Sitawisha Uwezo wa Kufikiri Pamoja na Wengine
1 Hotuba ya mtume Paulo aliyofanya katika sinagogi huko Antiokia ya Pisidia, kama inavyoandikwa kwenye Matendo 13:16-41, inatoa mfano bora kuhusu jinsi ya kufikiri na wengine. Paulo alifikiria malezi na namna ya kufikiri ya wasikilizaji wake na akapatanisha utoaji wake wa habari njema na hali hiyo. Tunapochunguza simulizi hili, tufikirie jinsi tunavyoweza kufanya hivyohivyo katika huduma yetu.
2 Tafuta Mambo Mnayokubaliana: Ingawa ujumbe wa Paulo ulizungumzia sana daraka la Yesu katika kutimiza kusudi la Mungu, Paulo hakuanza hotuba yake na jambo hilo. Badala yake, yeye alisema kuhusu jambo fulani ambalo walikubaliana na wasikilizaji wake ambao wengi kati ya hao walikuwa Wayahudi—yaani, historia ya Wayahudi. (Mdo. 13:16-22) Hivyohivyo, tutakuwa wenye matokeo zaidi katika kufikia mioyo ya wengine ikiwa tunajaribu kupata mambo ambayo tunakubaliana. Hilo linaweza kuomba kwamba tuwatie moyo kwa kuwauliza maulizo yenye busara ili watoe mawazo yao na kuwasikiliza kwa uangalifu ili kutambua kwa kweli mambo yaliyo ya maana kwao.
3 Katika kuzungumzia historia ya Wayahudi, Paulo aliwakumbusha wasikilizaji wake kuhusu ahadi ya Mungu ya kutokeza Mwokozi kutoka kizazi cha Daudi. Lakini, Wayahudi wengi walikuwa wenye kungojea shujaa wa kijeshi ambaye angewakomboa kutoka utawala wa Waroma na kuinua taifa la Wayahudi juu ya mataifa mengine yote. Bila shaka, walijua kwamba viongozi wa dini ya Kiyahudi huko Yerusalemu walimkataa Yesu, na kumtoa kwa Waroma wenye mamlaka ili auawe. Paulo angewasadikisha namna gani kwamba Huyo alikuwa Masihi aliyeahidiwa?
4 Patanisha Utoaji Wako na Hali: Akijua namna ya kufikiri ya wasikilizaji wake, Paulo alitumia Maandiko ili kufikiri pamoja nao juu ya mambo ambayo tayari walikuwa wamekubali. Kwa mfano, alijulisha kwamba Yesu alikuwa mzao wa Daudi na kwamba ni yeye aliyetambulishwa na Yohana Mbatizaji, aliyeonwa sana kuwa nabii wa Mungu. (Mdo.13:23-25) Paulo alionyesha kwamba kwa kumkataa Yesu na kumhukumia kifo, viongozi wa kidini walikuwa ‘wametimiza mambo yaliyosemwa na Manabii.’ (Mdo. 13:26-28) Zaidi ya hiyo, alieleza kwamba kulikuwa na mashahidi ambao walikuwa wameona jinsi Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu, na akavuta uangalifu kwenye Maandiko ambayo wasikilizaji wake Wayahudi walijua na ambayo yalikuwa yametimizwa wakati wa ufufuo wa Yesu.—Mdo. 13:29-37.
5 Kwa upande mwingine, alipokuwa akisema na wasikilizaji Wagiriki katika Areopago huko Athene, Paulo alitumia utoaji tofauti. (Mdo. 17:22-31) Lakini alitoa ujumbe uleule wa msingi, na katika hali zote mbili hizo jitihada zake zilitokeza matokeo mazuri. (Mdo. 13:42, 43; 17:34) Vivyo hivyo leo, tutazidi kuwa wenye matokeo katika huduma yetu ikiwa tunajaribu kupata mambo ya kukubaliana pamoja na wasikilizaji na ikiwa tunapatanisha utoaji wetu kulingana na malezi yao pia na namna yao ya kufikiri.
[Maulizo ya Funzo]
1. Ni simulizi gani la Biblia tutakalochunguza, na kwa nini?
2. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Paulo alivyoanza hotuba yake?
3. Ni nini kilichofanya iwe vigumu kwa wasikilizaji wa Paulo kukubali kwamba Yesu alikuwa Masihi aliyeahidiwa?
4. Paulo aliwezaje kufikiri kwa ufundi na wasikilizaji wake Wayahudi?
5. (a) Paulo alipatanishaje utoaji wake kulingana na hali alipokuwa akizungumza na wasikilizaji Wagiriki? (b) Tunawezaje kuiga mfano wa Paulo tunapohubiri katika eneo letu?