Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati
10 Sasa Wafilisti walikuwa wakipigana na Waisraeli. Na wanaume wa Israeli wakawakimbia Wafilisti, na wengi wakauawa kwenye Mlima Gilboa.+ 2 Wafilisti wakamkaribia sana Sauli na wanawe, nao wakamuua Yonathani, Abinadabu, na Malki-shua,+ wana wa Sauli. 3 Vita vikawa vikali sana dhidi ya Sauli, na wapiga mishale wakampata na kumjeruhi.+ 4 Ndipo Sauli akamwambia mtu aliyembebea silaha: “Chomoa upanga wako unichome nao, ili watu hawa wasiotahiriwa wasije kunitendea kikatili.”*+ Lakini mtu aliyembebea silaha hakutaka kufanya hivyo, kwa sababu aliogopa sana. Basi Sauli akachukua upanga na kuuangukia.+ 5 Mtu aliyembebea silaha alipoona kwamba Sauli amekufa, yeye pia akauangukia upanga wake mwenyewe na kufa. 6 Basi Sauli na wanawe watatu wakafa, na watu wote wa nyumba yake wakafa pamoja.+ 7 Watu wote wa Israeli waliokuwa bondeni* walipoona kwamba kila mtu amekimbia na kwamba Sauli na wanawe wamekufa, wakaanza kuyaacha majiji yao na kukimbia; kisha Wafilisti wakaja na kukaa humo.
8 Siku iliyofuata, Wafilisti walipokuja kuwavua waliouawa vitu walivyokuwa navyo, walimkuta Sauli na wanawe wakiwa wameanguka kwenye Mlima Gilboa.+ 9 Basi wakamvua mavazi yake, wakamkata kichwa na kuchukua silaha zake, nao wakatuma ujumbe kotekote katika nchi ya Wafilisti ili habari hizo zienezwe kwa sanamu+ zao na watu. 10 Kisha wakaweka silaha zake katika nyumba ya* mungu wao na kulitundika fuvu lake kwenye nyumba ya Dagoni.+
11 Wakaaji wote wa Yabeshi+ kule Gileadi waliposikia mambo yote ambayo Wafilisti walikuwa wamemtendea Sauli,+ 12 mashujaa wote wakaondoka na kubeba maiti ya Sauli na maiti za wanawe. Wakawaleta Yabeshi na kuzika mifupa yao chini ya mti mkubwa kule Yabeshi,+ nao wakafunga kwa siku saba.
13 Kwa hiyo Sauli alikufa kwa sababu hakuwa mwaminifu kwa Yehova kwa maana hakutii neno la Yehova,+ na pia kwa sababu alitafuta ushauri kutoka kwa mtu aliyewasiliana na roho+ 14 badala ya kutafuta ushauri kutoka kwa Yehova. Kwa hiyo Akamuua na kumpa Daudi mwana wa Yese ufalme.+