Wagalatia
Kwa Wagalatia
1 Paulo, mtume, si kutokana na wanadamu wala kupitia binadamu fulani, bali kupitia Yesu Kristo na Mungu Baba, aliyemfufua yeye kutoka kwa wafu, 2 na ndugu wote walio pamoja nami, kwa makutaniko ya Galatia:
3 Na mwe na fadhili isiyostahiliwa na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na Bwana Yesu Kristo. 4 Alijitoa mwenyewe kwa ajili ya dhambi zetu ili kulingana na mapenzi ya Mungu na Baba yetu apate kutukomboa kutoka katika mfumo mwovu wa mambo uliopo, 5 kwake kuwe utukufu milele na milele. Ameni.
6 Mimi nastaajabu kwamba mnakuwa mkiondolewa upesi hivyo kutoka kwa Yule aliyewaita nyinyi kwa fadhili isiyostahiliwa ya Kristo hadi kwenye namna nyingine ya habari njema. 7 Lakini si nyingine; ila tu kuna watu fulani wanaowasababishia nyinyi taabu na kutaka kupotosha habari njema juu ya Kristo. 8 Lakini, hata ikiwa sisi au malaika kutoka mbinguni tungewatangazia nyinyi kuwa habari njema jambo fulani kupita lile tulilowatangazia nyinyi kuwa habari njema, acheni alaaniwe. 9 Kama ambavyo tumesema juu, sasa mimi pia nasema tena, Yeyote yule anayewatangazia nyinyi kuwa habari njema jambo fulani kupita lile mlilopokea, acheni alaaniwe.
10 Kwa kweli, je, sasa ni wanadamu ninaojaribu kushawishi au Mungu? Au je, ninatafuta sana kupendeza wanadamu? Kama ningekuwa bado ninapendeza wanadamu, mimi singekuwa mtumwa wa Kristo. 11 Kwa maana nawajulisha nyinyi, akina ndugu, kwamba habari njema iliyotangazwa nami kuwa habari njema si jambo fulani la kibinadamu; 12 kwa maana sikuipokea kutoka kwa mwanadamu, wala sikufundishwa hiyo, ila kupitia ufunuo wa Yesu Kristo.
13 Bila shaka, nyinyi mlisikia juu ya mwenendo wangu hapo zamani katika Dini ya Kiyahudi, kwamba kufikia hatua ya kuzidi mno nilifuliza kulinyanyasa kutaniko la Mungu na kuliangamiza kabisa, 14 nami nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa zaidi katika Dini ya Kiyahudi kuliko wengi wa umri wangu katika jamii yangu, kwa kuwa nilikuwa mwenye bidii zaidi sana kwa mapokeo ya baba zangu. 15 Lakini wakati Mungu, aliyenitenga mimi tangu tumbo la uzazi la mama yangu na kuniita kupitia fadhili yake isiyostahiliwa, alipoona vema 16 kufunua Mwana wake kuhusiana nami, ili nipate kutangaza habari njema juu yake kwa mataifa, mimi sikwenda mara moja kuingia katika mashauriano pamoja na mwili na damu. 17 Wala sikupanda kwenda Yerusalemu kwa wale waliokuwa mitume kabla yangu, bali nilienda zangu kuingia Arabuni, nami nikarudi tena Damasko.
18 Kisha miaka mitatu baadaye nilipanda kwenda Yerusalemu kumzuru Kefa, nami nikakaa pamoja naye siku kumi na tano. 19 Lakini sikuona mwingine yeyote wa wale mitume, ila tu Yakobo ndugu ya Bwana. 20 Sasa kuhusu mambo ninayowaandikia nyinyi, tazameni! machoni pa Mungu, mimi sisemi uwongo.
21 Baada ya hilo nilienda kuingia katika mikoa ya Siria na ya Kilikia. 22 Lakini nilikuwa sijulikani kwa uso na makutaniko ya Yudea yaliyokuwa katika muungano na Kristo; 23 yalikuwa tu na kawaida ya kusikia: “Yule mtu ambaye hapo zamani alitunyanyasa sasa anaitangaza habari njema juu ya imani ambayo hapo zamani aliangamiza kabisa.” 24 Kwa hiyo yakaanza kumtukuza Mungu kwa sababu yangu.