Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 6: Wakati Mwanafunzi Anapotokeza Ulizo
1 Wakati funzo la Biblia linapoanzishwa vizuri, kwa kawaida ni vizuri zaidi kuchunguza mafundisho ya Biblia katika njia yenye utaratibu badala ya kurukaruka habari. Hilo linasaidia mwanafunzi ajenge msingi wa ujuzi sahihi na kuendelea kiroho. (Kol. 1:9, 10) Hata hivyo, mara nyingi, wanafunzi wanatokeza maulizo kuhusu habari mbalimbali wakati wa funzo. Namna gani tunaweza kuyashughulikia?
2 Tumia Ufahamu: Kwa kawaida, maulizo yanayohusiana na habari mnayojifunza yanapaswa kujibiwa hapohapo. Ikiwa ulizo litajibiwa baadaye katika kichapo mnachojifunza, huenda ikatosha kumwonyesha tu kwamba jambo hilo linazungumziwa katika sura fulani ya kitabu. Lakini, ikiwa ulizo halihusu habari mnayojifunza au litaomba kufanyiwa utafiti ili kujibu inavyostahili, ingekuwa vema kulichunguza baada ya funzo au wakati mwingine. Wahubiri wengine wameona kwamba kuandika ulizo hilo kunahakikishia mwanafunzi kwamba ulizo lake linachukuliwa kwa uzito na wakati huohuo kunasaidia funzo lisikengeushwe.
3 Mafundisho mengi ya Biblia yanaelezwa tu kwa kifupi katika vichapo vyetu vya funzo. Tufanye nini ikiwa mwanafunzi ana magumu ya kukubali fundisho fulani au anashikamana kwa nguvu na fundisho fulani la uwongo? Ingekuwa jambo lenye faida kuchunguza habari ya ziada ambayo inazungumzia kwa ukamili yale ambayo Biblia inasema kuhusu jambo hilo. Ikiwa bado mwanafunzi hasadiki, mnaweza kuacha jambo hilo pembeni ili kulizungumzia wakati mwingine na hivyo kuendelea na funzo lenu la kawaida. (Yoh. 16:12) Kadiri anavyoongeza ujuzi wake wa Biblia na kuendelea kiroho, huenda akafikia kuelewa fundisho hilo la Biblia.
4 Uwe Mwenye Kiasi: Ikiwa hauna uhakika kuhusu jibu la ulizo, epuka mtego wa kujaribu kutoa maoni yako. (2 Tim. 2:15; 1 Pet. 4:11) Eleza kwamba utafanya utafiti kuhusu jambo hilo na kuleta jibu utakaporudi. Unaweza hata kutumia nafasi hiyo ili kufundisha mwanafunzi jinsi ya kufanya utafiti. Umwonyeshe hatua kwa hatua jinsi ya kutumia vyombo mbalimbali vya utafiti vinavyotolewa na tengenezo la Yehova. Katika njia hiyo, hatimaye atakuwa na uwezo wa kupata majibu kwa maulizo yake mwenyewe.—Mdo. 17:11.