Wagalatia
2 Kisha baada ya miaka kumi na minne nilipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikichukua pia Tito pamoja nami. 2 Lakini nilipanda kwenda likiwa tokeo la ufunuo. Nami nikatokeza mbele yao habari njema ambayo ninahubiri miongoni mwa mataifa, hata hivyo, kwa faragha mbele ya wale waliokuwa watu wenye kutokeza, kwa kuhofu kwamba isije ikawa kwa njia fulani nilikuwa nikikimbia au nilikuwa nimekimbia bure. 3 Hata hivyo, wala Tito, aliyekuwa pamoja nami, hakushurutishwa kutahiriwa, ijapokuwa yeye alikuwa Mgiriki. 4 Lakini kwa sababu ya akina ndugu wasio wa kweli walioletwa ndani kimya-kimya, walioingia kisiri-siri ili kujasisi uhuru wetu tulio nao katika muungano na Kristo Yesu, ili wapate kutufanya sisi watumwa kabisa— 5 kwa hao sisi hatukuacha nafasi kwa njia ya kunyenyekea, la, hata kwa saa moja, ili kweli ya habari njema ipate kuendelea kuwa pamoja nanyi.
6 Lakini kwa upande wa wale walioonekana kuwa kitu fulani—namna yoyote ile ya watu waliokuwa hapo zamani haifanyizi tofauti yoyote kwangu—Mungu hafuati kuonekana kwa nje kwa mtu—kwangu, kwa kweli, watu hao wenye kutokeza hawakunipa kitu chochote kipya. 7 Bali, kinyume chake, walipoona kwamba mimi nilikuwa nimekabidhiwa habari njema kwa ajili ya wale wasiotahiriwa, kama vile Petro alivyokuwa nayo kwa ajili ya wale waliotahiriwa— 8 kwa maana Yeye aliyempa Petro nguvu zenye kuhitajika sana kwa ajili ya utume kwa wale waliotahiriwa alinipa mimi pia nguvu kwa ajili ya wale walio wa mataifa; 9 ndiyo, walipokuja kujua fadhili isiyostahiliwa niliyopewa, Yakobo na Kefa na Yohana, wale walioonekana kuwa nguzo, walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa kushiriki pamoja, ili sisi twende kwa mataifa, bali wao kwa wale waliotahiriwa. 10 Ila tu twapaswa kuwakumbuka walio maskini. Jambo hilihili mimi pia nimejitahidi sana kwa bidii kulifanya.
11 Hata hivyo, Kefa alipokuja Antiokia, mimi nilimkinza uso kwa uso, kwa sababu alipatikana mwenye kuhukumiwa hatia. 12 Kwa maana kabla ya kuwasili kwa watu fulani kutoka kwa Yakobo, alikuwa na kawaida ya kula pamoja na watu wa mataifa; lakini walipowasili, akaanza kujiondoa na kujitenga mwenyewe, kwa kuwahofu hao wa tabaka ya waliotahiriwa. 13 Wale wengine wa Wayahudi pia walijiunga naye katika kufanya kisingizio hicho, hivi kwamba hata Barnaba akaongozwa pamoja nao katika kisingizio chao. 14 Lakini nilipoona kwamba wao hawakuwa wakitembea kwa unyoofu kulingana na kweli ya habari njema, mimi nikamwambia Kefa mbele yao wote: “Ikiwa wewe, ingawa ni Myahudi, waishi kama mataifa wafanyavyo, na si kama Wayahudi wafanyavyo, ni jinsi gani wewe unashurutisha watu wa mataifa kuishi kulingana na zoea la Kiyahudi?”
15 Sisi tulio Wayahudi kwa asili, na si watenda-dhambi kutoka kwa mataifa, 16 tukijua kama sisi tujuavyo kwamba mtu hutangazwa kuwa mwadilifu, si kwa sababu ya kazi za sheria, ila tu kupitia imani kuelekea Kristo Yesu, hata sisi tumeweka imani yetu katika Kristo Yesu, ili tupate kutangazwa kuwa waadilifu kwa sababu ya imani kuelekea Kristo, na si kwa sababu ya kazi za sheria, kwa sababu kutokana na kazi za sheria hakuna mwili wowote utakaotangazwa kuwa wenye uadilifu. 17 Basi ikiwa sisi, katika kutafuta sana kutangazwa kuwa waadilifu kwa njia ya Kristo, sisi wenyewe pia tumepatikana kuwa watenda-dhambi, je, Kristo kwa kweli ni mhudumu wa dhambi? Hilo lisitukie kamwe! 18 Kwa maana ikiwa mambo yaleyale ambayo wakati mmoja niliyaangusha chini nayajenga tena, mimi najionyesha mwenyewe kuwa mkiukaji-sheria. 19 Kwa habari yangu, kupitia sheria nilikufa kuelekea sheria, ili nipate kuwa hai kuelekea Mungu. 20 Mimi natundikwa mtini pamoja na Kristo. Si mimi tena niishiye, bali ni Kristo aishiye katika muungano nami. Kwa kweli, uhai niishio sasa katika mwili naishi kwa imani iliyo kuelekea Mwana wa Mungu, aliyenipenda mimi na akajikabidhi mwenyewe kwa ajili yangu. 21 Mimi sisukumi kando fadhili isiyostahiliwa ya Mungu; kwa maana ikiwa uadilifu upo kupitia sheria, Kristo kwa kweli alikufa bure.