Kwa Nini Uendelee Kuhubiri?
1 Je, kazi ya kuhubiri Ufalme imekuwa ikifanywa katika mtaa wenu kwa muda mrefu? (Mt. 24:14) Ikiwa ni hivyo, huenda ukahisi kwamba eneo la kutaniko limekwisha kutembelewa vya kutosha. Sasa wakati unapohubiri, labda watu wengi unaokutana nao wanaonekana kuwa wasiojali ujumbe wa Ufalme. Ijapokuwa hivyo, ona yale yanayosemwa kuhusu wanafunzi wa kweli wa Yesu kwenye ukurasa wa 141 wa kitabu Unabii wa Isaya II: “Mahali fulani fulani, huenda matokeo ya huduma yao yakaonekana kuwa si kitu yakilinganishwa na kiasi cha kazi na jitihada wanazofanya. Hata hivyo, wao huvumilia.” Lakini kwa nini uendelee kuhubiri?
2 Kumbuka Yeremia: Kuvumilia kwetu katika kazi ya kuhubiri hakupaswi kutegemea jambo la kwamba watu wanatusikiliza au hawatusikilizi. Yeremia alihubiri kwa miaka 40 katika eneo lilelile, ijapokuwa watu wachache sana ndio waliomsikiliza na kwamba wengi walipinga ujumbe wake. Kwa nini Yeremia alivumilia? Kwa sababu alikuwa akifanya kazi ambayo Mungu alimwamuru afanye, na kwa sababu ujuzi wake kuhusu kile ambacho kingetukia wakati ujao ulimlazimisha aendelee kusema kwa ujasiri.—Yer. 1:17; 20:9.
3 Hali yetu inafanana na hiyo. Yesu “alituagiza sisi tuwahubiri watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa hakimu wa walio hai na wafu.” (Mdo. 10:42) Ujumbe tunaopeleka ni jambo la uzima au la kifo kwa wale wanaousikia. Watu watahukumiwa kulingana na jinsi walivyoitikia habari njema. Kwa sababu hiyo, daraka letu ni kufanya tu kama vile tulivyoamuriwa. Hata wakati watu wanapokataa kusikiliza, hilo hututolea nafasi ya kuonyesha kina cha upendo wetu kuwaelekea na ujitoaji wetu kwa Yehova kwa kudumu katika kufanya yale tunayopaswa kufanya. Lakini kuna mengi zaidi.
4 Tunafaidika: Kufanya mapenzi ya Mungu, bila kujali itikio la watu katika eneo, kunatupatia amani ya ndani, kutosheka, na furaha, mambo ambayo hayawezi kupatikana kwa njia nyingine. (Zab. 40:8) Maisha yetu yanapata maana na kusudi la kweli. Kwa kadiri tunavyoshiriki katika huduma, kwa kadiri hiyohiyo mioyo yetu na akili zetu zinakazwa juu ya lile tumaini na furaha ya kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu. Kutafakari ahadi hizo za Kimaandiko kunaongeza hali yetu ya kiroho na kunatia nguvu uhusiano wetu pamoja na Yehova.
5 Hata ikiwa hatuoni matokeo ya mara moja katika kazi yetu ya kuhubiri, huenda mbegu ya kweli ikawa imepandwa katika moyo wa mtu, mbegu itakayochipuka pa wakati wenye kufaa machoni pa Yehova. (Yn. 6:44; 1 Kor. 3:6) Hakuna mmoja kati yetu anayejua ni watu wengine wangapi watakaojifunza kuhusu Ufalme kupitia jitihada za watu wa Yehova, iwe mahali penu au ulimwenguni pote.
6 Kuliko wakati mwingine wowote, tunapaswa kusikiliza agizo la Yesu: “Fulizeni kutazama, fulizeni kuwa macho, kwa maana hamjui ni lini ulio wakati uliowekwa rasmi. Lakini lile niwaambialo nyinyi nawaambia wote, Fulizeni kulinda.” (Mk. 13:33, 37) Kwa hiyo, basi, acheni sote tuendelee kutangaza habari njema ya Ufalme, tukifurahisha moyo wa Yehova kadiri tunavyoshiriki katika kutakasa jina lake kuu na lililo takatifu.