizokuwa amepokea. (Kum. 16:16, 17) Hivyohivyo leo, moyo wenye shukrani utatuchochea kufanya kadiri hali zetu zinavyoturuhusu katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Mara nyingi miezi ya Agosti na Septemba inatoa nafasi zaidi ya kuonyesha shukrani yetu. Watu fulani wanafaidika na likizo kazini au shuleni ili kuongeza wakati wanaopitisha katika utumishi wa shambani, na hata wanafanya upainia msaidizi. Je, unaweza kupanua huduma yako mnamo Agosti na Septemba?
4 Tujawe Kabisa na Shukrani: Njia ya maana zaidi ya kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova ni katika sala. (1 The. 5:17, 18) Neno la Mungu linatusihi ‘tujawe kabisa na imani katika kutoa shukrani.’ (Kol. 2:7) Hata wakati tunapokuwa na shughuli nyingi au chini ya mkazo, tunapaswa kila siku kutia shukrani katika sala zetu za kila siku. (Flp. 4:6) Kwa kweli, kupitia huduma na sala zetu vilevile, na ‘tuwe matajiri kwa maonyesho mengi ya shukrani kwa Mungu.’—2 Kor. 9:12.