-
Luka 4:31-37Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya
-
-
31 Kisha akashuka kwenda jiji la Kapernaumu, huko Galilaya. Naye alikuwa akiwafundisha siku ya Sabato,+ 32 nao wakashangazwa na njia yake ya kufundisha,+ kwa sababu alikuwa akizungumza kwa mamlaka. 33 Basi katika sinagogi kulikuwa na mtu mwenye roho mwovu, naye akapiga kelele akisema:+ 34 “Ah! Kwa nini unatusumbua, wewe Yesu Mnazareti?+ Je, umekuja kutuangamiza? Ninajua wewe ni nani, Mtakatifu wa Mungu.”+ 35 Lakini Yesu akamkemea, akisema: “Nyamaza na umtoke.” Basi baada ya kumwangusha mtu huyo mbele yao, yule roho mwovu akamtoka bila kumuumiza. 36 Wote wakashangaa na kuanza kuambiana: “Anazungumza kwa mamlaka sana! Anawaagiza roho waovu kwa mamlaka na nguvu, nao wanatoka!” 37 Basi habari kumhusu zikazidi kuenea kila mahali katika maeneo yaliyokuwa karibu.
-