Endelea Kuhubiri
1 Tunaishi nyakati za hatari. Mapigano ya wenyewe kwa wenyewe, vita vya kikabila, misiba ya asili, na matukio mengine yenye kuogopesha ni mambo ya kawaida. Sasa kuliko wakati wowote ule, familia ya wanadamu inahitaji habari njema. Hata hivyo, kutojali mambo ya kiroho kunaenea. Katika maeneo fulani, inaweza kuwa vigumu kupata watu nyumbani na hata vigumu sana kupata watu watakaotusikiliza au wanaopenda kujifunza Biblia. Hata hivyo, ni jambo la maana kwamba tuendelee kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu uliosimamishwa.—Mt. 24:14.
2 Upendo kwa Watu: Kazi yetu ya kuhubiri inaonyesha upendo wa Yehova kwa watu. “Hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9; Ezek. 33:11) Kwa hiyo, kama Yesu alivyosema, yeye aliagiza kwamba “katika mataifa yote lazima habari njema ihubiriwe kwanza.” (Mk. 13:10) Mungu anaomba watu wageuke kwake na kuepuka hukumu inayojia ulimwengu wa Shetani. (Yoeli 2:28, 29, 32; Zef. 2:2, 3) Je, sisi si wenye shukrani kwamba Yehova ametutolea nafasi hiyo?—1 Tim. 1:12, 13.
3 Ripoti ya ulimwenguni pote inaonyesha kwamba mnamo mwaka wa utumishi 2004, wastani ya mafunzo ya Biblia 6,085,387 yaliongozwa kila mwezi, na wastani wa karibu wanafunzi wapya 5,000 walibatizwa kila juma! Wengine kati ya wapya hao waliojitoa wakfu walipatikana kwa sababu Yehova alibariki jitihada za kuendelea za wahubiri waliojitahidi kusema na kila mtu katika maeneo waliyogawiwa. Hilo limetokeza furaha kubwa katika makutaniko, na ni pendeleo kuwa mfanyakazi mwenzi wa Mungu katika kazi hii yenye kuokoa uhai!—1 Kor. 3:5, 6, 9.
4 Kusifu Jina la Mungu: Tunaendelea kuhubiri ili kumsifu Yehova waziwazi na kulitakasa jina lake mbele ya wanadamu wote. (Ebr. 13:15) Shetani amepotosha “dunia nzima inayokaliwa” kwa kufanya watu waamini kwamba Mungu hana nguvu ya kutatua matatizo ya wanadamu, kwamba yeye ni asiyejali mateso ya wanadamu, au kwamba yeye hayupo tu. (Ufu. 12:9) Kupitia kazi yetu ya kuhubiri, tunatetea kweli kuhusu Baba yetu mtukufu wa mbinguni. Na tuendelee kusifu jina lake—sasa na milele.—Zab. 145:1, 2.