HABARI YA KUJIFUNZA YA 36
Watu wa Yehova Wanapenda Haki
“Wenye furaha ni wale wenye njaa na kiu ya haki.”—MT. 5:6.
WIMBO 9 Yehova Ni Mufalme Wetu!
KIFUPI YA HABARIa
1. Yosefu alipata jaribu gani, na alitenda namna gani?
YOSEFU, mwana wa Yakobo, alipata jaribu ya nguvu. Mwanamuke moya alimuambia, “Lala na mimi.” Alikuwa bibi ya bwana wake, Potifa. Yosefu alikatala ile ombi. Leo, pengine mutu anaweza kujiuliza, ‘Juu ya nini Yosefu alikatala kulala na ule mwanamuke?’ Potifa hakukuwa pale. Zaidi ya ile, Yosefu alikuwa mutumwa mu ile nyumba; na ule mwanamuke angemutesa juu alikatala kulala naye. Lakini, Yosefu aliendelea kukatala. Juu ya nini? Alisema hivi: “Ninaweza namna gani kufanya ubaya huu mukubwa na kwa kweli nimutendee Mungu zambi?”—Mwa. 39:7-12.
2. Yosefu alijua namna gani kama kufanya uzinifu ni kumutendea Mungu zambi?
2 Yosefu alijua namna gani kama Mungu angeona uzinifu kuwa “ubaya . . . mukubwa”? Sheria ya Musa, yenye ilikuwa na amri hii yenye kuwa wazi, “Haupaswe kufanya uzinifu,” ilikuwa haiyatolewa. Ilitolewa kisha miaka mia mbili hivi. (Kut. 20:14) Lakini, Yosefu alimujua Yehova muzuri na alijua kama Yehova hangekubali uzinifu. Kwa mufano, Yosefu alijua muzuri kama Yehova alianzisha ndoa juu ikuwe kati ya mwanaume moya na mwanamuke moya. Na pengine alisikiaka namna mara mbili Yehova alilinda tate yake Sara wakati alikuwa mu hatari ya kubakwa. Vilevile, Mungu alilinda Rebeka, bibi ya Isaka. (Mwa. 2:24; 12:14-20; 20:2-7; 26:6-11) Wakati Yosefu alikuwa nafikiri juu ya ile mambo, alifikia kutambua mambo yenye Mungu anaona kuwa sawa na yenye Mungu anaona kuwa makosa. Juu Yosefu alimupenda Mungu wake, alipenda pia kanuni za haki za Yehova, na alikuwa tayari kuzitumikisha.
3. Tutazungumuzia nini mu hii habari?
3 Unapendaka haki? Bila shaka. Lakini, juu siye wote hatukamilike, na kama hatuko waangalifu, tunaweza kuanza kuwa na mawazo ya ulimwengu juu ya haki. (Isa. 5:20; Ro. 12:2) Njo maana, tutazungumuzia haki ni nini, na faida yenye tunapata wakati tunapenda haki. Kisha, tutazungumuzia mambo tatu yenye tunaweza kufanya juu tupende sana kanuni za haki za Yehova.
HAKI NI NINI?
4. Watu wengi wanawazaka kama mutu mwenye haki ni mutu wa namna gani?
4 Watu wengi wanawazaka kama mutu mwenye haki ni mutu mwenye kiburi, mwenye kuchambua-chambua wengine, ao mwenye kujiona kuwa mwenye haki. Lakini, Mungu hapendake mutu wa vile. Wakati Yesu alikuwa ku dunia, alilaumu kwa ukali viongozi wa dini juu walikuwa najiwekea kanuni zao za haki. (Muh. 7:16; Lu. 16:15) Haki ya kweli iko tofauti kabisa na kujiona kuwa mwenye haki.
5. Kulingana na Biblia, haki ni nini? Leta mifano.
5 Haki ni sifa ya muzuri. Kwa kifupi, haki ni kufanya mambo yenye kuwa sawa mu macho ya Yehova Mungu. Mu Biblia, maneno yenye inatumiwa juu ya kuzungumuzia “haki” inaleta wazo ya kuishi kulingana na kanuni za juu sana, ni kusema, kanuni za Yehova. Kwa mufano, Yehova aliamuru kama wafanyabiashara wanapaswa kutumia “jiwe la kupimia . . . la haki.” (Kum. 25:15) Kwa hiyo, Mukristo mwenye anapenda kuwa mwenye haki mu macho ya Mungu atajikaza kuwa mwenye haki mu mambo yake yote ya biashara. Mutu mwenye haki anachukiaka wakati anaona mutu anatendewa bila haki. Na “ili kumupendeza [Yehova] kwa ukamili,” mutu mwenye haki kabisa anafikiriaka namna Yehova ataona maamuzi yenye anataka kukamata.—Kol. 1:10.
6. Juu ya nini Yehova tu njo anaweza kutuambia kama hii ni kosa na hii haiko kosa? (Isaya 55:8, 9)
6 Biblia inaonyesha kama Yehova njo chanzo ya haki. Njo maana, anaitwa “makao ya haki.” (Yer. 50:7) Juu Yehova njo Muumbaji wetu, yeye tu njo anaweza kutuambia kama hii ni kosa na hii haiko kosa. Juu Yehova ni mukamilifu, mawazo yake juu ya mambo yenye kuwa sawa na mambo yenye kuwa makosa iko tofauti sana na mawazo yetu yenye mara mingi inachochewa na hali yetu ya kutokamilika na zambi. (Mez. 14:12; soma Isaya 55:8, 9.) Lakini, juu tuliumbwa kwa mufano wa Mungu, tunaweza kuishi kulingana na kanuni zake za haki. (Mwa. 1:27) Na tunapendaka kufanya vile. Juu tunamupenda Baba yetu, ile inatuchocheaka kumuiga kadiri tunaweza—Efe. 5:1.
7. Juu ya nini tuko na lazima ya kanuni zenye kutegemeka? Leta mifano.
7 Tunapata faida wakati tunatii kanuni za haki za Yehova. Unajua sababu? Wazia mambo inaweza kuwa namna gani kama kila banke inajiwekea kanuni zake kuhusu samani ya makuta ao kama kila kompanyi ya ujenzi inafuata kanuni zake kuhusu vipimo vya ujenzi. Ile italeta muvurugo. Na kama wanganga hawafuate kanuni zenye zinapaswa kufuatwa wakati ya kutunza wagonjwa, ile inaweza kufanya wagonjwa fulani wakufe. Kusema kweli, kanuni zenye kutegemeka ni ulinzi. Vilevile, kanuni za haki za Mungu zinatulinda.
8. Wale wenye wanajikaza kuishi kulingana na kanuni za haki watapata baraka gani?
8 Yehova anabariki wale wenye wanajikaza kuishi kulingana na kanuni zake. Anaahidi hivi: “Wenye haki watariti dunia, na wataishi milele juu yake.” (Zb. 37:29) Unaweza kuwazia namna wanadamu watakuwa wenye umoja, amani, na furaha wakati kila mutu ataishi kulingana na kanuni za Yehova? Yehova anapenda ukuwe na maisha ya vile. Kila mumoja wetu iko kabisa na sababu ya kupenda haki! Tunaweza kufanya nini juu tupende sana sifa ya haki? Tuone mambo tatu yenye tunaweza kufanya.
MAMBO YA KUFANYA JUU UPENDE SANA KANUNI ZA HAKI ZA YEHOVA
9. Unaweza kufanya nini juu upende haki?
9 Jambo ya 1: Upende ule mwenye anaweka kanuni za haki. Juu tupende haki, tunapaswa kupenda sana ule mwenye anaweka kanuni za mema na mabaya. Kadiri tunamupenda Yehova zaidi, ni vile tutapenda kuisha kulingana na kanuni zake za haki. Kwa mufano, kama Adamu na Eva wangemupenda Yehova, wangetii sheria yake ya haki.—Mwa. 3:1-6, 16-19.
10. Abrahamu alifanya nini juu afikie kuelewa muzuri zaidi mawazo ya Yehova?
10 Hatupendi kufanya kosa ileile yenye Adamu na Eva walifanyaka. Tunaweza kuepuka kufanya vile kama tunaendelea kujifunza juu ya Yehova, kama tunafurahia sifa zake, na kujikaza kuelewa mawazo yake. Kama tunafanya vile, tutamupenda Yehova zaidi. Fikiria mufano wa Abrahamu. Alimupenda kabisa Yehova. Hata wakati ilikuwa nguvu kwake kuelewa maamuzi ya Yehova, Abrahamu hakuasi. Kuliko kufanya vile, alijikaza kumujua Yehova muzuri zaidi. Kwa mufano, wakati Abrahamu alijua kama Yehova ameamua kuharibu Sodoma na Gomora, ku mwanzo aliogopa kama “muamuzi wa dunia yote” angeharibu wanye haki pamoya na waovu. Abrahamu aliona kama ile haiwezekane. Njo maana, kwa unyenyekevu, alimuuliza Yehova maulizo mingi. Yehova alimujibia kwa uvumilivu. Ku mwisho, Abrahamu alifikia kuelewa kama Yehova anachunguzaka moyo wa kila mwanadamu na kama hawezi hata kidogo kupatia malipizi mwenye hana kosa pamoya na mwenye iko na kosa.—Mwa. 18:20-32.
11. Abrahamu alifanya nini juu ya kuonyesha kama alimupenda Yehova na alimutumainia?
11 Abrahamu aliguswa sana na mazungumuzo yenye alifanya na Yehova kuhusu muji wa Sodoma na Gomora. Bila shaka, Abrahamu alifikia kumupenda na kumuheshimia Yehova hata zaidi kuliko zamani. Lakini kisha miaka fulani, imani ya Abrahamu ilijaribiwa sana. Yehova alimuomba atoe mwana wake mupendwa Isaka kuwa zabihu. Lakini sasa, Abrahamu alikuwa amemujua Mungu muzuri zaidi. Kwa hiyo, hakukuwa tena na maulizo ya kumuuliza Mungu. Abrahamu alianza tu kufanya mambo yenye Yehova alimuomba. Sasa, wazia namna moyo wake ulikuwa na huzuni wakati alikuwa najitayarisha kufanya mambo yenye Yehova alimuomba! Abrahamu alipaswa kuwaza sana juu ya mambo yenye alikuwa amejifunza juu ya Yehova. Alijua kama Yehova hawezi hata kidogo kufanya jambo yoyote yenye inakosa haki ao yenye inakosa upendo. Kulingana na mutume Paulo, Abrahamu alifikiria kama Yehova angefufua mwana wake mupendwa Isaka. (Ebr. 11:17-19) Alikuwa na sababu ya kufikiri vile juu Yehova alikuwa ameahidi kama Isaka angekuwa baba wa taifa, na kufikia ile wakati, Isaka hakukuwa na watoto. Abrahamu alimupenda Yehova. Kwa hiyo, alitumainia kama Yehova angetenda kwa haki. Kwa imani, alitii hata kama ilikuwa nguvu kufanya vile.—Mwa. 22:1-12.
12. Namna gani tunaweza kumuiga Abrahamu? (Zaburi 73:28)
12 Namna gani tunaweza kumuiga Abrahamu? Kama Abrahamu, tunapaswa kuendelea kujifunza kuhusu Yehova. Kama tunafanya vile, tutamukaribia zaidi na tutamupenda hata zaidi. (Soma Zaburi 73:28.) Zamiri yetu itazoezwa na itaanza kutuongoza kulingana na mawazo ya Yehova. (Ebr. 5:14) Na wakati mutu fulani atajaribu kutuchochea kufanya jambo ya mubaya, tutakatala. Hatutafikiria hata kidogo kufanya jambo yenye inaweza kumuhuzunisha Baba yetu na kuharibisha urafiki wetu naye. Lakini, tunaweza tena kufanya nini juu ya kuonyesha kama tunapenda haki?
13. Tunapaswa kufanya nini juu tufuatilie haki? (Mezali 15:9)
13 Jambo ya 2: Ujikaze kupenda haki kila siku. Kama tunapenda mwili wetu ukuwe na misuli ya nguvu, tunapaswa kujikaza sana kufanya mazoezi kila siku. Vilevile, inaomba kujikaza sana juu tufikie kupenda kanuni za haki za Yehova. Ile ni jambo yenye tunapaswa kufanya kila siku. Yehova iko na usawaziko, na hatazamie hata kidogo tufanye mambo yenye inapita nguvu yetu. (Zb. 103:14) Anatuhakikishia kama “anapenda mutu mwenye kufuatilia haki.” (Soma Mezali 15:9.) Kama tuko nafuatilia muradi fulani mu kazi ya Yehova, tunaendeleaka kujikaza mupaka tuufikie. Vilevile, tunapaswa kujikaza ili kufuatilia haki. Na Yehova atatusaidia kwa uvumilivu kufanya maendeleo, kufanya mabadiliko kadiri siku zinapita.—Zb. 84:5, 7.
14. “Bamba la kifua la haki” inafananisha nini, na inatusaidia namna gani?
14 Kwa upendo, Yehova anatukumbusha kama kutenda kwa haki haiko muzigo muzito. (1 Yo. 5:3) Lakini, ni ulinzi, na tuko na lazima ya ulinzi kila siku. Fikiria silaha za kiroho zenye mutume Paulo alizungumuzia. (Efe. 6:14-18) Unakumbuka sehemu yenye inapaswa kulinda moyo wa Mukristo? Ni “bamba la kifua la haki,” yenye inafananisha kanuni za haki za Yehova. Sawa vile bamba ya kifua ilikuwa nalinda moyo halisi, kanuni za haki za Yehova zinalinda moyo wetu wa mufano, ni kusema, mutu wetu wa ndani. Njo maana, ni jambo ya maana sana tusikose kuvala bamba la kifua la haki!—Mez. 4:23.
15. Namna gani unaweza kuvala bamba la kifua la haki?
15 Namna gani unaweza kuvala bamba la kifua la haki? Unaweza kufanya vile kwa kutenda kulingana na kanuni za Mungu mu maamuzi yako ya kila siku. Wakati unaamua kuzungumuza kuhusu jambo fulani, muziki wenye utasikiliza, mambo ya kujifurahisha yenye utaangalia, ao vitabu vyenye utasoma, ujiulize kwanza hivi: ‘Itaingiza mambo gani mu moyo wangu? Yehova anaikubali? Ao inachochea mutu apende mambo yenye Yehova anasema kama haiko ya haki, sawa vile uasherati, jeuri, pupa, kutafuta tu faida zake mwenyewe?’ (Flp. 4:8) Kama maamuzi yenye unakamata inapatana na mapenzi ya Yehova, utakuwa uko naacha kanuni zake za haki zilinde moyo wako.
Haki yako, ni kusema, matendo yako ya haki inaweza kuwa “kama mawimbi ya bahari” (Ona fungu ya 16-17)
16-17. Isaya 48:18 inatumia mufano gani wenye unatuhakikishia kama tunawea kuishi kulingana na kanuni za haki za Yehova kila siku?
16 Ulishakajiuliza kama unaweza kuishi kulingana na kanuni za haki za Yehova kila siku, kila mwaka? Fikiria mufano wenye Yehova anatumia, mu Isaya 48:18. (Soma.) Yehova anaahidi kama haki yetu, ni kusema matendo yetu ya haki, inaweza kuwa “kama mawimbi ya bahari.” Wazia uko nasimama pembeni ya bahari kubwa, na uko naangalia namna mawimbi inaendelea kujipiga kwenye sehemu ya pembeni ya bahari, ingine kisha ingine. Wakati uko fasi ya vile yenye utulivu, unaweza kuogopa kama kuko siku yenye ile mawimbi itaachaka kufanya vile? Hapana! Unajua kama ile mawimbi imeendelea kujipiga kwenye sehemu ya pembeni ya bahari kwa miaka mingi sana, na itaendelea tu kufanya vile.
17 Haki yako, ni kusema, matendo yako ya haki inaweza kuwa sawa vile tu ile mawimbi ya bahari! Namna gani? Wakati unataka kukamata uamuzi fulani, fikiria mambo yenye Yehova anapenda ufanye. Kisha, uifanye. Hata kama inaweza kuwa nguvu kukamata uamuzi fulani, sikuzote Baba yako mwenye upendo atakupatia nguvu na atakusaidia uendelee kuishi kila siku kulingana na kanuni zake za haki.—Isa. 40:29-31.
18. Juu ya nini tunapaswa kuepuka kuhukumu kulingana na kanuni zetu?
18 Jambo ya 3: Mambo ya hukumu, uiachie Yehova. Wakati tuko najikaza kuishi kulingana na kanuni za haki za Yehova, tunapaswa kuepuka kuhukumu wengine na kujiona kuwa wenye haki. Kuliko kuzarau wengine na kufanya sawa vile tuko na haki ya kuhukumu wengine kulingana na kanuni zetu, tunapaswa kukumbuka kama Yehova njo “muamuzi wa dunia yote.” (Mwa. 18:25) Yehova hatupatie kazi ya kuhukumu wengine. Yesu alituambia hivi: “Muache kuhukumu ili musihukumiwe.”—Mt. 7:1.b
19. Namna gani Yosefu alionyesha kama alitumainia hukumu ya Yehova?
19 Tufikirie tena mufano wa Yosefu, mwanaume mwenye haki. Aliepuka kuhukumu wengine, hata wale wenye walimutendeaka mubaya. Ndugu zake walimutendeaka mubaya, wakamuuzisha mu utumwa, na wakasadikisha baba yao kama Yosefu alikuwa amekufa. Kisha miaka fulani, Yosefu aliungana tena na familia yake. Yosefu, mwenye ile wakati alikuwa mutawala mwenye nguvu, angeweza kuhukumu ndugu zake kwa ukali na kutafuta kulipiza kisasi. Ndugu za Yosefu waliogopa kama anaweza kufanya vile, hata kama walihuzunikia kabisa mambo yenye walifanyaka. Lakini, Yosefu aliwahikikishia hivi: “Musiogope. Je, mimi niko pahali pa Mungu?” (Mwa. 37:18-20, 27, 28, 31-35; 50:15-21) Kwa unyenyekevu, Yosefu alitambua kama Yehova njo alikuwa na haki ya kuhukumu ndugu zake.
20-21. Namna gani tunaweza kuepuka kujiona kuwa wenye haki?
20 Sawa vile Yosefu, mambo ya hukumu, tuiachie Yehova. Kwa mufano, tusijifanye sawa vile tunajua mambo yenye kuchochea ndugu na dada zetu watende kwa njia fulani. Hatuwezi kujua mambo yenye iko mu moyo wa mutu; ni “Yehova [tu njo] anachunguzaka nia.” (Mez. 16:2) Anapenda watu wa namna zote, wa desturi, na hali zote za maisha. Tena, Yehova anatutia moyo ‘tufungue mioyo yetu wazi.’ (2 Ko. 6:13) Tunapaswa kupenda ndugu na dada zetu wote, hapana kuwahukumu.
21 Hatupaswe pia kuhukumu wenye hawako Mashahidi. (1 Ti. 2:3, 4) Ulishakahukumu mutu wa familia yako mwenye haiko Shahidi, kwa kusema, “Huyu hatakuwaka Shahidi wa Yehova”? Ile ni kimbelembele, ni kujiona kuwa mwenye haki. Yehova angali napatia “wanadamu wote kila mahali” nafasi ya kutubu. (Mdo. 17:30) Kila mara usisahau kama kujiona kuwa mwenye haki ni kukosa haki.
22. Juu ya nini unaazimia kupenda kanuni za haki za Yehova?
22 Kupenda kanuni za haki za Yehova kutatusaidia tukuwe na furaha, kutachochea wengine watukaribie, na wamukaribie Mungu wetu. Tusiache basi hata kidogo kuwa na “njaa na kiu ya haki.” (Mt. 5:6) Ukuwe hakika kama Yehova anaona bidii yako na anafurahia namna uko najikaza kufanya mambo yenye kuwa sawa. Hii dunia inaendelea kuzama mu matendo ya kukosa haki. Lakini, usiogope! Sikuzote ukumbuke kama “Yehova anapenda wenye haki.”—Zb. 146:8.
WIMBO 139 Wazia Uko mu Dunia Mupya
a Mu hii dunia ya mubaya, ni nguvu kupata watu wenye kupenda haki. Lakini leo, kuko mamilioni ya watu wenye wanapenda haki. Bila shaka uko kati yao. Unajikaza kuishi kulingana na kanuni za haki juu unamupenda Yehova, na juu Yehova anapenda haki. Tunaweza kufanya nini juu tupende sana sifa ya haki? Mu hii habari, tutaona haki ni nini, na faida yenye tunapata wakati tunapenda haki. Tutaona pia mambo yenye tunaweza kufanya juu tupende sana sifa ya haki.
b Wakati fulani, wazee wanapaswa kuhukumu mambo yenye inahusu zambi nzito na kuamua ikiwa mutu ametubu, ao hapana. (1 Ko. 5:11; 6:5; Yak. 5:14, 15) Lakini kwa unyenyekevu, wanajua kama hawawezi kusoma moyo na kama wanahukumu kwa ajili ya Yehova. (Linganisha na 2 Mambo ya Nyakati 19:6.) Wakati wanahukumu, wanajikaza kumuiga Yehova kwa kuwa wenye usawaziko, rehema, na haki.