Je, Unaweza Kujikaza Kufahamiana na Mwenzi wa Dada ao wa Ndugu Asiye Shahidi?
1. Kwa nini Wakristo walio na waume ao wake wasio Mashahidi si wao tu wanaotaka kuwasaidia waume ao wake zao wakubali kweli?
1 Katika kutaniko lenu, je, kuna wahubiri fulani ambao wenzi wao si Mashahidi? Ikiwa ni hivyo, bila shaka wahubiri hao wanataka waume ao wake zao wajiunge nao katika ibada ya kweli. Lakini si wao tu wanaotamani kuwaona wenzi wao wakipendezwa na kweli. Kama Mungu, kutaniko nzima linataka “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Namna gani tunaweza kujikaza kufahamiana na mume wa dada ao muke wa ndugu asiye Shahidi?
2. Kwa nini ni vizuri kuwa na utambuzi ili kumsaidia mwenzi wa dada ao mwenzi wa ndugu asiye Shahidi?
2 Kwanza, tujikaze kuona mambo kama vile watu hao wasio Mashahidi wanavyoyaona. Wenzi hao wasio Mashahidi wanapenda familia zao na wanajikaza kuwa wenzi wa ndoa na wazazi wazuri. Labda wanaamini sana mafundisho ya dini zao yaliyo tofauti na yetu. Ao labda hawajui mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova; wanajua tu yale ambayo rafiki zao wasiotujua vizuri ao wanaotuchukia wamewambia. Wengine hawafurahi kuona waume ao wake zao wakichukua wakati waliokuwa wakipitisha pamoja katika familia na kuutumia kwa ajili ya mambo ya ibada. Kuwa na utambuzi kutatusaidia kumtendea vizuri na kwa heshima mume wa dada yetu ao muke wa ndugu yetu na kuepuka kuwa na wasiwasi mwingi tunapozungumza naye.—Met. 16:20-23.
3. Ni nini iliyo njia nzuri zaidi ili kumvuta kwenye kweli mwenzi asiye Shahidi?
3 Tupendezwe Naye: Njia nzuri zaidi ya kumvuta kwenye kweli, kwanza ni kupitia matendo yetu si kwa kumhubiria. (1 Pet. 3:1, 2) Kwa hiyo, kupendezwa naye ni jambo la maana sana. Dada katika kutaniko wanaweza kupendezwa na wake wa ndugu zetu, na ndugu wanaweza kufanya vivyo hivyo kuelekea waume wa dada zetu. Namna gani?
4. Namna gani tunaweza kuonyesha kupendezwa na mume wa dada ao muke wa ndugu asiye Shahidi?
4 Ikiwa haujazungumza na mwenzi wa ndugu asiye Shahidi, labda unaweza kuzungumza kwanza na mume ao muke wake Mkristo mbele ya kufanya hivyo. Usivunjike moyo ikiwa mwanzoni mume wa dada ao muke wa ndugu yetu anaonekana kuwa hajali. Kuzungumza naye kwa njia ya kirafiki na kupendezwa naye kunaweza kumchochea awe na maoni mazuri kuhusu Mashahidi wa Yehova. (Rom. 12:20) Wakristo fulani wenye kukomaa kiroho wamealika mume wa dada ao muke wa ndugu yetu pamoja na familia yake ili kula chakula pamoja, wamefanya hivyo ili kufahamiana naye vizuri na kumsaidia aondoe chuki yoyote ambayo anaweza kuwa nayo kuhusu Mashahidi wa Yehova. Wamezungumzia mambo yanayompendeza kuliko kuzungumzia mambo ya kiroho. Baadaye, wanaweza kuzungumzia mambo ya kiroho wakati mume wa dada ao muke wa ndugu yetu anakuwa na maoni mazuri kuhusu Mashahidi wa Yehova. Mume wa dada ao muke wa ndugu yetu anaweza kukubali kuhuzuria mkutano mmoja kati ya mikutano yetu ili kuona mambo ambayo mume ao muke wake anajifunza, hasa kwa kuwa tayari anafahamiana na watu fulani katika kutaniko. Hata ikiwa hakubali kujifunza kweli, tunaweza kumpongeza kwa sababu anamtegemeza mume ao muke wake aliye Shahidi.
5. Namna gani wazee wanaweza kujikaza kufahamiana na mwenzi fulani asiye Shahidi?
5 Wazee hasa wanapaswa kujikaza kufahamiana na wenzi wasio Mashahidi na kuwa tayari kuwatolea ushahidi kila wakati nafasi inapopatikana. Anapokuwa katika hospitali ao anapopambana na matatizo makali ya afya, mume wa dada ao muke wa ndugu yetu ambaye hakupendezwa na mazungumzo yenye kutegemea Biblia anaweza kusikiliza wakati ndugu ao dada fulani anamtia moyo. Familia ambayo mwenzi mmoja wa ndoa si Shahidi inapopatwa na tatizo, kama vile kufiwa na mutu wa familia, wazee wanaweza kumwalika mume ao muke asiye Shahidi awe hapo wanapokuja kufariji familia.
6. Kuna sababu gani zinazotufanya tujikaze kufahamiana na wenzi wasio Mashahidi ili kuwasaidia wakubali kweli?
6 Wazia furaha ambayo ndugu ao dada wa kutaniko letu anaweza kuwa nayo ikiwa mume ao muke wake anakubali kweli na kuwa Shahidi wa Yehova! Tukio kama hilo lenye kupendeza linamfurahisha sana Yehova pia, malaika, na ndugu na dada wengine katika kutaniko. (Luka 15:7, 10) Hata ikiwa mwanzoni mume wa dada ao muke wa ndugu yetu anaonekana kuwa hajali, tunaweza kuendelea kuwa na furaha kwa kuwa bidii ambayo tunaendelea kufanya ili kumsaidia inampendeza Yehova, ambaye “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Pet. 3:9.
[Wazo la fungu kwenye ukurasa wa 6]
Njia nzuri zaidi ya kumvuta kwenye kweli, kwanza ni kupitia matendo yetu si kwa kumhubiria