Uvumilivu Unathawabishwa
1 “Nanyi kwa kuvumilia mtajipatia nafsi zenu.” (Luka 21:19) Maneno hayo ambayo ni sehemu ya unabii wa Yesu kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo,” yanaonyesha wazi kwamba ili kulinda utimilifu au ushikamanifu wetu, tunapaswa kuwa tayari kupambana na majaribu mengi. Lakini kwa nguvu ya Yehova, kila mmoja wetu anaweza ‘kuvumilia mpaka mwisho’ na ‘kuokolewa.’—Mt. 24:3, 13; Flp. 4:13.
2 Mateso, matatizo ya afya, magumu ya kifedha, na taabu ya kihisia-moyo vinaweza kufanya kila siku iwe ngumu sana. Hata hivyo, hatupaswi kusahau kamwe kwamba Shetani ni mwenye kujaribu kuvunja utimilifu wetu kwa Yehova. Kila siku inayopita tukiwa washikamanifu kwa Baba yetu, tunashiriki katika kutoa jibu kwa Mdhihaki anayeshakia utimilifu wetu. Ni jambo lenye kuthawabisha kama nini kujua kwamba tunapopambana na majaribu “machozi” yetu hayasahauliwi! Ni yenye thamani kwa Yehova, na utimilifu wetu unafanya moyo wake kushangilia!—Zab. 56:8; Met. 27:11.
3 Kusafishwa Kupitia Majaribu: Taabu inaweza kufunua udhaifu wa imani au kosa la mtu, kama vile kiburi au kukosa subira. Badala ya kujaribu kuepuka au kumaliza majaribu kwa njia zisizo za kimaandiko, tunapaswa kufuata shauri la Neno la Mungu linalosema “acheni uvumilivu ukamilishe kazi yake.” Kwa nini? Kwa kuwa kuvumilia majaribu kwa uaminifu kunatusaidia kuwa “kamili na timamu katika mambo yote.” (Yak. 1:2-4) Uvumilivu unaweza kutusaidia tukuze sifa zenye thamani, kama vile usawaziko, hisia-mwenzi, na rehema.—Rom. 12:15.
4 Sifa Iliyojaribiwa ya Imani: Tunapovumilia majaribu, tunapata sifa iliyojaribiwa ya imani ambayo ina thamani kubwa machoni pa Mungu. (1 Pet. 1:6, 7) Imani hiyo inatutolea vifaa vinavyotusaidia tubaki imara katika kipindi cha majaribu ya wakati ujao. Zaidi ya hilo, tunaweza kujisikia kuwa tunakubaliwa na Mungu, na hilo linatia tumaini letu nguvu, na kulifanya liwe halisi zaidi kwetu.—Rom. 5:3-5
5 Thawabu kubwa ya uvumilivu inakaziwa kwenye Yakobo 1:12, inayosema: “Mwenye furaha ni mtu anayeendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima.” Kwa hiyo, na tubaki imara katika ujitoaji wetu kwa Yehova, tukiwa hakika kwamba atathawabisha kwa wingi “wale wanaoendelea kumpenda.”