Kazi Yetu ya Kuhubiri Inaonyesha Kwamba Tunampenda Mungu
1. Upendo kwa Mungu ulimchochea Yesu afanye nini?
1 Upendo ulimchochea Yesu atimize kazi yake ya kuhubiri. Kila sehemu ya kazi yake ya kuhubiri ilihakikisha kabisa kwamba anampenda Yehova. Yesu alisema hivi: “Kusudi ulimwengu ujue kwamba ninampenda Baba, kama vile Baba amenipa amri kufanya, ndivyo ninavyofanya.” (Yoh. 14:31) Kwa kuwa tunafuata mfano wa Yesu, sisi pia tuna pendeleo la kuonyesha kwamba tunampenda Mungu sana kupitia kazi yetu ya kuhubiri.—Mt. 22:37; Efe. 5:1, 2.
2. Namna gani upendo wetu kwa Yehova unatuchochea kuhubiri?
2 “Jina Lako Litakaswe”: Tunapotumia kwa bidii kila nafasi ya kuzungumza na wengine kuhusu Yehova na Ufalme wake, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu, na hivyo tunashiriki katika kutakasa jina lake. (Zab. 83:18; Ezek. 36:23; Mt. 6:9) Kama Yesu, kupitia kazi yetu ya kuhubiri tunaendelea kuonyesha kwamba tunampenda Yehova kabisa na kwamba tunataka jina lake litakaswe na mapenzi yake yatendeke.—Mt. 26:39.
3. Ni katika njia gani, upendo wetu kwa Yehova unatusaidia kushinda vizuizi?
3 Upendo Unatusaidia Kushinda Vizuizi: Kumpenda Yehova kunatusaidia kushinda vizuizi vyote. (1 Kor. 13:4, 7) Yesu alikutana na hali mbalimbali ambazo zingemzuia asitimize kazi yake ya kuhubiri. Hata hivyo, alipokutana na vizuizi, upendo wake kwa Yehova na tamaa yake ya kufanya mapenzi Yake, vilimsaidia ashinde vizuizi hivyo. (Mk. 3:21; 1 Pet. 2:18-23) Sisi pia tunapatwa na magumu mengi, lakini upendo wetu kwa Mungu unaweza kutusaidia tushinde magumu hayo. Kwa kufuata kabisa mfano wa Kristo, tunaweza kuwa hakika kwamba hakuna kitu chochote kinachoweza kutuzuia kutimiza kazi yetu ya kuhubiri. Ijapokuwa kupingwa na watu wa familia, afya mbaya, kuzeeka, ao watu hawapendezwi na ujumbe wetu, mambo hayo hayawezi kutuzuia kuonyesha upendo wetu kwa Yehova kwa kutimiza kazi yetu ya kuhubiri kadiri tuwezavyo.
4. Upendo wetu kwa Yehova unatutolea pendeleo gani?
4 Upendo una nguvu, na sisi tunabarikiwa kwa kuwa tuna uwezo wa kuonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa nafsi yetu yote katika kazi yetu ya kuhubiri. (1 Kor. 13:13) Kwa kuwa tunakaribia sana wakati ambapo jina la Yehova litatakaswa mara moja kwa wakati wote, ‘upendo wenu na uwe mwingi hata zaidi na zaidi.’—Flp. 1:9; Mt. 22:36-38.