“Endeleeni Kufanya Hivi kwa Kunikumbuka Mimi” Kifo cha Yesu Kitaazimishwa Tarehe 2 mwezi wa 4
1 Mamilioni ya watu ulimwenguni pote watakusanyika tarehe 2 mwezi wa 4, 2007, ili kuazimisha kifo cha Yesu cha zabihu. Yesu alikufa kwa sababu alikuwa mteteaji wa enzi kuu ya Baba yake wa mbinguni. Kwa kifo chake, Yesu alionyesha wazi kwamba Shetani ni mwongo aliposema kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu kwa sababu ya faida zao wenyewe. (Ayu. 2:1-5) Chakula cha Bwana cha Jioni kinatukumbusha pia kwamba, kupitia kifo chake akiwa mwanadamu mkamilifu na asiye na zambi, Yesu ‘alitoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mt. 20:28) Kwa hiyo, Yesu aliwaamuru wanafunzi wake hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (Luka 22:19) Je, kuonyesha shukrani kwa ajili ya zawadi hiyo bora ya Mungu kunakuchochea kuanza kujitayarisha ili kuazimisha tendo hilo kubwa zaidi la upendo?—Yoh. 3:16.
2 Tayarisha Moyo Wako: Kwa kufikiria mambo ambayo yalitukia katika kila mojawapo ya siku za mwisho-mwisho za maisha ya Yesu akiwa mwanadamu, tunaweza kutayarisha mioyo yetu kwa ajili ya kuazimisha Ukumbusho huo. (Ezra 7:10) Ili kutusaidia kuhusu jambo hilo, programu ya pekee ya usomaji wa Biblia inapatikana katika kitabu Kuyachunguza Maandiko—2007 na kwenye kalenda ya 2007. Programu hiyo ya usomaji inalingana sana na siku ambamo matukio yanayohusiana na kifo cha Yesu yalitukia, kulingana na kalenda tunayotumia leo. Siku na tarehe mbalimbali zinazotajwa katika masimulizi ya Biblia, zinategemea kalenda ya Wayahudi, inayohesabu siku kuanzia kutua kwa jua mpaka kutua kwa jua kwa siku inayofuata. Tofauti hiyo katika namna ya kuhesabu siku ilifuatwa na inaonyeshwa wazi katika programu ya usomaji wa Biblia kwa ajili ya Ukumbusho. Kujikumbusha habari hizo kupitia usomaji wa Biblia na kufikiri sana katika sala kuhusu upendo mwingi sana wa Mungu, kutatusaidia tupate faida nyingi sana kupitia mwazimisho wa Ukumbusho.
3 Alika Wengine Wahuzurie: Nyongeza ya Huduma Yetu ya Ufalme ya mwezi wa 2 ilitangaza kampanye ya pekee ya kualika watu kwenye tukio hilo la maana. Je, umepanga kushiriki kabisa katika kampanye hiyo? Je, umeandika kwenye karatasi watu unaofahamiana nao ambao utaalika, na umeanza kuonana nao? Fanya mipango ya kufika mbele ya wakati jioni hiyo ya Ukumbusho ili kukaribisha wale ambao ulialika na pia waalikwa wengine wenye kupendezwa. Unaweza kukaa pamoja nao na kuwatolea Biblia na kitabu cha nyimbo ikiwa hawana. Uwajulishe kwa washiriki wengine wa kutaniko. Mwishoni mwa programu, unaweza kujibu maulizo yao. Uwaalike waje kuhuzuria hotuba ya pekee ya watu wote itakayotolewa tarehe 15 mwezi wa 4. Zaidi sana wazee ndio watahakikisha kwamba wale ambao wamejiunga na kutaniko, lakini wameacha kutenda, wamepata karatasi ya kuwaalika waje kuhuzuria Ukumbusho na hotuba ya pekee.
4 Saidia Wapya Wanaopendezwa na Wale Ambao Wameacha Kutenda Ili Wafanye Maendeleo: Msemaji atakayetoa hotuba ya Ukumbusho atafasiria namna tunavyojifunza Biblia na watu na pia atawatia moyo wale wenye kupendezwa waendelee kujifunza kumhusu Yehova. Unaweza kutumia mambo atakayoeleza ili kusaidia wale ambao umealika wakubali kujifunza mengi kumhusu Yehova. Ikiwa hawajaanza kujifunza Biblia, kisha Ukumbusho uwatembelee bila kukawia na uwaonyeshe jinsi funzo la Biblia linavyofanywa. Ili wafanye maendeleo ya kiroho, watahitaji kuhuzuria mikutano ya kutaniko. (Ebr. 10:24, 25) Ili kutimiza hilo, uwatie moyo waanze kuhuzuria mikutano kwa ukawaida. Wazee watafanya mipango ya kutembelea Wakristo ambao wameacha kutenda waliohuzuria Ukumbusho na kuwasaidia wafikirie sana mawazo yaliyozungumziwa katika hotuba. Jambo hilo linaweza kuwasaidia ili warudilie tena utendaji wao katika kutaniko.
5 Kuazimisha Ukumbusho kunatutolea nafasi ya kufikiri sana kuhusu kile ambacho Yehova na Yesu wamefanya kwa ajili yetu. Kufikiri hivyo kunatufanya tumpende sana Yehova na Yesu na kunatusaidia tuwe na mwenendo mzuri. (2 Kor. 5:14, 15; 1 Yoh. 4:11) Sasa, huu ndio wakati wa kuanza kujitayarisha na kutayarisha pia wale wanaopendezwa na tukio hilo la maana, wakati ambapo ‘tunatangaza kifo cha Bwana.’—1 Kor. 11:26.
[Maulizo ya Funzo]
1. Kwa nini Siku ya Kwanza tarehe 2 mwezi wa 4, 2007, ni siku ya maana sana?
2. Namna gani tunaweza kutayarisha mioyo yetu kwa ajili ya Ukumbusho?
3. Namna gani tunaweza kusaidia wenye kupendezwa na wale ambao wameacha kutenda ili wapate faida kutokana na Ukumbusho?
4. Namna gani tunaweza kusaidia watu ili wazidi kufanya maendeleo ya kiroho kisha mwazimisho wa Ukumbusho?
5. Ni faida gani ambazo tunaweza kupata kwa kuazimisha Ukumbusho?