Yehova Ananiona Namna Gani?
1. Sababu gani Biblia inafananishwa na kioo?
1 Mara ngapi unajiangalia katika kioo? Wengi kati yetu wanajiangalia kila siku katika kioo kwa sababu kufanya hivyo kunawasaidia waone mahali kunahitaji kutengenezwa kwenye mwili wao. Biblia imefananishwa na kioo. Kusoma Neno la Mungu kunatusaidia kuona moyo wetu ao mutu wetu wa ndani, mutu ambaye Yehova anaona. (1 Sam. 16:7; Yak. 1:22-24) Neno la Mungu linaweza “kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Namna gani kusoma na kutafakari Neno la Mungu kila siku kunaweza kutusaidia kuona mahali ambapo tunapaswa kutengeneza ili tuwe wahubiri wazuri zaidi?—Zab. 1:1-3.
2. Namna gani Biblia inaweza kutusaidia tujichunguze?
2 Tumia Biblia Kama Kioo: Habari zinazopatikana katika Biblia kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova zinatufundisha sifa zinazomupendeza Mungu. Kwa mufano, Daudi alionyesha bidii kwa ajili ya jina la Mungu. (1 Sam. 17:45, 46) Isaya alijitoa ili kuhubiri kwa bidii katika eneo ngumu. (Isa. 6:8, 9) Kwa sababu Yesu alimupenda sana Baba yake wa mbinguni, jambo hilo lilimuchochea afurahie sana kazi ya kuhubiri kuliko kuiona kuwa muzigo wenye kuchokesha. (Yohana 4:34) Wakristo wa kwanza-kwanza walihubiri kwa bidii, walimutegemea Yehova, na kuendelea kuhubiri bila kuchoka. (Mdo. 5:41, 42; 2 Kor. 4:1; 2 Tim. 4:17) Kutafakari juu ya mifano hiyo kutatusaidia tujichunguze ili tufanye vizuri zaidi kazi yetu ya kuhubiri.
3. Sababu gani tusichelewe kufanya mabadiliko yanayohitajiwa?
3 Ondoa Uchafu Ambao Umeona: Bila shaka, hakuna faida ya kujiangalia katika kioo bila kuondoa uchafu ambao tumeona. Tunaweza kumuomba Yehova atusaidie tujichunguze na kufanya mabadiliko yanayohitajiwa. (Zab. 139:23, 24; Luka 11:13) Kwa sababu wakati unaobakia umepunguka na uzima wa watu uko katika hatari, tunapaswa kufanya mabadiliko yanayohitajiwa bila kuchelewa.—1 Kor. 7:29; 1 Tim. 4:16.
4. Mutu anayechunguza Neno la Mungu na kutenda kulingana na yale ambayo ameona, anapata faida gani?
4 Mutu wetu wa ndani—ambaye Yehova anachunguza—ni wa maana sana kuliko sura yetu ya inje. (1 Pet. 3:3, 4) Mutu anayechunguza ndani ya Neno la Mungu na kisha anatenda kulingana na yale ambayo ameona, anapata faida gani? Kwa sababu ‘amekuwa, si musikiaji musahaulifu, bali mutendaji wa kazi, atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.’ (Yak. 1:25) Bila shaka tutakuwa wenye furaha na wahubiri wazuri sana kwa sababu ‘tunatoa kama vioo murudisho wa utukufu wa Yehova.’—2 Kor. 3:18.