Tuendelee kuhubiri!
1 Ni mapenzi ya Mungu kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Kwa sababu hiyo, yeye ametutolea mgawo wa kuhubiri habari njema. (Mt. 24:14) Ikiwa tunatambua kwa nini tunapaswa kuendelea kuhubiri, kivunja-moyo chochote au jambo lolote linaloweza kutupumbazisha ambalo tunakutana nalo halitatuzuia kutenda.
2 Kwa nini tuendelee? Kuna vipumbaza-fikira vingi katika ulimwengu ambavyo vinafanya watu wasahau au kutochukua kwa uzito yale tunayowaambia. Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kuwakumbusha ujumbe wa Mungu wa wokovu. (Mt. 24:38, 39) Kwa kuongezea, hali katika maisha ya watu ni zenye kubadilika sikuzote. Hata hali za ulimwengu zinaweza kubadilika kikamili katika usiku mmoja. (1 Kor. 7:31) Kesho, juma lijalo, au mwezi ujao, watu tunaohubiria wanaweza kukabiliana na matatizo au mahangaiko mapya ambayo yanawafanya wafikirie kwa uzito habari njema tunayowaletea. Je, wewe si mwenye shukrani kuona kwamba Shahidi aliyekuletea kweli aliendelea kuja?
3 Ili kuiga rehema ya Mungu: Kwa uvumilivu, Yehova ameruhusu wakati upite kabla ya kutekeleza hukumu juu ya waovu. Kupitia sisi ameendelea kuita watu wenye moyo mnyofu wamwendee na kuokolewa. (2 Pet. 3:9) Tutakuwa wenye hatia ya damu ikiwa hatutangazi ujumbe wenye rehema wa Mungu kwa watu na kuwaonya kuhusu kutekelezwa kunakokuja kwa hukumu ya Mungu juu ya wale wote wasioacha njia zao mbaya. (Eze. 33:1-11) Ingawa mahubiri yetu hayapokewi vizuri sikuzote, hatupaswi kamwe kulegea katika kufanya kila jitihada ili kusaidia watu wanyofu wathamini rehema kubwa ya Mungu.—Mdo. 20:26, 27; Rom. 12:11.
4 Ili kuonyesha upendo wetu: Ni Yehova Mungu, kupitia Yesu Kristo, ndiye aliamuru kwamba habari njema ihubiriwe katika dunia yote. (Mt. 28:19, 20) Hata wakati watu wanapokataa kusikiliza, tunayo nafasi ya kuonyesha upendo wetu na ujitoaji wetu kwa Mungu kwa kuendelea kufanya yale yaliyo sawa.—1 Yn. 5:3.
5 Acheni tuwe na nia thabiti ya kuendelea kuhubiri! Acheni tufanye hivyo kwa bidii wakati bado ingali “siku ya wokovu” ya Yehova.—2 Kor. 6:2.