Barua Kutoka Baraza Linaloongoza
Ndugu na Dada Wapendwa:
“Na muwe na fadhili zisizostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo.” (1 Kor. 1:3) Jinsi tunavyotazamia sana wakati ambapo kila kitu kinachopumua kitampa Yehova utukufu anaostahili! (Zab. 150:6) Tunapongojea siku hiyo tukufu, tunaendelea kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu na kufanya wanafunzi.
Huduma ya kueneza evanjeli ni sehemu inayokaziwa fikira kuhusu kazi za Yehova duniani. (Marko 13:10) Kwa kuwa tunajua vizuri kwamba Yehova anapendezwa na kazi hiyo, tunamuomba katika sala atusaidie ili kuitimiza, tukitambua kwamba kila mwanadamu ana nafasi ya kufaidika na uandalizi wa fidia. (Ufu. 14:6, 7, 14, 15) Kwa kweli, tunapambana na magumu, lakini sisi ni wenye shukrani kama nini kuwa wenye ‘kuvikwa nguvu kutoka juu’ ili kutimiza huduma hiyo!—Luka 24:49.
Ni jambo lenye kufurahisha kutazama nyuma kwenye mwaka wa utumishi uliopita na kufikiria juu ya yale ambayo Yehova ametimiza kupitia watumishi wake washikamanifu. Kwa kuwa walipewa nguvu na roho takatifu, watu wa Mungu wameonyesha upendo kama wa Kristo, wakishinda chuki ulimwenguni pote. Upendo kama huo ulionekana kwa wazi katika mikusanyiko yetu. Kutoka Juni mpaka Desemba 2003, wajumbe wenye kutoka inchi zaidi ya mia moja walisafiri kwenda kwenye mikusanyiko ya kimataifa 32 iliyofanywa katika kontinenti tano. Wamishonari, watumishi wa kimataifa, na wanabetheli wenye kutumikia katika inchi za kigeni walihojiwa kwenye mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa.
Kwenye mikusanyiko hiyo, tulipata vichapo “Ona Nchi Nzuri” na Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu. Kwa kuongezea, ilitangazwa kwamba kitabu kwa ajili ya Shule ya Utumishi wa Painia kitafanyiwa mabadiliko ya lazima na kwamba inapangwa kitumiwe mwisho wa mwaka wa utumishi 2004. Hatua kwa hatua, mapainia wanaotumikia kwa muda mrefu ambao wamekwisha kuhudhuria shule watahudhuria pamoja na mapainia wapya.
Tegemeo la Mungu na ukarimu wa wanadamu vimefanya iwezekane kujenga Majumba ya Ufalme mengi zaidi, hasa katika inchi zisizo na mali nyingi. Kwa sababu ya uhitaji unaozidi wa chakula cha kiroho ulimwenguni pote, mipango ya upanuzi wa tawi ni yenye kuendelea katika inchi nyingi. Broshua Furahia Milele Maisha Duniani! inapatikana sasa katika lugha 299, ikiwa na nakala za chapa zote milioni 139; Kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele kimezidi nakala milioni 93 katika lugha 161; na nakala zaidi ya milioni 200 za broshua Mungu Anataka Nini Kwetu? zimekuwa zikichapwa katika lugha 267.
Tunakaribisha kwa shauku watu 258,845 ambao walibatizwa katika maji ili kuonyesha wakfu wao mnamo mwaka wa utumishi uliopita! Ingawa kutegemeza kwenu Ufalme wa Mungu kuliwafanya muwe shabaha ya pekee ya chuki ya Shetani, kuliwafanya pia muwe wapokeaji wa baraka za Yehova na ulinzi wa kiroho mnapokimbia shindano la mbio lililowekwa mbele yenu. (Ebr. 12:1, 2; Ufu. 12:17) Ndiyo, muwe hakika kwamba ‘Yeye anayewalinda hawezi kamwe kusinzia.’—Zab. 121:3.
Andiko la mwaka 2004, “Endeleeni kukesha . . . Iweni tayari,” ni lenye kufaa kabisa. (Mt. 24:42, 44) Katika Neno la Mungu Wakristo wanaelezwa kuwa wakaaji wa muda katika mfumo huu wa mambo ambao ni wenye kufa. (1 Pet. 2:11; 4:7) Kwa sababu hiyo, tunahitaji kukaza fikira juu ya mambo ya kiroho, kuishi maisha ya kawaida, na kuchunguza mioyo yetu kwa uangalifu. “Joka mkubwa” anataka kutumeza, akitufanya tuwe sehemu ya mfumo wake wa mambo.—Ufu. 12:9.
Jambo la maana sana ili kudumisha uangalifu wetu ni usomaji wa Biblia wa kila siku. Usomaji huo unaweza kutusaidia ‘tufanye Ndiyo yetu imaanishe ndiyo’ ili kutimiza wakfu wetu na ‘kuushikilia sana uhakika tuliokuwa nao mwanzoni imara mpaka mwisho.’ (Yak. 5:12; Ebr. 3:14) Usomaji wa Biblia wa kila siku unaweza kutusaidia tukumbuke jinsi ambavyo ulimwengu umekengeuka mbali sana kutoka viwango vya Mungu visivyobadilika. (Mal. 3:6; 2 Ti. 3:1, 13) Ujuzi wa Biblia unaweza kutusaidia kuepuka kabisa “hadithi za uwongo zilizotungwa kwa ufundi” na kubaki waaminifu kwa Yehova.—2 Pet. 1:16; 3:11.
Wazazi, mnapolea watoto wenu katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova, je, nyinyi ni wenye kuwasaidia wajiwekee miradi ya kiroho na ‘kuendelea kukesha’? (Efe. 6:4) Je, nyinyi ni wenye kuwazoeza ili waone wakati wao ujao kama vile Yesu, mtu mwenye hekima zaidi aliyepata kuishi duniani, alivyoona wakati wake ujao? Yesu angaliweza kuwa seremala, mvumbuzi, au daktari mkubwa kupita wote aliyepata kuishi, badala ya hiyo alifuatia huduma ya wakati wote. Mfano wake na ukuchochee kusaidia watoto wako watangulize faida za Ufalme katika maisha yao.
Jamii ya mtumwa mwaminifu, inayowakilishwa na Baraza Linaloongoza, ambayo ina daraka la kufanya ‘hii habari njema ya ufalme ihubiriwe katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi,’ ni yenye kujaa na shukrani yenye kutoka moyoni kuelekea “umati mkubwa” kwa sababu ya msaada wayo. (Ufu. 7:9; Mt. 24:14, 45) Nyinyi wapendwa iweni na uhakikisho kwamba Yehova anakumbuka “kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu nanyi mnaendelea kuhudumu.” (Ebr. 6:10) Mtakaposoma mambo yaliyoonwa yenye kusisimua na kufahamu matokeo ya jitihada zenu zenye umoja katika kurasa za Kitabu-Mwaka, mjue kwamba mmetimiza sehemu ya maana sana katika kutoa ushahidi huo ulimwenguni pote.
Na mpambane na wakati ujao kwa moyo mkuu mkiendelea ‘kukaza macho kwenye malipo ya thawabu,’ bila kuacha mtu yeyote au roho mwovu kuwanyang’anya malipo hayo. (Ebr. 11:26; Kol. 2:18) Ndiyo, mtegemeeni Yehova, mkiwa hakika kwamba atasaidia wote wanaompenda ili wafikie maisha kamili.—Yoh. 6:48-54.
Muwe hakika na furaha yetu katika kutumikia pamoja nanyi kwa sifa ya utukufu wa Yehova.
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova