MASIMULIZI KUHUSU MAISHA YA WATU
Maskini Kimwili Lakini Tajiri Kiroho
Baba yangu na baba yake waliishi katika nyumba ambayo ilikuwa haijamalizwa kujengwa huko Cotiujeni, kijiji cha watu maskini kilicho katika sehemu ya kaskazini mwa inchi inayoitwa leo Moldova. Nilizaliwa huko Mwezi wa 12, 1939. Mwanzoni mwa miaka kati ya 1931 na 1940, baba yangu na baba yake wakakuwa Mashahidi wa Yehova. Mama pia akakuwa Shahidi wa Yehova kisha kuona kwamba baba yake na baba alijua Biblia vizuri kuliko padiri wa kijiji chetu.
Nilipokuwa na miaka tatu, baba yangu, mujomba wangu, na baba yake na baba walipelekwa katika kambi za kazi ngumu kwa sababu walikataa kujiingiza katika mambo ya siasa. Baba yangu peke yake ndiye alitoka katika kambi hiyo akiwa muzima. Katika mwaka wa 1947, kisha Vita ya Pili ya Ulimwengu, alirudi nyumbani mugongo wake ukiwa wenye kuvunjika. Hata ikiwa hali yake ya kimwili ilikuwa mbaya, alibakia mwaminifu.
MABADILIKO MAKUBWA KATIKA MAISHA YETU
Nilipokuwa na miaka kenda, familia yetu na mamia ya ndugu wengine wa Moldova, tulipelekwa huko Siberia. Tarehe 6 Mwezi wa 7, 1949, tulipakizwa ndani ya vyumba vya treni vya kubebea ngombe. Kisha kusafiri siku 12 na kufanya kilometa zaidi ya 6400, tulisimama kwenye kituo cha treni cha Lebyazhe. Wakubwa wa polisi walikuwa wanatungojea kwenye kituo hicho. Tuligawanywa katika vikundi vidogo-vidogo na mara moja tukatawanywa katika eneo lote. Kikundi chetu kiliwekwa katika nyumba za masomo yaliyokuwa yameachwa. Tulikuwa wenye kuchoka sana na wenye kuhuzunika sana. Mwanamuke mumoja muzee aliyekuwa pamoja na sisi alianza kuimba kwa sauti ya chini wimbo uliotungwa na Mashahid wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Kisha sisi wote tuliungana naye kuimba kwa moyo wote maneno ya wimbo huo yanayofuata:
“Ndugu wengi sana walipelekwa mbali uhamishoni.
Waliwapeleka kaskazini na mashariki.
Kwa sababu ya kufanya kazi ya Mungu, walipatwa na magumu na wakavumilia majaribu yaliyo kama kifo.”
Baada ya muda, tuliweza kuhuzuria mikutano ili kujifunza Biblia kila Siku ya Yenga katika nyumba iliyokuwa kwenye umbali wa kilometa 13 kutoka mahali ambapo tuliishi. Mara nyingi tulitoka asubuhi sana na kungali giza wakati wa majira ya baridi na tulitembea ndani ya seluji (matone meupe madogo-madogo ya mvua yaliyoganda) iliyotufikia kwenye kiuno wakati hali ya joto ilikuwa digrii 40 chini ya zero. Watu makumi tano ao zaidi walibanana katika chumba kidogo sana. Tulianza mikutano kwa kuimba wimbo mumoja, nyimbo mbili ao tatu. Sala yenye kutoka moyoni ilitolewa, na kisha tulizungumuzia habari zinazohusu Biblia. Mazungumuzo hayo yaliendelea kwa muda wa saa moja ao zaidi. Tuliimba nyimbo zingine, na kisha tulizungumuzia tena habari zingine zinazohusu Biblia. Huo ulikuwa wakati wenye kutia nguvu kabisa!
MATATIZO MENGINE YA KUPAMBANA NAYO
Kwenye kituo cha treni cha Dzhankoy, mwaka wa 1974 hivi
Kuanzia mwaka wa 1960, Mashahidi waliopelekwa uhamishoni walipewa uhuru zaidi. Ijapokuwa tulikuwa maskini, niliweza kutembelea huko Moldova, mahali nilikutana na Nina, ambaye wazazi wake na wazazi wa wazazi wake walikuwa pia Mashahidi wa Yehova. Muda mufupi kisha hapo, tulioana na tukarudi tena huko Siberia. Binti yetu anayeitwa Dina alizaliwa huko katika mwaka wa 1964 na mutoto wetu mwanaume anayeitwa Viktor akazaliwa pia huko katika mwaka wa 1966. Miaka miwili kisha hapo, tulihamia Ukrainia na tukaishi katika nyumba ndogo katika muji ulio umbali wa kilometa 160 kutoka Yalta, peninsula ya Crimea (Peninsula ni sehemu kubwa na ndefu ya udongo inayoingia ndani ya bahari).
Huko Crimea, kazi zote za Mashahidi wa Yehova zilikatazwa, kama ilivyokuwa katika inchi zote za Muungano wa Kisovieti. Lakini hatukubanwa sana kiasi cha kukosa kuhubiri, wala hatukuteswa sana. Kwa hiyo, Mashahidi fulani walianza kuwa na roho ya uzembe katika mahubiri. Walifikiri kwamba kwa kuwa waliteseka sana huko Siberia, ilikuwa lazima watumike sana ili kupata vitu vya kimwili ambavyo walihitaji.
MABADILIKO YENYE KUSISIMUA
Tarehe 27 Mwezi wa 3, 1991, kazi yetu ilikubaliwa kisheria katika inchi zote za Muungano wa Kisovieti. Mara moja, mipango ilifanywa kwa ajili ya mikusanyiko saba ya pekee ya siku 2 katika inchi yote. Tulipaswa kuhuzuria mukutano wa pekee uliofanywa huko Odessa, Ukrainia, uliopangwa kuanza tarehe 24 Mwezi wa 8. Nilifika mwezi mumoja mbele ya mukusanyiko kuanza ili kusaidia kutayarisha uwanja mukubwa wa kabumbu.
Kisha kutumika siku nzima, wakati wa usiku mara nyingi tulilala kwenye viti virefu vya mbao. Vikundi vya Mashahidi wanawake vilisafisha bustani iliyozunguka uwanja huo. Uchafu wenye uzito wa tani karibu 70 uliondolewa katika uwanja. Wale waliokuwa wakitumika katika idara ya kupangisha wageni walizunguka katika jiji lote ili kutafuta mahali pa kupangisha wajumbe 15000 ambao walitazamiwa kufika kwenye mukusanyiko. Kisha, kwa gafula, tukajulishwa habari yenye kuhuzunisha!
Tarehe 19 Mwezi wa 8, siku tano tu mbele ya mukusanyiko kuanza, Raisi wa Muungano wa Kisovieti, Mikhail Gorbachev alizuiwa kurudia kwenye makao yake alipokuwa kwenye mapumuziko karibu na Yalta. Tulikatazwa kufanya mukusanyiko hata ikiwa tulikuwa tumekwisha kupewa ruhusa. Wajumbe walianza kuita ofisi ao biro ya mukusanyiko, na kuuliza, “Tutafanya nini juu ya tikiti za bisi na treni ambazo tumekwisha kukata?” Kisha kusali sana, ndugu ambao walikuwa na daraka la kutayarisha mukusanyiko waliwaambia, “Munaweza kuja tu!”
Tuliendelea kufanya matayarisho na kusali. Idara ya usafiri ilianza kukutana na wajumbe ambao walikuwa wanakuja kutoka sehemu nyingi za Muungano wa Kisovieti na kuwapeleka mahali palipotayarishwa kuwapangisha. Kila asubuhi, ndugu wa Halmashauri ya Mukusanyiko waliacha ofisi zao na kuenda kukutana na wakuu wa muji. Kila usiku, walirudi bila habari nzuri.
SALA ZETU ZINAJIBIWA
Siku ya Ine, tarehe 22 Mwezi wa 8, siku mbili mbele ya tarehe iliyopangwa kuanza mukusanyiko, ndugu wa Halmashauri ya Mukusanyiko walirudi wakiwa na habari hii nzuri: Wakuu wamekubali tufanye mukusanyiko! Tulikuwa wenye furaha sana wakati tuliimba wimbo wa kwanza, na wakati tulifuata sala ya kufungua mukusanyiko. Kisha kipindi cha mwisho Siku ya Posho, tulibaki hapo mupaka mangaribi tukizungumuza na kufanya tena upya urafiki wetu wa zamani. Kwenye mukusanyiko huo kulikuwa Wakristo wenye imani yenye nguvu sana ambao walishinda majaribu makali zaidi.
Mukusanyiko huko Odessa, mwaka wa 1991
Katika kipindi cha miaka zaidi ya 22 iliyofuata mukusanyiko huo, kumekuwa na maendeleo makubwa ya kiroho. Majumba ya Ufalme yamejengwa katika inchi yote ya Ukrainia, na hesabu ya wahubiri wa Ufalme imeongezeka. Katika mwaka wa 1991 kulikuwa wahubiri 25000 lakini sasa kuna wahubiri zaidi ya 150000!
BADO NINGALI TAJIRI KIROHO
Familia yetu ingali inaishi katika nyumba ileile huko Dzhankoy, muji ambao sasa una wakaaji karibu 40000. Ijapokuwa kulikuwa familia chache tu za Mashahidi wa Yehova tulipofika huko kutoka Siberia katika mwaka wa 1968, sasa kuna makutaniko sita ya Mashahidi wa Yehova huko Dzhankoy.
Familia yetu imeongezeka pia. Sasa familia yetu ina watu wa vizazi ine ambao wangali wazima na ambao wanaendelea kumutumikia Yehova, ni kusema, mimi na bibi yangu, watoto wetu, watoto wa watoto wetu, na wajukuu wa watoto wetu.