Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 5: Kukadiria Kiasi cha Habari ya Kujifunza
1 Alipokuwa akifundisha, Yesu alifikiria uwezo wa wanafunzi wake, kwa kusema nao “kadiri walivyoweza kusikiliza.” (Marko 4:33; Yoh. 16:12) Kwa njia hiyohiyo, walimu wa Neno la Mungu leo wanahitaji kukadiria kiasi cha habari ya kujifunza kwenye funzo la Biblia. Kiasi cha habari ya kujifunza kitategemea uwezo na hali za mwalimu na mwanafunzi.
2 Kujenga Imani Thabiti: Kwa wanafunzi fulani itahitaji kujifunza nao habari moja mara mbili au mara tatu ili waelewe, wakati ambapo kwa wanafunzi wengine itahitaji kujifunza habari hiyohiyo mara moja tu ili kuielewa bila magumu. Ni jambo la maana sana kusaidia mwanafunzi aelewe habari waziwazi kuliko kujifunza habari nyingi katika wakati mfupi. Kila mwanafunzi anahitaji msingi thabiti katika Neno la Mungu kwa ajili ya imani yake mpya.—Met. 4:7; Rom. 12:2.
3 Unapoongoza funzo la Biblia kila juma, tumia wakati wowote unaohitajiwa ili kusaidia mwanafunzi aelewe na kukubali yale anayojifunza kutoka Neno la Mungu. Epuka kwenda haraka zaidi ili mwanafunzi asikose kufaidika kikamili na habari kuhusu kweli anazojifunza. Chukua wakati wa kutosha ili kukazia mambo makuu na kuchunguza maandiko ya msingi ambayo yanategemeza mambo mnayojifunza.—2 Tim. 3:16, 17.
4 Kushikamana na Habari Mnayojifunza: Huku tukiepuka kwenda harakaharaka na funzo, ni lazima pia tuepuke kukengeushwa. Ikiwa mwanafunzi anaelekea kusemea sana mambo yake ya kibinafsi, tunaweza kufanya mpango ili kuzungumzia mambo hayo baada ya funzo.—Mhu. 3:1.
5 Kwa upande mwingine, shauku yetu wenyewe kuhusu kweli inaweza kuwa tatizo, inaweza kutufanya tuwe wenye kuzungumza zaidi wakati wa funzo. (Zab. 145:6, 7) Wakati fulani, mfano au jambo lililoonwa linaweza kutajirisha funzo, lakini hatungependa mambo hayo yawe mengi mno au marefu, kiasi kwamba yazuie mwanafunzi kutwaa ujuzi sahihi wa mafundisho ya Biblia ya msingi.
6 Kwa kukadiria kiasi cha habari ya kujifunza kwenye kila funzo, tunasaidia wanafunzi wa Biblia ‘kutembea katika nuru ya Yehova.’—Isa. 2:5.