Onyesha Kupendezwa Kibinafsi na Wengine—Kwa Kuwatazama Usoni
1 Tunapohubiri mahali watu wengi wanapopatikana na pia nyumba kwa nyumba, mara nyingi tunatazama watu usoni kabla ya kuzungumza nao. Katika muda huo mfupi, tunaweza kutambua kupitia ishara zao za uso namna wanavyojisikia kuhusu kuwapo kwetu na hata ikiwa wao ni wenye furaha au hapana. Nao pia wanaweza kutambua mambo mengi kutuhusu. Mwanamke mmoja alisema hivi baada ya Shahidi kumtembelea: ‘Jambo ninalokumbuka kuhusu sura yake yenye furaha ilikuwa ile amani. Nilivutiwa sana.’ Hilo lilifungulia mwanamke huyo njia ya kusikiliza habari njema.
2 Kutazama wengine usoni ni njia yenye matokeo inayotuwezesha kutolea watu ushahidi tunapohubiri barabarani au mahali pengine ambapo watu wengi wanapatikana. Ndugu mmoja anawatazama usoni watu wanaomkaribia. Anapowatazama usoni, anacheka kidogo na kisha anawatolea magazeti. Kwa kufanya hivyo, anakuwa na mazungumzo mengi yenye kufurahisha na anatoa vichapo vingi.
3 Tambua Hisia za Wengine: Kutazama watu usoni kutatusaidia kutambua hisia zao. Kwa mfano, ikiwa mtu fulani hatuelewi vizuri au hakubaliani na jambo ambalo tumesema, kwa kawaida hilo litaonekana kwenye uso wake. Ikiwa mtu ana shughuli nyingi au ikiwa anakosa uvumilivu, tutatambua hivyo kwa kutazama ishara zake za uso. Hivyo tunaweza kupatanisha utoaji wetu na hali au kuufupisha. Kuelewa hisia za watu wengine ni njia bora inayoonyesha kwamba tunapendezwa nao.
4 Unyoofu na Usadikisho: Katika jamii nyingi, kutazama mtu machoni ni uthibitisho wa kwamba wewe ni mnyoofu. Ona jinsi Yesu alivyojibu wanafunzi wake walipomwuliza: “Ni nani kwa kweli anayeweza kuokolewa?” Biblia inasema: “Akiwatazama usoni, Yesu akawaambia: ‘Kwa wanadamu jambo hilo haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.’” (Mt. 19:25, 26) Bila shaka usadikisho ambao Yesu alionyesha kupitia macho yake uliongeza uzito wa maneno yake. Vivyo hivyo, kutazama watu usoni kwa njia inayofaa kutatusaidia kueleza ujumbe wa Ufalme kwa unyoofu na usadikisho.—2 Kor. 2:17; 1 The. 1:5.