Tuige Mufano wa Manabii—Sefania
1. Sefania alifanya kazi ya kutoa unabii katika hali gani, na sababu gani yeye ni mufano muzuri kwetu leo?
1 Ilikuwa katika miaka ya 650 hivi mbele ya kuzaliwa kwa Yesu, na ibada ya Baali ilikuwa ikifanywa waziwazi katika Yuda. Mufalme mubaya Amoni ameuawa hivi karibuni, na Mufalme kijana Yosia anatawala sasa. (2 Nyak. 33:21–34:1) Wakati huo, Yehova alimuchagua Sefania ili kutangaza Ujumbe wa hukumu Yake. Hata kama Sefania alikuwa mutu wa familia ya kifalme ya Yuda, hakupunguza uzito wa ujumbe wa hukumu ya Yehova juu ya viongozi wa Yuda. (Sef. 1:1; 3:1-4) Vivyo hivyo, sisi pia tunajikaza kuiga bidii ya Sefania na haturuhusu uhusiano wetu na watu wa jamaa utuzuie kumuabudu Yehova. (Mt. 10:34-37) Sefania alitangaza ujumbe gani na matokeo yalikuwa nini?
2. Tunapaswa kufanya nini ili tufikie kufichwa katika siku ya hasira ya Yehova?
2 Umutafute Yehova: Ni Yehova peke yake ndiye anaweza kuwaokoa watu katika siku ya hasira yake. Kwa hiyo, Sefania aliwashauri watu wa Yuda wamutafute Yehova, watafute uadilifu ao haki, na watafute upole bila kuchelewa. (Sef. 2:2, 3) Shauri hilo ni la maana pia leo. Kama Sefania, tunatia wengine moyo wamutafute Yehova, lakini sisi pia tunapaswa kumutafuta, tuazimie kabisa tusiwe hata kidogo ‘wanaorudi nyuma wasimufuate Yehova.’ (Sef. 1:6) Tunamutafuta Yehova kwa kujifunza kwa uangalifu Neno lake na kusali ili kupata muongozo wake. Tunatafuta uadilifu ao haki kwa kuishi tukiwa na mwenendo safi. Tunatafuta upole kwa kujikaza kutii na kuwa tayari kufuata muongozo wa tengenezo la Yehova.
3. Sababu gani tunapaswa kuendelea kuwa na maoni yanayofaa katika mahubiri?
3 Matokeo Mazuri: Ujumbe wa hukumu wa Sefania ulichochea watu fulani katika Yuda, zaidi sana kijana Yosia, aliyeanza kumutafuta Yehova wakati alikuwa angali kijana. Baadaye, Yosia alianza kazi kubwa ya kuondoa ibada ya sanamu katika inchi. (2 Nyak. 34:2-5) Leo, hata ikiwa mbegu fulani za Ufalme zinaanguka kando ya barabara, kwenye udongo yenye majiwe, katikati ya miiba, lakini zingine pia zinaanguka juu ya udongo muzuri na kutoa matunda. (Mt. 13:18-23) Tuko hakika kwamba Yehova ataendelea kutubariki tunapojikaza kuwa na mengi ya kufanya katika kupanda kila mahali mbegu za Ufalme—Zab. 126:6.
4. Sababu gani tunapaswa kuendelea kumungojea Yehova?
4 Watu fulani katika Yuda waliwaza kwamba Yehova hatafanya jambo lolote. Lakini, Yehova aliwahakikishia wote kwamba siku yake kubwa ilikuwa inakaribia. (Sef. 1:12, 14) Wale ambao wangekimbilia kwake ndiyo tu wangeokolewa. (Sef. 3:12, 17) Tunapoendelea kumungojea Yehova, acheni tupate furaha katika kumutumikia Mungu wetu mukubwa kwa umoja pamoja na waabudu wenzetu!—Sef. 3:8, 9.