NYONGEZA
Namna ya Kumaliza Kutoelewana Katika Mambo ya Biashara
Katika 1 Wakorintho 6:1-8, mutume Paulo anazungumuzia namna Wakristo wa Korintho walikuwa wakishitakana mbele ya tribinali. Alisema kwamba jambo hilo, ni kusema, ‘kusubutu kuenda mahakamani mbele ya watu wasio waadilifu,’ lilimuhuzunisha sana. (Mustari wa 1) Mutume Paulo alionyesha sababu gani Wakristo hawapaswe kufanya hivyo, pia wanapaswa kumaliza magumu yao katika kutaniko. Acheni sasa tuone sababu fulani zilizomuchochea kutoa shauri hilo; na kisha tutazungumuzia hali fulani ambazo hazitajwe moja kwa moja katika shauri hilo.
Ikiwa ndugu fulani haelewane na ndugu mwengine katika mambo ya biashara, kwanza watajikaza kumaliza matatizo yao kwa kufuata shauri la Yehova, wala si mawazo yao wenyewe. (Methali 14:12) Yesu alisema ni vizuri kumaliza haraka hali ya kutoelewana mbele haijakuwa mbaya zaidi. (Mathayo 5:23-26) Lakini, jambo la kuhuzunisha ni kwamba Wakristo fulani wanakokotana sana, na hata wanapeleka ugomvi wao kwenye tribinali za ulimwengu. Mutume Paulo alisema: ‘Inamaanisha kushindwa kwenu kabisa kwamba munakuwa na mashitaka ya kisheria mutu na mwenzake.’ Sababu gani Paulo alisema hivyo? Sababu kubwa ni kwamba mashitaka kama hayo yanaweza kutukanisha kutaniko na jina la Mungu tunayemuabudu. Kwa hiyo, inatuomba tufikirie vizuri ulizo hili la mutume Paulo: ‘Kwa nini musiache mukosewe?’—Mustari wa 7.
Tena, alisema kwamba Mungu ametia wanaume wazee katika kutaniko ili kumaliza matatizo mengi kama hayo. Wao wamepata hekima kupitia ujuzi wa Biblia, na ‘wanaweza kuhukumu kati ya ndugu’ kuhusu “mambo ya maisha haya.” (Mustari wa 3-5) Yesu alionyesha kwamba matatizo yanapotokea kwa sababu ya kusingiziwa na kupunjwa, yanapaswa kumalizwa kwa kufuata hatua tatu zinazofuata: Kwanza, wale wenye kukokotana wanapaswa kufanya nguvu ya kuzungumuza ili kumaliza matatizo yao kati yao wenyewe. Pili, hatua ya kwanza ikishindwa, shahidi mumoja ao wawili wanaweza kuletwa. Na tatu, ikiwa hawapatane tu, jambo hilo litapelekwa kwenye kutaniko, ni kusema, mbele ya wazee.—Mathayo 18:15-17.
Kwa kweli, wazee wa kutaniko si waamuzi wala wanasheria, na labda wao si wafanya-biashara, na daraka lao si hilo. Hawana sheria za kumaliza kutoelewana katika mambo ya biashara kati ya ndugu. Lakini, wanajikaza kusaidia ndugu hao wajue namna ya kutumia mashauri ya Biblia na pia wamalize matatizo yao kwa amani. Ikiwa tatizo hilo ni ngumu, wanaweza kuzungumuza na mwangalizi wa muzunguko ao biro ya tawi. Hata hivyo, kuna hali fulani ambazo hazisemwe moja kwa moja katika shauri la mutume Paulo. Ni hali gani hizo?
Katika hali fulani, kupeleka jambo kwenye tribinali inaweza kufanyika kwa sababu ndugu wanaona tu ni vizuri iwe hivyo ili jambo lao limalizike kwa amani ao kwa sababu sheria ya serikali inaomba hivyo, hata ikiwa ndugu hawakokotane. Kwa mufano, labda kuenda kwenye tribinali ndio njia moja tu inayokubaliwa na serikali ikiwa mutu anataka kupata cheti cha kuvunja ndoa, kupewa ruhusa ya kuwatunza watoto, kulipwa na mwenzi aliyevunja ndoa, kupata malipo ya asiranse, kuandikisha jina kati ya watu ambao inaombwa walipwe wakati kompanyi fulani imefunga, na kufanya testama ikubaliwe kisheria. Kuna hali zingine pia zinazoweza kufanya ndugu aone kwamba ni lazima apeleke jambo kwenye tribinali ili serikali ijue haki yake na kuepuka kutoelewana wakati mutu mwengine anaweza kumushitaki.a
Ikiwa Wakristo wanashitakana hivyo bila roho ya mashindano, hatuwezi kusema mara moja kwamba wanavunja shauri la mutume Paulo.b Hata hivyo, Mukristo anapaswa kwanza kuhangaikia kutakaswa kwa jina la Yehova na pia amani na umoja wa kutaniko. Upendo ndio unaotambulisha wafuasi wa Kristo, na ‘upendo hautafute faida zake.’—1 Wakorintho 13:4, 5; Yohana 13:34, 35.
a Hata ikiwa si jambo la kawaida, inawezekana Mukristo fulani amutendee Mukristo mwenzake tendo fulani mbaya sana, kama vile, kumulala kinguvu, kumushambulia, kumuua, ao kumuiba kitu fulani cha bei sana. Katika hali kama hizo, hakuna ubaya ikiwa Mukristo anashitaki jambo hilo, hata ikiwa itawaomba kuenda kwenye tribinali.
b Ili kupata habari zaidi, soma Munara wa Mulinzi wa tarehe 5 Mwezi wa 3, 1997, ukurasa wa 17-22, na ule wa tarehe 15 Mwezi wa 10, 1991, ukurasa wa 25-28.