UIGE IMANI YAO | ABELI
“Ijapokuwa Alikufa, Bado Anasema”
ABELI anatazama kundi lake la kondoo likikula majani kwa amani juu ya mulima. Kisha, labda anatazama mbali sana na kondoo zake, na anaona mahali palipo na mwangaza mudogo sana. Anajua kwamba mahali hapo pana upanga unaowaka moto unaoendelea kuzunguka-zunguka ili kuzuia njia ya kuingia katika bustani ya Edeni. Wakati fulani wazazi wake waliishi mahali hapo, lakini iwe wazazi wake wala watoto wao hawawezi tena kuingia mahali hapo. Wazia akilini upepo wa mangaribi unaopeperusha nywele za Abeli anapotazama juu na kuwaza juu ya Muumbaji wake. Je, uhusiano kati ya mwanadamu na Mungu ungerudishwa tena siku fulani? Hilo ndilo jambo ambalo Abeli anatamani sana.
Abeli anasema na wewe leo. Je, unaweza kumusikia? Unaweza kusema kwamba jambo hilo haliwezekane. Kwa kweli, mutoto huyo wa pili wa Adamu alikufa kumepita miaka mingi. Mifupa yake ilioza zamani sana na kuchanganyika na udongo karibu miaka 6 000 iliyopita. Biblia inatufundisha kama wafu ‘hawajue lolote kamwe.’ (Mhubiri 9:5, 10) Zaidi ya hayo, hakuna neno lolote ambalo Abeli alisema linaloandikwa katika Biblia. Kwa hiyo, namna gani anasema na sisi?
Mutume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika juu ya Abeli hivi: “Ijapokuwa alikufa, bado anasema.” (Waebrania 11:4) Abeli anasema na sisi kupitia nini? Kupitia imani yake. Abeli alikuwa mwanadamu wa kwanza aliyekomalisha sifa hiyo nzuri. Alionyesha imani yenye nguvu hivi kwamba leo tunaendelea kukumbuka mufano wake muzuri na tunaweza kuiga mufano huo. Ikiwa tunajifunza kutokana na imani yake na kujikaza kuiga imani hiyo, ni kama vile tunamusikiliza Abeli akisema na sisi.
Kwa sababu Biblia haiseme mambo mengi juu ya Abeli, basi, namna gani tunaweza kujifunza juu yake na imani yake? Acheni tuone.
ALIKOMAA WAKATI WATU HAWAKUWA WENGI DUNIANI
Abeli alizaliwa muda mufupi kisha wanadamu wa kwanza kuumbwa. Yesu alisema baadaye kama Abeli alikuwa ‘musingi wa ulimwengu.’ (Luka 11:50, 51) Kwa maneno hayo, ni wazi kwamba Yesu alimaanisha wanadamu ambao wana tumaini la kukombolewa kutokana na zambi. Ijapokuwa Abeli alikuwa mwanadamu wa ine kuishi, inaonekana kwamba alikuwa mwanadamu wa kwanza ambaye Mungu aliona kuwa anahitaji kukombolewa.a Ni wazi kwamba Abeli alipoendelea kukomaa, hapakuwa na watu ambao walikuwa mifano mizuri ya kuiga.
Hata ikiwa wanadamu hawakuwa wengi wakati huo, walikuwa tayari wameanza kupambana na hali ngumu za maisha. Inawezekana Adamu na Eva, wazazi wa Abeli, walikuwa watu wenye sura nzuri na wenye nguvu. Lakini, walikuwa wamefanya zambi nzito, na walijua hilo. Kwanza walikuwa wakamilifu na walikuwa na tumaini la kuishi milele. Kisha, walimuasi Yehova Mungu na wakafukuzwa katika makao yao ya Paradiso, ni kusema, bustani ya Edeni. Kwa kuweka tamaa zao pa nafasi ya kwanza kuliko vitu vingine vyote, hata mahitaji ya wazao wao, Adamu na Eva walipoteza ukamilifu na uzima wa milele.—Mwanzo 2:15–3:24.
Maisha ya Adamu na Eva inje ya bustani yalikuwa magumu sana. Lakini, mutoto wao wa kwanza alipozaliwa, walimuita Kaini, ao “Kitu Kilichotokezwa,” na Eva akasema hivi: ‘Nimezaa mwanaume kwa musaada wa Yehova.’ Maneno yake yanaonyesha kama labda alifikiria ahadi ambayo Yehova alitoa katika bustani ya Edeni, iliyoonyesha kama mwanamuke fulani angetokeza “uzao” ambao siku moja ungeharibu yule muovu aliyemudanganya Adamu na Eva. (Mwanzo 3:15; 4:1) Je, Eva alifikiri yeye ndiye mwanamuke aliyetajwa katika unabii huo na kama Kaini ndiye “uzao” ulioahidiwa?
Ikiwa alifikiri hivyo, alidanganyika sana. Zaidi ya hilo, ikiwa yeye na Adamu walimutia Kaini mawazo hayo akilini alipoendelea kukomaa, walimufanya mutu huyo asiyekamilika awe mwenye kiburi hata zaidi. Kisha hapo, Eva alizaa mutoto wa pili, lakini katika Biblia hatuone maneno kama hayo ya kumusifu-sifu mutoto huyo. Alimuita Abeli, jina ambalo linaweza kumaanisha “Pumuzi” ao “Ubatili.” (Mwanzo 4:2) Je, walichagua jina hilo ili kuonyesha kama hawakumutumainia Abeli sana kama walivyomutumainia Kaini? Labda ni hivyo, lakini hatuna uhakika.
Iwe ni hivyo ao hapana, wazazi wa leo wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na wazazi hao wa kwanza. Kupitia maneno na matendo yenu, je, mutawafanya watoto wenu wawe na kiburi, tamaa ya kutafuta mambo makubwa, na mielekeo ya uchoyo? Ao je, mutawafundisha kumupenda Yehova Mungu na kufanya urafiki naye? Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wazazi wa kwanza walishindwa kutimiza daraka lao. Hata hivyo, kulikuwa tumaini kwa wazao wao.
NAMNA GANI ABELI ALIKOMALISHA IMANI?
Kaini na Abeli walipoendelea kukomaa, labda Adamu aliwafundisha kazi ambayo wangefanya ili kutimiza mahitaji ya familia. Kaini akakuwa mulimaji; na Abeli akakuwa muchungaji wa wanyama.
Hata hivyo, Abeli alifanya jambo fulani la maana sana. Kwa muda wa miaka mingi, alikomalisha imani, sifa nzuri ambayo Paulo alizungumuzia baadaye. Fikiria imani hiyo. Hapakuwa na mutu yeyote ambaye Abeli angeweza kuiga mufano wake. Basi, namna gani alikomalisha imani katika Yehova Mungu? Fikiria sababu tatu kubwa zilizomusaidia kuwa na imani hiyo.
Uumbaji wa Yehova.
Ni kweli kwamba Yehova alikuwa ameulaani udongo, na kuufanya uzae miiba na mibaruti ambayo ilifanya kazi ya kulima iwe ngumu. Hata hivyo, udongo ulitoa chakula kingi ambacho kiliiwezesha familia ya Abeli kuendelea kuishi. Na Mungu hakuwalaani wanyama, ndege na samaki; hakuilaani milima, mitoni, na bahari; wala hakulaani anga, mawingu, jua, mwezi, na nyota. Kila mahali ambapo Abeli alitazama, aliona mambo yaliyoonyesha upendo, hekima, na wema wa Yehova Mungu, yule aliyeviumba vitu vyote. (Waroma 1:20) Kufikiri sana juu ya vitu vyote hivyo kulifanya imani yake iwe yenye nguvu zaidi.
Bila shaka, Abeli alijiwekea wakati wa kufikiri sana juu ya mambo ya kiroho. Umuone akilini akiwalinda wanyama wake. Maisha ya muchungaji yaliomba kutembea sana. Aliwaongoza wanyama wake kwenye vilima, kupitia mabonde, kuvuka mitoni, akitafuta majani mabichi, mashimo mazuri yenye maji, na mahali pazuri zaidi pa kuwalisha wanyama. Kati ya wanyama wote ambao Mungu aliumba, kondoo ni wanyama wanaoonekana kuwa zaifu zaidi, kama kwamba waliumbwa wakiwa na uhitaji wa mwanadamu ili kuwaongoza na kuwalinda. Je, Abeli aliona pia kwamba alihitaji Mutu fulani mwenye hekima na nguvu zaidi kuliko mwanadamu yeyote ili amuongoze, amulinde na kumushugulikia? Bila shaka, alieleza mawazo kama hayo katika sala zake, na hilo lilifanya imani yake iendelee kukomaa.
Uumbaji ulimusaidia Abeli kuwa na imani yenye nguvu katika Muumbaji mwenye upendo
Ahadi za Yehova.
Bila shaka, Adamu na Eva waliwaelezea watoto wao mambo yaliyofanya wafukuzwe katika bustani ya Edeni. Hivyo, Abeli alikuwa na mambo mengi yaliyomusaidia afikiri sana juu ya Mungu.
Yehova alisema udongo ungelaaniwa. Ni wazi kwamba Abeli aliona utimizo wa maneno hayo alipoona miiba na mibaruti. Pia, Yehova alitabiri kama Eva angepata maumivu wakati wa mimba na kuzaa watoto kwa uchungu. Abeli aliona maneno hayo pia yakitimia wakati ndugu na dada zake wadogo walipozaliwa. Yehova aliona mbele ya wakati kuwa Eva angekuwa na uhitaji wa kupendwa na kuhangaikiwa sana na bwana yake, na kwamba Adamu bwana yake angemutawala. Abeli aliona mambo yote hayo yenye kuhuzunisha yakitimia mbele ya macho yake. Katika kila hali, Abeli aliona kuwa neno la Yehova linategemeka kabisa. Kwa hiyo, alikuwa na sababu nzuri ya kuamini ahadi ya Mungu juu ya “uzao” ambao siku moja ungemaliza maovu yaliyoanza katika bustani ya Edeni.—Mwanzo 3:15-19.
Watumishi wa Yehova.
Abeli hakuwa na mutu yeyote ambaye alikuwa mufano muzuri wa kuiga, lakini wakati huo si wanadamu tu ndio walikuwa viumbe wenye akili duniani. Wakati Adamu na Eva walifukuzwa katika bustani ya Edeni, Yehova alichukua mipango ili kuwazuia wao na watoto wao wasiingie katika bustani ya Edeni. Ili kuwazuia kuingia katika bustani ya Edeni, Yehova aliweka makerubi, malaika wa hali ya juu sana, kwenye mwingilio wa bustani hiyo na pia upanga wenye kuwaka moto ambao uliendelea kuzunguka-zunguka.—Mwanzo 3:24.
Fikiria Abeli anapowaona makerubi hao alipokuwa kijana. Kwa sababu wanaonekana katika miili ya kibinadamu, Abeli anawaona kuwa wenye nguvu sana. Na “upanga” huo unaoendelea kuwaka moto na kuzunguka-zunguka, unamuogopesha sana. Abeli anapoendelea kukomaa, je, kuna siku aliona malaika hao wanachoka na kuacha kazi yao? Hapana. Muchana na usiku, mwaka baada ya mwaka, makumi ya miaka baada ya makumi ya miaka, viumbe hao wenye akili na wenye nguvu sana, walibaki mahali pale pale. Kwa hiyo, Abeli alijua kwamba Yehova Mungu ana watumishi wenye haki na washikamanifu. Aliona kama makerubi hao walikuwa na sifa ya ushikamanifu na utii kwa Yehova, sifa ambazo hakuona katika familia yake. Bila shaka, mufano wa malaika hao ulitia imani yake nguvu.
Katika maisha yake yote, Abeli aliona kwamba wale makerubi walikuwa watumishi waaminifu na watiifu kwa Yehova
Imani ya Abeli inaendelea kuwa yenye nguvu zaidi anapofikiri sana juu ya mambo ambayo Yehova alifunua kupitia uumbaji, ahadi zake, na mifano ya watumishi Wake. Abeli anasema na sisi kupitia mufano wake, sivyo? Vijana hasa wanaweza kutiwa moyo kwa kujua kwamba inawezekana wao pia wakomalishe imani ya kweli katika Yehova Mungu, hata iwe watu wa familia yao wanatenda namna gani. Leo, tuna musingi wa kukomalisha imani yetu kwa sababu tunazungukwa na maajabu yote ya uumbaji, tuna Biblia yote nzima, na pia tuna mifano mingi ya watu wenye imani.
SABABU GANI TOLEO LA ABELI LILIPITA LILE LA NDUGU YAKE?
Imani ya Abeli katika Yehova ilipoendelea kukomaa, alitafuta nafasi ya kuonyesha imani hiyo kwa matendo. Lakini, mutu wa udongo tu angemupatia nini Muumbaji wa ulimwengu wote? Bila shaka, Mungu hakuhitaji zawadi yoyote kutoka kwa wanadamu. Muda mufupi baadaye, Abeli alielewa kweli hii ya musingi: Ikiwa alimutolea Yehova kwa nia njema zawadi nzuri zaidi kati ya vitu alivyokuwa navyo, Baba yake wa mbinguni mwenye upendo angefurahi.
Kwa hiyo, Abeli alitayarisha kondoo fulani za kundi lake ili kuzitoa. Alichagua kondoo nzuri zaidi katika kundi lake, ni kusema, kati ya wazao wa kwanza wa kondoo zake, na akatoa sehemu alizoona kuwa nzuri zaidi za wanyama hao. Wakati huohuo, Kaini alitafuta pia kukubaliwa na kubarikiwa na Mungu, kwa hiyo alitayarisha mavuno yake na kuyatoa kwa Mungu. Lakini, nia yake haikuwa nzuri kama ya Abeli. Tofauti kati ya ndugu hao wawili ilionekana wazi wakati walimutolea Mungu matoleo yao.
Abeli alitoa zabihu yake kwa imani; lakini Kaini hakufanya hivyo
Inawezekana watoto hao wawili wa Adamu walitumia mazabahu na moto ili kutoa matoleo yao, na labda makerubi ambao ndio waliokuwa tu wajumbe wa Yehova duniani wakati huo, walikuwa wakiona. Yehova alitenda namna gani? Tunasoma hivi: ‘Yehova alikuwa akimutazama Abeli na toleo lake kwa kibali.’ (Mwanzo 4:4) Namna gani Mungu alionyesha kama alikubali toleo la Abeli? Biblia haiseme jambo lolote. Lakini, sababu gani alikubali toleo la Abeli?
Je, ilikuwa kwa sababu toleo hilo lilikuwa nzuri? Abeli alitoa wanyama, ni kusema, viumbe wenye kupumua, na akamuanga damu ya wanyama hao. Je, Abeli alijua kama zabihu hiyo ingekuwa ya maana sana? Miaka mingi kisha wakati wa Abeli, Mungu alitumia zabihu ya mwana-kondoo asiye na kasoro ili kuonyesha zabihu ya Mwana wake mukamilifu, “Mwana-Kondoo wa Mungu,” ambaye damu yake isiyo na kosa ingemuangwa. (Yohana 1:29; Kutoka 12:5-7) Hata hivyo, Abeli hakujua ao kuelewa namna Yehova angetumia baadaye zabihu mbalimbali.
Jambo ambalo tunajua kwa uhakika ni hili: Abeli alitoa kitu kizuri zaidi kati ya vitu alivyokuwa navyo. Yehova hakupendezwa tu na zabihu hiyo lakini pia alipendezwa na mutu aliyeitoa. Abeli alitenda kwa sababu alichochewa na upendo na imani ya kweli kwa Yehova.
Lakini haikuwa hivyo kumuhusu Kaini. Yehova ‘hakumutazama Kaini na toleo lake kwa kibali chochote.’ (Mwanzo 4:5) Haikuwa kwa sababu toleo la Kaini lilikuwa mbaya; baadaye Sheria ya Mungu iliwaruhusu watu kutoa toleo la mazao ya udongo. (Mambo ya Walawi 6:14, 15) Lakini Biblia inasema juu ya Kaini kwamba “matendo yake mwenyewe yalikuwa maovu.” (1 Yohana 3:12) Kama watu wengi leo, ni wazi Kaini alifikiri kuwa ilitosha tu kuonyesha kijuu-juu kama anajitoa kwa Mungu. Kukosa kwake imani ya kweli ao upendo kwa Yehova kulionekana haraka kupitia matendo yake.
Kaini alipoona kama hakukubaliwa na Yehova, je, alitafuta kujifunza kutokana na mufano wa Abeli? Hapana. Alimukasirikia ndugu yake na kumuchukia. Yehova aliona mambo yaliyokuwa yakitokea katika moyo wa Kaini na alifikiri naye kwa uvumilivu. Alimuonya Kaini kwamba hasira na chuki yake ingemuongoza kufanya zambi nzito, na aliahidi ‘kumuinua’ ikiwa tu angebadilika.—Mwanzo 4:6, 7.
Kaini alipuuza onyo la Mungu. Alimuomba ndugu yake mudogo asiye na kosa amusindikize kwenye mashamba. Wakiwa huko, Kaini alimushambulia ndugu yake na kumuua. (Mwanzo 4:8) Tunaweza kusema kwamba Abeli alikuwa mutu wa kwanza aliyeteswa na kuuawa kwa sababu ya imani yake. Alikufa, lakini habari ya maisha yake haikusahauliwa.
Kwa njia ya mufano, damu ya Abeli ilimulilia Yehova Mungu ili alipize kisasi, ao haki itendeke. Na Mungu alifanya haki itendeke, kwa kumuazibu yule muovu Kaini kwa sababu ya tendo lake la uuaji. (Mwanzo 4:9-12) Jambo la maana zaidi, Abeli anasema na sisi leo kupitia imani yake. Maisha ya Abeli yalikuwa mafupi, labda miaka 100 hivi, ukiyalinganisha na ya watu wengine wa wakati wake, lakini aliishi kwa njia iliyomupendeza Mungu. Alikufa akiwa mwenye kujua kwamba alipendwa na kukubaliwa na Yehova, Baba yake wa mbinguni. (Waebrania 11:4) Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Abeli iko mahali salama katika kumbukumbu la Yehova, akingojea afufuliwe ili kuishi katika paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29) Je, utakutana naye katika paradiso? Unaweza kukutana naye ikiwa unaazimia kumusikiliza anaposema na sisi na kuiga imani yake yenye nguvu.
a Maneno ‘musingi wa ulimwengu’ yanatoa pia wazo la kutupa mbegu chini, ni kusema, kuzaa, na hilo linahusiana na uzao wa mwanadamu wa kwanza. Basi, sababu gani Yesu alisema kama Abeli alikuwa ‘musingi wa ulimwengu’ ijapokuwa Kaini ndiye alikuwa mwanadamu aliyezaliwa kwanza? Maamuzi na matendo ya Kaini yalifanya amuasi Yehova Mungu kimakusudi. Kama vile wazazi wake, inawezekana Kaini pia hatafufuliwa na kufaidika na ukombozi.