1 Jina la Mungu Katika Maandiko ya Kiebrania na Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo
“Yehova.” Kiebrania, יהוה (YHWH au JHVH)
Jina la pekee la Mungu, “Yehova” (Kiebrania, יהוה, YHWH), linapatikana kwanza katika Mwa 2:4. Hilo jina la Mungu ni kitenzi kisababishi cha Kiebrania הוה (ha·wahʹ, “kuwa”) kinachoonyesha tendo linaloendelea. Kwa hiyo, jina la Mungu linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Hiyo inaonyesha kwamba Yehova, kwa tendo linaloendelea, Ndiye anayejisababisha kuwa Mtimizaji wa ahadi, Yeye ambaye sikuzote hutimiza ahadi zake.
Watafsiri wa kisasa humkosea kabisa heshima Mungu aliye Mtungaji wa Maandiko Matakatifu, kwa kuliondoa au kulificha jina lake la pekee sana. Jina lake linapatikana mara 6,828 katika maandiko ya Kiebrania likiwa limeandikwa hivi: יהוה (YHWH au JHVH). Kwa kawaida herufi hizo huitwa Tetragramatoni (maana yake ni “jina lenye herufi nne”). Kwa kulitumia jina “Yehova,” tumeenda sambamba na yale maandishi ya kwanza wala hatukufuata mazoea ya kutumia majina ya cheo kama vile “Bwana,” “Adonai” au “Mungu” badala ya jina la Mungu, ile Tetragramatoni.
Jina “Yehova” linapatikana mara 6,973 katika Maandiko ya Kiebrania ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Kwa kweli Tetragramatoni inapatikana mara 6,828 katika Maandiko ya Kiebrania, kutia ndani maneno matatu ya majina yaliyounganishwa (Mwa 22:14; Kut 17:15; Amu 6:24) na mara sita katika utangulizi wa Zaburi (7; 18 [mara 3]; 36; 102). Tumetafsiri Tetragramatoni kuwa “Yehova” mara zote 6,828 isipokuwa katika Amu 19:18, ambapo kiwakilishi-nafsi cha kwanza, “yangu,” kilicho katika umoja kilisomwa badala ya jina la Mungu. Zaidi ya hayo, tumerudisha Tetragramatoni katika Kum 30:16; 2Sa 15:20 na 2Nya 3:1 kama ilivyo katika Septuajinti. Tumerudisha pia jina la Mungu katika Isa 34:16 na Zek 6:8 ambapo jina “Yehova” linapaswa kusomwa badala ya kiwakilishi-nafsi cha kwanza, “-angu,” kilicho katika umoja. Jina la Mungu lilirudishwa pia katika sehemu nyinginezo 141 ambapo Wasoferi walilibadili jina hilo na kusoma ʼAdho·naiʹ au ʼElo·himʹ.
Ili kuepuka kuvuka mipaka ya mtafsiri kwa kufasiri maandiko, tumetafsiri kwa uangalifu sana jina la Mungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, huku sikuzote tukifuata kwa makini sana Maandiko ya Kiebrania. Tumechunguza upatano kutoka kwenye tafsiri za Kiebrania zilizopo za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ili kuthibitisha tafsiri yetu.
Herufi za Kiebrania za Tetragramatoni (יהוה) zilitumiwa katika maandishi ya Kiebrania na katika Septuajinti ya Kigiriki. Kwa hiyo, hata ikiwa Yesu na wanafunzi wake waliyasoma Maandiko katika Kiebrania au Kigiriki, waliliona jina la Mungu. Yesu alipoenda kwenye sinagogi huko Nazareti, aliposimama akachukua kitabu cha Isaya na kusoma sura ya 61:1, 2 ambapo pana Tetragramatoni, alilitamka jina la Mungu. Jambo hilo linapatana na azimio lake la kuwajulisha watu jina la Yehova kama alivyosali kwa Baba yake: “Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni. . . . Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha.”—Yoh 17:6, 26.
Tumetafsiri jina la Mungu mara 237 katika tafsiri yetu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Matumizi hayo yanapatana na tafsiri kadhaa za Kiebrania ambazo zimerudisha jina hilo katika sehemu 237 za Maandiko ya Kigiriki.