Julai
Jumanne, Julai 1
Akapita katika nchi akitenda mema na kuwaponya.—Mdo. 10:38.
Mambo yote ambayo Yesu alisema na kufanya, kutia ndani miujiza aliyofanya, ilionyesha kikamili njia ya kufikiri na hisia za Baba yake. (Yoh. 14:9) Tunaweza kujifunza nini kutokana na miujiza ya Yesu? Yesu na Baba yake wanatupenda sana. Alipokuwa duniani, Yesu alionyesha jinsi alivyowapenda sana watu kwa kutumia uwezo wake kufanya miujiza ili kuwasaidia wale waliokuwa wakiteseka. Pindi moja, wanaume wawili waliokuwa vipofu walimlilia wakiomba msaada. (Mt. 20:30-34) Ona kwamba Yesu ‘aliwasikitikia’ na akawaponya. Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “akawasikitikia” kinarejelea huruma nyingi ambayo mtu anahisi ndani kabisa mwilini. Huruma hiyo nyingi, ambayo ni wonyesho wa upendo, ilimchochea pia Yesu kuwalisha wenye njaa na kumponya mtu mwenye ukoma. (Mt. 15:32; Marko 1:41) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova, Mungu mwenye “huruma nyororo,” na Mwana wake wanatupenda sana na wanaumia tunapoteseka. (Luka 1:78; 1 Pet. 5:7) Bila shaka, wanatamani sana kuondoa matatizo yanayowapata wanadamu! w23.04 15:4-5
Jumatano, Julai 2
Enyi mnaompenda Yehova, chukieni maovu. Anaulinda uhai wa washikamanifu wake;huwaokoa kutoka katika mkono wa mwovu.—Zab. 97:10.
Tunaweza kuchukua hatua hususa ili kuepuka kusoma au kusikiliza mawazo yasiyofaa ambayo yameenea katika ulimwengu wa Shetani. Tunaweza kujaza akili zetu mawazo yanayofaa kwa kusoma na kujifunza Biblia. Kuhudhuria mikutano na kuhubiri kutatusaidia pia kulinda fikira zetu. Naye Yehova anatuahidi kwamba hataacha tujaribiwe kuliko tunavyoweza kuhimili. (1 Kor. 10:12, 13) Kuliko wakati mwingine wowote, kila mmoja wetu anahitaji kusali ili kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova katika siku hizi za mwisho zilizo ngumu. Yehova anataka ‘tumwage mioyo yetu mbele zake’ katika sala. (Zab. 62:8) Msifu Yehova na umshukuru kwa mambo yote anayofanya. Mwombe akusaidie uwe mwenye ujasiri katika huduma. Msihi akusaidie kushughulika na tatizo lolote na kupinga majaribu yoyote ambayo huenda unakabili. Usimruhusu mtu au kitu chochote kikuzuie kusali kwa ukawaida kwa Yehova. w23.05 20:17-18
Alhamisi, Julai 3
Acheni tufikiriane . . . , tutiane moyo.—Ebr. 10:24, 25.
Kwa nini tunahudhuria mikutano ya kutaniko? Sababu ya msingi ni ili tumsifu Yehova. (Zab. 26:12; 111:1) Pia, tunahudhuria mikutano ili tutiane moyo katika nyakati hizi ngumu. (1 The. 5:11) Tunapoinua mkono na kutoa maelezo, tunachangia kutimiza mambo hayo mawili. Lakini tunapotoa maelezo tunaweza kukabili changamoto. Tunaweza kuwa na wasiwasi kuhusu kutoa maelezo, au huenda tukatamani sana kushiriki lakini hatupati fursa za kushiriki mara nyingi kama tunavyotaka. Tunawezaje kukabiliana na changamoto hizo? Mtume Paulo alisema kwamba tunapaswa kukazia fikira ‘kutiana moyo.’ Tunapotambua kwamba wahudhuriaji wengine wanaweza kutiwa moyo na hata maneno rahisi yanayoonyesha imani yetu, hilo litapunguza wasiwasi kuhusu kujibu. Na ikiwa hatutachaguliwa mara nyingi kujibu, tunaweza kuwa na furaha kwamba wengine kutanikoni watapata fursa ya kujibu.—1 Pet. 3:8. w23.04 18:1-3
Ijumaa, Julai 4
[Panda] kwenda Yerusalemu, . . . na kuijenga upya nyumba ya Yehova.—Ezra 1:3.
Mfalme Koreshi alikuwa ametoa agizo! Wayahudi ambao walikuwa mateka huko Babiloni kwa miaka 70 hivi, walikuwa huru kurudi katika nchi yao, Israeli. (Ezra 1:2-4) Ni Yehova tu ambaye angeweza kutimiza jambo hilo. Kwa kawaida, Wababiloni hawakuwaweka huru mateka wao. (Isa. 14:4, 17) Lakini Babiloni lilikuwa limeshindwa, na mtawala mpya alikuwa amewaambia Wayahudi kwamba wangeweza kuondoka. Kila Myahudi, hasa vichwa vya familia, walihitaji kufanya uamuzi huu: kuondoka Babiloni au kuendelea kuishi huko. Huo haukuwa uamuzi rahisi. Kwa wengi waliozeeka, huenda ingekuwa vigumu kufunga safari hiyo. Na kwa kuwa Wayahudi wengi walikuwa wamezaliwa huko Babiloni, waliona nchi hiyo kuwa nyumbani kwao. Walihisi kwamba nchi ya Israeli ilikuwa nchi ya babu zao. Inaonekana kwamba baadhi ya Wayahudi walikuwa wamepata utajiri huko Babiloni, kwa hiyo huenda ilikuwa vigumu kwao kuacha nyumba zao zenye kustarehesha au biashara zao na kuanza kuishi kwenye nchi wasiyofahamu. w23.05 22:1-2
Jumamosi, Julai 5
Iweni tayari.—Mt. 24:44.
Neno la Mungu linatutia moyo tuendelee kusitawisha sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo. Andiko la Luka 21:19 linasema: “Mkivumilia, mtauokoa uhai wenu.” Andiko la Wakolosai 3:12 linasema: “Jivikeni . . . huruma.” Andiko la 1 Wathesalonike 4:9, 10 linasema: “Ninyi wenyewe mmefundishwa na Mungu kupendana. . . . Hata hivyo, tunawahimiza, akina ndugu, endeleeni kufanya hivyo kwa ukamili zaidi.” Mistari hiyo yote iliandikwa kwa ajili ya wanafunzi ambao tayari walikuwa wameonyesha sifa ya uvumilivu, huruma, na upendo. Hata hivyo, walipaswa kuendelea kusitawisha sifa hizo. Ni lazima tufanye hivyo pia. Ili kukusaidia kufanya hivyo, chunguza jinsi ambavyo Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha sifa hizo. Kisha utaona jinsi unavyoweza kuwaiga wanafunzi hao, na hivyo kuthibitisha kwamba uko tayari kwa ajili ya dhiki kuu. Halafu dhiki kuu itakapoanza, tayari utakuwa umejifunza jinsi ya kuvumilia na utaazimia kuendelea kuvumilia. w23.07 29:4, 8
Jumapili, Julai 6
Huko kutakuwa na barabara kuu, . . . Njia ya Utakatifu.—Isa. 35:8.
Iwe sisi ni watiwa-mafuta au ni “kondoo wengine,” tunapaswa kuendelea kutembea katika “Njia ya Utakatifu” inapotupitisha kwenye paradiso ya kiroho na kutuongoza kwenye baraka za wakati ujao katika Ufalme wa Mungu. (Yoh. 10:16) Tangu mwaka wa 1919 W.K., mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wametoka katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo, na wameanza kutembea katika barabara hiyo ya mfano. Wayahudi walipoondoka Babiloni, Yehova alihakikisha kwamba vizuizi vyote njiani viliondolewa. (Isa. 57:14) Namna gani “Njia ya Utakatifu” katika siku zetu? Kwa karne nyingi kabla ya mwaka wa 1919, Yehova alitumia wanaume waliokuwa wanamwogopa Mungu kutayarisha njia ya kutoka katika Babiloni Mkubwa. (Linganisha Isaya 40:3.) Walifanya matayarisho muhimu—kutengeneza barabara ya kiroho—ili kufanya baadaye iwezekane kwa watu wenye mioyo minyoofu kutoka katika Babiloni Mkubwa na kuingia katika paradiso ya kiroho, ambako ibada safi ya Yehova ilikuwa imerudishwa. w23.05 22:8-9
Jumatatu, Julai 7
Mtumikieni Yehova kwa kushangilia. Njooni mbele zake kwa kelele za shangwe.—Zab. 100:2.
Yehova anataka tumtumikie kwa furaha na kwa hiari. (2 Kor. 9:7) Hivyo je, bado tunapaswa kufanyia kazi lengo la kiroho ikiwa hatuna tamaa ya kufanya hivyo? Fikiria mfano wa mtume Paulo. Alisema hivi: “Ninautia nidhamu sana mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Kor. 9:25-27, maelezo ya chini) Paulo alijilazimisha kufanya jambo lililofaa hata alipokosa tamaa ya kufanya hivyo. Je, Yehova alifurahishwa na utumishi wa Paulo? Bila shaka! Na Yehova alimbariki kwa sababu ya jitihada zake. (2 Tim. 4:7, 8) Vivyo hivyo, Yehova anafurahi kuona tukifanyia kazi lengo letu hata ikiwa hatuna tamaa ya kufanya hivyo. Anafurahi kwa sababu ingawa hatufanyi kila mara jambo hilo kwa sababu tunalipenda, anajua kwamba tunalifanya kwa sababu tunampenda yeye. Kama vile Yehova alivyombariki Paulo, atabariki jitihada zetu pia. (Zab. 126:5) Na tunapoona baraka za Yehova, huenda tukachochewa zaidi. w23.05 24:9-10
Jumanne, Julai 8
Siku ya Yehova inakuja.—1 The. 5:2.
Mtume Paulo aliwalinganisha wale ambao hawataokoka siku ya Yehova na watu wanaolala usingizi. Hawajui mambo yanayoendelea katika mazingira yanayowazunguka na pia hawajui muda. Hivyo, hawawezi kutambua matukio muhimu au kuchukua hatua inayofaa. Leo, watu wengi wamelala usingizi wa kiroho. (Rom. 11:8) Hawaamini mambo yanayothibitisha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” na kwamba dhiki kuu itakuja hivi karibuni. (2 Pet. 3:3, 4) Hata hivyo, sisi tunatambua kwamba shauri lililoongozwa na roho la kuendelea kukaa macho linaendelea kuwa muhimu zaidi kadiri siku zinavyopita. (1 The. 5:6) Hivyo, ni lazima tuendelee kuwa watulivu na thabiti. Kwa nini? Ili tusianze kujihusisha na mambo ya kisiasa au ya kijamii katika ulimwengu huu. Mkazo wa kuunga mkono upande fulani kuhusiana na mambo hayo utazidi kuongezeka kadiri siku ya Yehova inavyokaribia. Ingawa hivyo, hatupaswi kuhangaika kuhusu jinsi tutakavyotenda. Roho ya Mungu inaweza kutusaidia kuwa na utulivu na kuwa thabiti kiakili na hivyo tufanye maamuzi kwa hekima.—Luka 12:11, 12. w23.06 26:6-7
Jumatano, Julai 9
Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, nikumbuke, tafadhali, na kunitia nguvu.—Amu. 16:28.
Unafikiria kuhusu nini unaposikia jina Samsoni? Inawezekana kwamba unamfikiria mwanamume aliyekuwa na nguvu sana. Hilo ni kweli. Lakini Samsoni alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia mateso mengi. Hata hivyo, Yehova alikazia fikira mambo yote ambayo Samsoni alikuwa amefanya ili kumtumikia kwa uaminifu, na alitia ndani mfano wa Samsoni katika Biblia ili kutunufaisha. Yehova alimtumia Samsoni kutimiza mambo yenye kustaajabisha ili kuwasaidia watu aliowachagua, Waisraeli. Karne nyingi baada ya kifo cha Samsoni, Yehova alimwongoza mtume Paulo kutia ndani jina la Samsoni kwenye orodha ya wanaume waliokuwa na imani ya pekee. (Ebr. 11:32-34) Mfano wa Samsoni unaweza kututia moyo. Alimtegemea Yehova, hata alipokabili hali ngumu. Tunaweza kutiwa moyo na pia kujifunza masomo fulani kutokana na mfano wake. w23.09 37:1-2
Alhamisi, Julai 10
Mjulisheni Mungu maombi yenu.—Flp. 4:6.
Tunaweza kusitawisha sifa ya uvumilivu kwa kuzungumza na Yehova kwa ukawaida kuhusu mambo yanayotuhangaisha. (1 The. 5:17) Labda sasa hukabiliani na jaribu kali. Hata hivyo, je, wewe hutafuta mwongozo wa Yehova kila mara unapokasirika, unapochanganyikiwa, au kulemewa na hisia? Ikiwa sasa unamwomba Mungu msaada kwa ukawaida unapokabiliana na changamoto za kila siku, hutasita kufanya hivyo utakapokabili changamoto kubwa zaidi wakati ujao. Utakuwa na uhakika kwamba Yehova anajua kihususa wakati na jinsi ya kukusaidia. (Zab. 27:1, 3) Itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumilia dhiki kuu wakati ujao ikiwa sasa tunavumilia majaribu. (Rom. 5:3) Kwa nini tunasema hivyo? Ndugu wengi wametambua kwamba kila jaribu la imani walilovumilia liliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata. Uvumilivu uliwasaidia kuimarisha imani yao kwamba Yehova yuko tayari na anataka kuwasaidia. Kisha imani yao iliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata.—Yak. 1:2-4. w23.07 29:7-8
Ijumaa, Julai 11
Nitakutendea . . . kwa fadhili.—Mwa. 19:21.
Unyenyekevu na huruma ya Yehova humchochea kuwa mwenye usawaziko. Kwa mfano, Yehova alionyesha unyenyekevu kabla ya kuharibu watu waovu huko Sodoma. Kupitia malaika wake, Yehova alimwagiza Loti mwadilifu akimbilie kwenye eneo lenye milima. Loti aliogopa kwenda huko. Basi, akaomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia huko Soari, mji mdogo ambao ulipaswa kuharibiwa. Yehova angeweza kusisitiza kwamba Loti anapaswa kufuata kikamili maagizo yaliyotolewa. Badala yake, alikubali ombi la Loti, ingawa hilo lilimaanisha kwamba mji wa Soari haungeharibiwa. (Mwa. 19:18-22) Karne nyingi baadaye, Yehova aliwaonyesha huruma wakaaji wa Ninawi. Alimtuma nabii Yona atangaze kuhusu uharibifu ambao ungelipata jiji hilo na wakaaji wake waovu. Lakini Waninawi walipotubu, Yehova aliwahurumia, naye hakuharibu jiji hilo.—Yona 3:1, 10; 4:10, 11. w23.07 32:5
Jumamosi, Julai 12
Walimuua [Yehoashi] . . . , lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme.—2 Nya. 24:25.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yehoashi? Alikuwa kama mti wenye mizizi mifupi ambao ulitegemezwa na nguzo, nguzo hiyo ilipoondolewa, yaani, Yehoyada alipokufa, upepo wa uasi-imani ulivuma na kumwangusha Yehoashi. Hilo ni somo lenye nguvu kwamba hatupaswi kumwogopa Mungu kwa sababu tu ya kuchochewa na Wakristo wenzetu, kutia ndani watu wa familia yetu. Ili tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho, ni lazima tuimarishe ujitoaji wetu kimungu na woga wetu kumwelekea Mungu kwa kujifunza kwa ukawaida, kutafakari, na kusali. (Yer. 17:7, 8; Kol. 2:6, 7) Yehova hadai mengi kutoka kwetu. Jambo ambalo anataka tufanye linatajwa kwenye andiko la Mhubiri 12:13, linalosema: “Mwogope Mungu wa kweli na ushike amri zake, kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.” Ikiwa tutamwogopa Mungu, tutafaulu kukabiliana na majaribu ya wakati ujao na kusimama imara. Hakuna kitu chochote kitakachoharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. w23.06 27:17-19
Jumapili, Julai 13
Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.—Ufu. 21:5.
Mstari wa 5 unaanza kwa kusema hivi: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema.” (Ufu. 21:5a) Maneno hayo ni ya pekee kwa sababu ni mojawapo ya sehemu tatu katika kitabu cha Ufunuo ambapo Yehova mwenyewe anazungumza. Kwa hiyo, uhakikisho huo unatolewa, si na malaika mwenye nguvu, au hata Yesu aliyefufuliwa, bali na Yehova mwenyewe! Jambo hilo linathibitisha kwamba tunaweza kutumaini maneno ya Yehova yanayofuata. Kwa nini? Kwa sababu Yehova ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Hivyo, maneno tunayosoma kwenye Ufunuo 21:5, 6 hakika yatatimia. Tuchunguze neno “Tazama!” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tazama!” limetumiwa mara kwa mara katika kitabu cha Ufunuo. Ni maneno gani yanayofuata baada ya alama ya mshangao? Mungu anasema: “Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” Ni kweli kwamba Yehova anazungumza kuhusu mabadiliko ya wakati ujao, lakini kwake, ahadi hiyo ni hakika na itatimia, hivi kwamba anayazungumzia mabadiliko hayo kana kwamba tayari yanatukia.—Isa. 46:10. w23.11 46:7-8
Jumatatu, Julai 14
Akaenda nje akalia kwa uchungu.—Mt. 26:75.
Mtume Petro alipambana na udhaifu wake mbalimbali. Fikiria mifano michache. Yesu alipoeleza jinsi ambavyo angeteseka na kufa ili kutimiza unabii wa Biblia, Petro alimkemea. (Marko 8:31-33) Petro na wale mitume wengine walibishana tena na tena kuhusu yule aliyekuwa mkuu zaidi kati yao. (Marko 9:33, 34) Usiku wa mwisho kabla ya kifo cha Yesu, Petro alimshambulia mwanamume fulani na kumkata sikio. (Yoh. 18:10) Usiku huohuo Petro alilemewa na woga na mara tatu akakana kwamba hamjui Yesu, rafiki yake. (Marko 14:66-72) Baada ya hapo Petro alilia kwa uchungu. Yesu hakumwacha mtume huyo aliyekuwa amevunjika moyo sana. Baada ya Yesu kufufuliwa, alimpa Petro fursa ya kuonyesha kwamba bado anampenda. Yesu alimwalika Petro awe mchungaji mnyenyekevu wa kondoo wake. (Yoh. 21:15-17) Petro aliitikia kwa njia nzuri. Alikuwa huko Yerusalemu siku ya Pentekoste na alikuwa miongoni mwa Wakristo wa kwanza kutiwa mafuta kwa roho takatifu. w23.09 40:6-7
Jumanne, Julai 15
Chunga kondoo wangu wadogo.—Yoh. 21:16.
Petro aliwahimiza hivi wazee wenzake: “Lichungeni kundi la Mungu.” (1 Pet. 5:1-4) Ikiwa wewe ni mzee wa kutaniko, tunajua kwamba unawapenda ndugu na dada zako, na unataka kuwachunga kiroho. Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ukahisi kwamba una shughuli nyingi sana au una uchovu mwingi sana hivi kwamba huwezi kutimiza mgawo huo. Unaweza kufanya nini? Mmiminie Yehova mahangaiko yako. Petro aliandika hivi: “Yeyote akihudumu, na afanye hivyo kama anayetegemea nguvu ambazo Mungu hutoa.” (1 Pet. 4:11) Huenda ndugu na dada zako wanakabili matatizo ambayo hayawezi kusuluhishwa kabisa katika mfumo huu wa mambo. Lakini kumbuka kwamba “mchungaji mkuu,” Yesu Kristo, anaweza kuwasaidia kwa njia nzuri zaidi kuliko unavyoweza. Anaweza kufanya hivyo leo na katika ulimwengu mpya. Mungu anataka wazee wawapende na kuwachunga ndugu zao na wawe “vielelezo kwa kundi.” w23.09 41:13-14
Jumatano, Julai 16
Yehova anajua kwamba kufikiri kwa watu wenye hekima ni ubatili.—1 Kor. 3:20.
Ni lazima tuepuke kutumia njia ya kufikiri ya wanadamu. Ikiwa tutaona mambo kulingana na maoni ya wanadamu, huenda tukampuuza Yehova na viwango vyake. (1 Kor. 3:19) Mara nyingi, “hekima ya ulimwengu huu” huchochea tamaa za mwili. Baadhi ya Wakristo huko Pergamamu na Thiatira waliwaiga watu waliowazunguka ambao walikuwa na maadili mapotovu na waliabudu sanamu. Yesu aliyapatia makutaniko hayo mawili shauri kali kwa sababu ya kuvumilia uasherati. (Ufu. 2:14, 20) Leo, tunashawishiwa kukubali maoni yasiyofaa. Huenda watu wa familia yetu na marafiki wakajaribu kutusadikisha kwamba tuna msimamo mkali sana na kwamba hatupaswi kufuata sheria za Yehova. Kwa mfano, huenda wakadai kwamba si jambo muhimu kuendelea kuwa safi kiadili na viwango vya maadili vya Biblia vimepitwa na wakati. Nyakati nyingine, huenda tukafikiri kwamba mwongozo ambao Yehova anatupatia hautoshi. Hata huenda tukashawishiwa ‘kupita mambo yaliyoandikwa.’—1 Kor. 4:6. w23.07 31:10-11
Alhamisi, Julai 17
Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.—Met. 17:17.
Maria, mama ya Yesu, alihitaji kutiwa nguvu. Angekuwa mjamzito, ingawa hakuwa amefunga ndoa. Hakuwa na uzoefu wa kulea watoto wake mwenyewe, lakini angemtunza mvulana ambaye baadaye angekuwa Masihi. Na kwa kuwa hakuwa amefanya ngono, Maria angemwelezaje jambo hilo Yosefu, mchumba wake? (Luka 1:26-33) Maria alipataje nguvu alizohitaji? Alitafuta msaada kutoka kwa watu wengine. Kwa mfano, alimwomba malaika Gabrieli ampe habari zaidi kuhusu mgawo huo. (Luka 1:34) Muda mfupi baada ya hapo, alisafiri kwenda kwenye “eneo lenye milima” la Yuda ili kumtembelea Elisabeti, mtu wake wa ukoo. Elisabeti alimpongeza Maria na aliongozwa na Yehova kusema unabii wenye kutia moyo kumhusu mwana wa Maria ambaye bado hakuwa amezaliwa. (Luka 1:39-45) Maria alisema kwamba Yehova alikuwa “amefanya mambo makuu kwa mkono wake.” (Luka 1:46-51) Kupitia malaika Gabrieli na Elisabeti, Yehova alimwimarisha Maria. w23.10 43:10-12
Ijumaa, Julai 18
Alitufanya tuwe ufalme, makuhani kwa Mungu na Baba yake.—Ufu. 1:6.
Idadi hususa ya wanafunzi wa Kristo wametiwa mafuta kwa roho takatifu, nao wana uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. Wakristo hao 144,000 watatumikia wakiwa makuhani mbinguni pamoja na Yesu. (Ufu. 14:1) Patakatifu pa hema la ibada panafananisha hali yao ya kuzaliwa kwa roho na kuwa wana wa Mungu wakiwa bado duniani. (Rom. 8:15-17) Patakatifu Zaidi pa hema la ibada panafananisha mbinguni, ambako Yehova anaishi. “Pazia” lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi lilifananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu ambao ulikuwa kizuizi cha kuingia mbinguni akiwa Kuhani Mkuu sana wa hekalu la kiroho. Kwa kuutoa uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu, Yesu alifungua njia ya uhai wa mbinguni kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta. Ili wapokee thawabu yao ya mbinguni, ni lazima wao pia wavue miili yao ya kibinadamu.—Ebr. 10:19, 20; 1 Kor. 15:50. w23.10 45:13
Jumamosi, Julai 19
Nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni.—Ebr. 11:32.
Gideoni alijibu kwa upole Waefraimu walipomkosoa. (Amu. 8:1-3) Hakujibu kwa hasira. Alionyesha unyenyekevu wa akili kwa kusikiliza mahangaiko yao, na kwa busara alifaulu kutuliza hali hiyo. Wazee wenye hekima wanamwiga Gideoni kwa kusikiliza kwa makini na kujibu kwa upole wanapokosolewa. (Yak. 3:13) Wanapofanya hivyo, wanachangia amani kutanikoni. Gideoni aliposifiwa kwa kuwashinda Wamidiani, alimwelekezea Yehova sifa. (Amu. 8:22, 23) Wazee wanawezaje kumwiga Gideoni? Wanapaswa kumsifu Yehova kwa mambo wanayotimiza. (1 Kor. 4:6, 7) Kwa mfano, mzee anaposifiwa kwa sababu ya uwezo wake wa kufundisha, anaweza kusema kwamba chanzo cha mwongozo huo ni Neno la Mungu, na sisi sote tunapata mazoezi katika tengenezo la Yehova. Nyakati nyingine, wazee wanaweza kujichunguza ili kuona kama wanajielekezea fikira. w23.06 25:7-8
Jumapili, Julai 20
Mawazo yangu si mawazo yenu.—Isa. 55:8.
Ikiwa sala yetu haijibiwi, huenda tukahitaji kujiuliza, ‘Je, ninasali kuhusu jambo linalofaa?’ Mara nyingi, huenda tukafikiri kwamba tunajua jambo ambalo linatufaa zaidi. Lakini inawezekana mambo tunayoomba hata yasitunufaishe. Ikiwa tunasali kuhusu tatizo fulani, huenda kukawa na suluhisho bora zaidi kuliko lile tunaloomba. Na labda baadhi ya mambo tunayoomba hayapatani na mapenzi ya Yehova. (1 Yoh. 5:14) Kwa mfano, fikiria mfano wa wazazi ambao walimwomba Yehova amsaidie mtoto wao abaki katika kweli. Hilo linaonekana kuwa ombi linalofaa. Hata hivyo, Yehova hamlazimishi yeyote kati yetu amtumikie. Anataka kila mmoja wetu, kutia ndani watoto wetu, wachague kumwabudu yeye. (Kum. 10:12, 13; 30:19, 20) Hivyo, wazazi wanaweza kumwomba Yehova awasaidie kugusa moyo wa mtoto wao ili aweze kuchochewa kumpenda Yehova na kuwa rafiki Yake.—Met. 22:6; Efe. 6:4. w23.11 49:5, 12
Jumatatu, Julai 21
Endeleeni kufarijiana.—1 The. 4:18.
Kwa nini kuwafariji wengine ni njia muhimu ya kuwaonyesha kwamba tunawapenda? Kulingana na rejeo fulani la Biblia, neno “kufarijiana” ambalo Paulo alitumia linamaanisha “kusimama kando ya mtu na kumtia moyo anapopata majaribu makali.” Hivyo, tunapotoa faraja tunamsaidia mwabudu mwenzetu anayekabili hali ngumu, asimame na kuendelea kutembea katika barabara ya uzima. Kila mara tunapomfariji ndugu au dada yetu, tunamwonyesha upendo mwabudu mwenzetu. (2 Kor. 7:6, 7, 13) Kuonyesha huruma na kufariji ni sifa zinazohusiana kwa ukaribu. Kwa njia gani? Mtu mwenye huruma huchochewa kuwafariji wengine na kujitahidi kuwapunguzia mateso yao. Hivyo, kwanza tunaonyesha huruma; kisha tunawafariji wengine. Ona jinsi Paulo anavyohusianisha huruma ya Yehova na faraja anayotoa. Paulo anamfafanua Yehova kuwa “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 Kor. 1:3. w23.11 47:8-10
Jumanne, Julai 22
Tushangilie tukiwa katika dhiki.—Rom. 5:3.
Wafuasi wote wa Kristo wanaweza kutazamia kupata dhiki. Fikiria mfano wa mtume Paulo. Aliwaambia hivi Wathesalonike: “Tulipokuwa pamoja nanyi, tulikuwa tukiwaambia mapema kwamba tutapatwa na dhiki, na imekuwa hivyo.” (1 The. 3:4) Na aliwaandikia hivi Wakorintho: “Hatutaki mkose kujua, akina ndugu, kuhusu dhiki tuliyopata . . . Hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu. (2 Kor. 1:8; 11:23-27) Leo pia, Wakristo wanaweza kutazamia kupatwa na dhiki ya aina fulani. (2 Tim. 3:12) Kwa sababu ya kumwamini Yesu na kumfuata, huenda marafiki na watu wa ukoo wakakutendea kwa ukatili. Je, unapata matatizo kazini kwa sababu ya azimio lako la kuendelea kuwa mnyoofu katika mambo yote? (Ebr. 13:18) Je, umekabili upinzani kutoka kwa serikali kwa sababu ya kuwaambia wengine tumaini lako? Hata tukabili dhiki ya aina gani, Paulo anasema tunapaswa kushangilia. w23.12 51:9-10
Jumatano, Julai 23
Mmeniletea taabu kubwa.—Mwa. 34:30.
Yakobo alikabili matatizo mengi. Wana wawili ya Yakobo, Simoni na Lawi, waliletea familia yao aibu, na kuliletea suto jina la Yehova. Isitoshe, Raheli, mke mpendwa wa Yakobo, alikufa alipokuwa akijifungua mtoto wao wa pili. Na kwa sababu ya njaa kali, Yakobo alilazimika kuhamia nchini Misri alipokuwa amezeeka. (Mwa. 35:16-19; 37:28; 45:9-11, 28) Licha ya matatizo hayo yote, Yakobo hakupoteza imani yake katika Yehova na katika ahadi Zake. Naye Yehova, akamwonyesha Yakobo kwamba alikuwa na kibali chake. Kwa mfano, Yehova alimbariki Yakobo kwa kumpa mali nyingi. Na wazia jinsi Yakobo alivyomshukuru Yehova alipoungana tena na mwanaye Yosefu—mwana ambaye alidhani alikufa muda mrefu uliopita! Urafiki wa karibu kati ya Yakobo na Yehova, ulimsaidia kukabiliana na majaribu yake kwa mafanikio. (Mwa. 30:43; 32:9, 10; 46:28-30) Ikiwa tutadumisha urafiki wa karibu pamoja na Yehova, sisi pia tunaweza kukabiliana kwa mafanikio na majaribu tusiyotarajia. w23.04 17:6-7
Alhamisi, Julai 24
Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.—Zab. 23:1.
Zaburi ya 23 ni wimbo unaotuhakikishia kwamba Yehova anatupenda na kututunza kwa wororo. Daudi, mwandishi wa zaburi hii, anaeleza kuhusu uhusiano wa karibu uliopo kati yake na Mchungaji wake, Yehova. Daudi alihisi akiwa salama kwa kumruhusu Yehova amwongoze, na alimtegemea Yehova kikamili. Daudi alijua kwamba upendo wa Yehova ungemfuatia sikuzote za maisha yake. Kwa nini alikuwa na uhakika huo? Daudi alihisi anatunzwa vizuri kwa sababu sikuzote Yehova alimpatia mahitaji yake. Pia, Daudi alifurahia urafiki na kibali cha Yehova. Ndiyo maana alikuwa na uhakika kwamba hata nini kitokee wakati ujao, Yehova angeendelea kumwandalia mahitaji yake. Kwa kuwa Daudi aliamini kwamba Yehova anampenda na angemtunza, hilo lilimsaidia asiogope, bali awe na furaha na aridhike.—Zab. 16:11. w24.01 4:12-13
Ijumaa, Julai 25
Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.—Mt. 28:20.
Tangu Vita vya Pili vya Ulimwengu, watu wa Yehova katika nchi nyingi wamefurahia amani ya kadiri na uhuru wanapoendelea na kazi ya kuhubiri. Isitoshe, kazi hiyo imekuwa na matokeo makubwa. Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza wanaendelea kuutegemea mwongozo wa Kristo. Wangependa maagizo wanayowapatia akina ndugu yapatane na maoni ya Yehova na Yesu. Na wanawatumia waangalizi wa mzunguko na wazee ili kuyapatia makutaniko mwongozo. Wazee watiwa-mafuta wako kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Kristo. (Ufu. 2:1) Bila shaka, wazee hao si wakamilifu na wanafanya makosa. Pindi fulani Musa na Yoshua walifanya makosa, kama ilivyokuwa kwa mitume pia. (Hes. 20:12; Yos. 9:14, 15; Rom. 3:23) Bado Kristo anamwongoza kwa makini mtumwa mwaminifu na wazee waliowekwa rasmi, na ataendelea kufanya hivyo. Hivyo, tuna kila sababu ya kutumaini mwongozo ambao anatupatia kupitia wale aliowaweka rasmi ili kuongoza. w24.02 8:13-14
Jumamosi, Julai 26
Iweni waigaji wa Mungu, kama watoto wapendwa.—Efe. 5:1.
Leo, tunaweza kumfurahisha Yehova kwa kuzungumza kumhusu kwa njia inayoonyesha kwamba tunamthamini na tunampenda sana. Tunapokuwa katika huduma, tunakumbuka kwamba lengo letu kuu ni kuwasaidia watu wamkaribie Yehova, na wahisi kama sisi tunavyohisi kumhusu Baba yetu mwenye upendo. (Yak. 4:8) Tunafurahi sana kuwaonyesha watu jinsi Biblia inavyomfafanua Yehova, inavyofunua upendo wake, haki, hekima, na sifa zake nyingine zenye kuvutia. Pia, tunamsifu Yehova na kumfurahisha kwa kujitahidi kumwiga. Tunapofanya hivyo, tunakuwa tofauti kabisa na watu katika ulimwengu huu mwovu. Huenda watu wakatambua kwamba tuko tofauti na kujiuliza kwa nini. (Mt. 5:14-16) Tunaposhughulika nao katika maisha ya kila siku, huenda tukapata fursa ya kuwaeleza kwa nini tunatenda kwa njia tofauti. Matokeo ni kwamba watu wanyoofu wanatamani kumkaribia Mungu wetu. Tunapomsifu Yehova kwa njia hizo, tunaufurahisha moyo wake.—1 Tim. 2:3, 4. w24.02 6:7
Jumapili, Julai 27
[Uweze] kutia moyo . . . na pia kuwakaripia.—Tito 1:9.
Ili uwe mwanamume Mkristo mkomavu, utahitaji kujifunza stadi zinazofaa. Stadi hizo zitakusaidia kutimiza majukumu yako kutanikoni, kupata kazi itakayokutegemeza wewe au familia yako, na zitakusaidia kuwa na uhusiano mzuri na wengine. Kwa mfano, jifunze kusoma na kuandika vizuri. Biblia inasema kwamba mwanamume mwenye furaha na mwenye mafanikio hutumia muda kila siku kusoma Neno la Mungu na kulitafakari. (Zab. 1:1-3) Kwa kusoma Biblia kila siku, atajua njia ya Yehova ya kufikiri ambayo itamsaidia kufikiria mambo kwa njia nzuri, na kujifunza jinsi ya kutumia Maandiko vizuri. (Met. 1:3, 4) Ndugu na dada zetu wanahitaji msaada wa wanaume wenye uwezo wa kufundisha na kuwapa ushauri unaotegemea Biblia. Ikiwa unajua kusoma na kuandika vizuri, utaweza kuandaa hotuba na maelezo yenye habari zenye kujenga na kuimarisha imani. Pia, utaweza kuandika mambo makuu kwa njia nzuri itakayokusaidia kujenga imani yako na kuwatia moyo wengine. w23.12 53:9-11
Jumatatu, Julai 28
Yule aliye katika muungano na ninyi ni mkuu kuliko yule aliye katika muungano na ulimwengu.—1 Yoh. 4:4.
Unapoogopa, tafakari mambo ambayo Yehova atafanya wakati ujao Shetani atakapoondolewa. Onyesho lililotolewa kwenye programu ya kusanyiko la eneo la mwaka wa 2014 lilionyesha baba akizungumza na familia yake kuhusu jinsi ambavyo maneno ya 2 Timotheo 3:1-5 yangesomwa ikiwa mistari hiyo iliyotabiriwa ingezungumzia hali zitakavyokuwa katika Paradiso. Alisema hivi: “Katika ulimwengu mpya, kutakuwa na nyakati zenye furaha sana. Maana watu watakuwa wenye kupendana, wenye kupenda mambo ya kiroho, wenye kiasi, wanyenyekevu, wenye kumsifu Mungu, wanaotii wazazi, wenye shukrani, washikamanifu, walio na upendo wa asili, wanaotaka makubaliano, wanaosema mema kuhusu wengine sikuzote, wanaojizuia, wapole, wanaopenda wema, wanaotumainika, wenye kutii, wanyenyekevu katika akili, wanaompenda Mungu badala ya kupenda raha, wakichochewa na upendo wa kweli kwa Mungu; nawe shikamana na watu hao.” Je, wewe huzungumza na watu wa familia yako au waabudu wenzako kuhusu jinsi maisha yatakavyokuwa katika ulimwengu mpya? w24.01 1:13-14
Jumanne, Julai 29
Nimekukubali.—Luka 3:22.
Tunafurahi sana kujua kwamba Yehova anawakubali watu wake wakiwa kikundi! Biblia inasema hivi: “Yehova anawafurahia watu wake.” (Zab. 149:4) Hata hivyo, wakati mwingine baadhi ya watu wanavunjika moyo na kujiuliza, ‘Je, Mungu ananikubali mimi binafsi?’ Watumishi wengi waaminifu wa Yehova walioishi nyakati za Biblia, pindi fulani walihangaishwa na mawazo kama hayo. (1 Sam. 1:6-10; Ayu. 29:2, 4; Zab. 51:11) Biblia inaonyesha wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kupata kibali cha Yehova. Jinsi gani? Ni lazima tuonyeshe kwamba tunamwamini Yesu Kristo na kubatizwa. (Yoh. 3:16) Hivyo, tunaonyesha hadharani kwamba tumetubu dhambi zetu na tumemwahidi Mungu kuwa tutafanya mapenzi yake. (Mdo. 2:38; 3:19) Yehova anafurahi tunapochukua hatua hizo ili kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye. Maadamu tunaendelea kufanya yote tuwezayo ili kuishi kulingana na ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu, Yehova anatukubali na kutuona kuwa rafiki zake wa karibu.—Zab. 25:14. w24.03 13:1-2
Jumatano, Julai 30
Hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.—Mdo. 4:20.
Tunaweza kuwaiga wanafunzi hao kwa kuendelea kuhubiri hata ikiwa wenye mamlaka watatuamuru tuache kuhubiri. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatusaidia kutimiza huduma yetu. Hivyo, sali ili upate ujasiri na hekima na umwombe Yehova akusaidie uvumilie licha ya matatizo. Wengi wetu tunakabiliana na changamoto za magonjwa au za kihisia, kufiwa na mpendwa wetu, hali fulani ngumu katika familia, mateso, au matatizo mengine. Na mambo kama vile mlipuko wa magonjwa na vita yamefanya iwe vigumu hata zaidi kushughulika na changamoto hizo. Mmiminie Yehova moyo wako. Mwambie kuhusu hali yako kama ambavyo ungemwambia rafiki wa karibu. Uwe na uhakika kwamba Yehova “atatenda kwa niaba yako.” (Zab. 37:3, 5) Kudumu katika sala kutatusaidia ‘kuvumilia chini ya dhiki.’ (Rom. 12:12) Yehova anajua mambo ambayo waabudu wake wanavumilia—yeye “husikia kilio chao cha kuomba msaada.”—Zab. 145:18, 19. w23.05 20:12-15
Alhamisi, Julai 31
Endeleeni kuhakikisha jambo linalokubalika kwa Bwana.—Efe. 5:10.
Tunapotaka kufanya maamuzi muhimu, tunahitaji “kuyafahamu mapenzi ya Yehova” na kisha tutende kupatana nayo. (Efe. 5:17) Tunapotafuta kanuni za Biblia zinazohusu hali yetu, kwa kweli tutakuwa tukitafuta mawazo ya Mungu kuhusu jambo hilo. Kisha, kadiri tunavyotumia kanuni za Mungu, ndivyo tutakavyoweza kufanya maamuzi mazuri. “Yule mwovu,” adui yetu Shetani, angependa tutumie muda mwingi kufuatilia mambo ya ulimwengu huu, hivi kwamba tukose wakati wa kufanya utumishi wetu kwa Mungu. (1 Yoh. 5:19) Inaweza kuwa rahisi sana kwa Mkristo kutanguliza mali, elimu, au kazi yake badala ya kutafuta fursa za kumtumikia Yehova. Ikiwa jambo hilo litatokea, itaonyesha kwamba Mkristo huyo ameathiriwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Kwa kweli, mali, elimu, au kazi si mambo mabaya, lakini hayapaswi kamwe kutangulizwa maishani mwetu. w24.03 12:16-17