Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 2/8 kur. 25-27
  • Kwa Nini Ninapaswa Kujifunza Biblia?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nini Ninapaswa Kujifunza Biblia?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho
  • Kupata Njia ya Kweli
  • Msaada Katika Kumkaribia Mungu
  • Thawabu kwa Juhudi Yako
  • Mungu Ni Nani?
    Biblia Inatufundisha Nini?
  • Ukweli Kumhusu Mungu
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Vijana Wenye Furaha Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • Vijana—Mnafuatia Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 2/8 kur. 25-27

Vijana Wanauliza. . .

Kwa Nini Ninapaswa Kujifunza Biblia?

“NINAPORUDI nyumbani kutoka shuleni, sitaki kujifunza tena. Nataka kwenda nje na kuwa na rafiki zangu!” Hayo yalikuwa maoni ya tineja aitwaye Ken kwa madokezo ya kwamba atumie wakati fulani akijifunza Biblia.

Kama ilivyo na matineja wengi, huenda ikawa hujatia bidii katika funzo la kibinafsi la Biblia. Pengine wewe huamini kwamba Biblia ni Neno la Mungu. Huenda ikawa kwamba wewe hata huhudhuria mikutano ya Kikristo. Lakini huenda ukahisi kwamba tayari unajua mambo ambayo Biblia hufundisha. Au huenda ukastaajabu: ‘Kwa nini nijifunze Biblia? Juhudi zangu zitanifaidi nini?’

Kutosheleza Mahitaji Yako ya Kiroho

Kuuliza maswali kama hayo si jambo baya au lenye kukosa staha. Kinyume cha hilo, huenda kukaonyesha kwamba unaanza kuona kile ambacho Yesu alikiita ‘uhitaji wa kiroho.’ (Mathayo 5:3, NW) Huo unatia ndani zaidi ya udadisi tu. Kama The New English Bible inavyotafsiri mstari huo, huo ni “uhitaji wa Mungu”—uhitaji wa kumjua Mungu kwa undani sana na kuelewa makusudi yake. Kwa mfano, ulipokuwa mtoto mchanga, huenda ikawa wazazi wako walikufundisha kweli za msingi za Biblia. Labda uliitikia waliyoyasema bila kutosadiki. Lakini ulipokuwa mtu mzima, huenda ikawa kwamba uliona uhitaji wa ‘kujaribu mambo yote’—ili kujua kama yale uliyofunzwa yalikuwa ya kweli au la.—1 Wathesalonike 5:21.

Tena, labda hukulelewa katika nyumba ya kidini. Je! hiyo yamaanisha kwamba huna uhitaji wa mambo ya kiroho? Hata kidogo! Fikiria hali katika nchi moja ambapo imani ya kutokuwapo kwa Mungu imeendelezwa kwa muda mrefu. Katika miaka ya karibuni, vijana huko wameonyesha kupendezwa kunakoongezeka katika dini. Mwanapropaganda mmoja ambaye hupinga dini alionyesha kati ya mambo mengine “kushindwa kwa wasioamini kuna Mungu kuandaa majibu ya kusadikisha kwa maswali juu ya umaana wa uchungu na mateso maishani.” Huenda ukajikuta ukijiuliza maswali kama hayo hayo—ushuhuda wa kwamba una uhitaji wa kiroho.

Hata hivyo, si dini zote zinazoandaa majibu ya kutosheleza. Kwa mfano Manishi aliye mchanga, alikua akiwa Mhindu, akiamini katika mamilioni ya miungu. Hata hivyo, yeye akiri hivi: “Nilianza kustaajabu, ‘Mungu ni nani?’” Na vijana wengi waliolelewa katika dini za Jumuiya ya Wakristo vivyo hivyo hawajapata majibu ya kutosheleza. Mtu aweza kutafuta wapi? Yesu Kristo ajibu: “Neno lako [Mungu] ndiyo kweli.”—Yohana 17:17.

Maarifa sahihi ya Neno la Mungu, Biblia, yaweza kutosheleza tamaa yako kwa ajili ya kweli za kiroho. Itajibu maswali yako juu ya utambulisho wa Mungu, sababu za hali za dunia zilizopo, na matumaini yako ya wakati ujao. Ni kweli, huenda ikawa umelelewa na wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova, na huenda ukahisi ya kwamba tayari wajua kadiri fulani ya ‘kweli.’ Lakini je, ‘umefahamu upana, na urefu, na kimo, na kina’ cha kweli za Biblia au maarifa yako ni ya kijuujuu tu? (Waefeso 3:18) Ikiwa ya pili ndiyo hali yako, unahitaji ‘kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ya ukamilifu,’ kwa kujifunza Biblia kikamili.—Warumi 12:2.

Kupata Njia ya Kweli

Je! umewahi kupewa maelezo yenye makosa ya jinsi ya kufika mahali ulipotaka kwenda? Wakati uliopoteza na bidii uliyotumia bure zaweza kukufadhaisha. Na bado, maisha za vijana wengi zinaelekea kwenye njia isiyo sawa! Biblia yasema hivi: “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu, lakini mwisho wake ni njia za mauti.”—Mithali 14:12.

Fikiria, kwa mfano, suala la maadili ya kingono. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 14 alisema hivi: “Hakuna jambo lolote la haki. Kuna maoni tu.” Ni kweli, tamaa ya kufanya ngono ni kubwa sana, hasa ukiwa kijana. Lakini isipozuiwa, tamaa hiyo inaweza kukupeleka kwenye “njia za mauti.” Kila mwaka, matineja wa U.S. milioni 2.5 hupata magonjwa ya kuambukizwa kingono. Wasichana wengi huwa akina mama wasioolewa au huua watoto wao kwa kutoa mimba! Na hata kama mimba au ugonjwa huenda ukazuiwa, ngono kabla ya ndoa sikuzote huleta hasira ya Mungu.—1 Wathesalonike 4:3.

Kwa hiyo kwa nini ujikwae katika “njia za mauti”? Biblia hutoa mwongozo wa wazi kabisa wa kukusaidia ‘uzikimbie tamaa za ujanani.’ (2 Timotheo 2:22) Hiyo inahusisha ‘kufisha’ si tamaa ya ngono ya kawaida katika ndoa ya kustahiwa, bali tamaa ya ngono isiyo ya kiadili. (Wakolosai 3:5) Kujifunza Biblia kwaweza kukusaidia kutimiza hilo. Kunaweza kukupa nguvu ya wema kukimbia kutoka kwa mabaya hata kama ubaya huo waonekana kuwa wenye kuvutia sana. Inaweza “kuwapa wajinga werevu, na kijana (au mwanamke) maarifa na hadhari” ili aweze kuepuka hali ziwezazo kuongoza kwenye mwenendo usio wa kiadili.—Mithali 1:4.

Dan aliye mchanga ni mmoja aliyefaidika kutokana na kujifunza Biblia. Ingawa alikiri kwamba matineja wasiojali kitu wanaonekana kuwa na furaha, asema pia ameona “watoto wakizaliwa nje ya ndoa, magonjwa ya ngono, na matatizo mengine mengi.” Auliza hivi: “Kama nisingejifunza Biblia, mimi ningekuwa nikiishije?” Biblia yaweza kukuokoa wewe, pia, kutokana na “njia za mauti.”

Msaada Katika Kumkaribia Mungu

Ingawa vijana wengi leo hudai kuamini katika Mungu fulani, imani katika Mungu wa kibinafsi inapotea vijana wanapokua. Makala katika jarida Adolescence ilionelea kwamba kwa vijana wengine, “wazo la Mungu ni gumu kuelewa.” Dini nyingi zimemfanya Mungu kuonekana kuwa fumbo kwa kuficha uhakika wa kwamba Mungu ana jina. Na hata hivyo, waweza kuhisije ukaribu na mtu ambaye hulijui jina lake?

Hata hivyo, Biblia yafunua kwamba, jina la Mungu ni Yehova, na hutumia jina hilo zaidi ya mara 7,000! (Zaburi 83:18) Kulijua jina hilo kunakufungulia njia ya kuwa na uhusiano wa pekee pamoja na Mwenyezi Mungu. Lakini hiyo inamaanisha zaidi ya kupendezwa na Biblia kijuujuu tu. Yasema 1 Mambo ya Nyakati 28:9: “Ukimtafuta, ataonekana nawe.” Hiyo inamaanisha kuchimba ndani ya Maandiko kwa juhudi ya kupata kumjua Yehova kindani.

Je! umefanya hivyo? Kwa mfano, waweza kueleza ni kwa nini Biblia yaongea juu ya Yehova akiwa na “macho,” “masikio,” “uso,” na “mkono”? (1 Petro 3:12; Ezekieli 20:33) Je! Biblia haisemi “Mungu ni roho”? (Yohana 4:24) Au unafahamu kadiri ya uwezo wa Mungu wa kukuchunguza, kujua kile utakachosema kabla hujakisema? (Zaburi 139:4) Na namna gani kuhusu sifa kuu za Mungu za upendo, hekima, haki na uwezo? Je! unaweza kueleza ni nini uliokuwa udhihirisho mkubwa zaidi wa upendo wa Yehova? (Yohana 3:16) Je! unajua tofauti kati ya roho ya Mungu na uwezo wake? (Mika 3:8) Unaweza kuthibitishaje kwamba Mungu ana hisia—na kwamba kuna uwezekano wa kuumiza hisia zake?—Zaburi 78:40.

Kuna njia moja tu ya kujibu maswali hayo—kwa kujifunza Biblia. Luther aliye mchanga amejifunza kwamba “kwa kujifunza Neno Lake, ninaweza ‘kuona’ utu wa Yehova, na ni mtu wa aina gani.” (Linganisha Ayubu 42:5) Jaquella pia amekuja kumjua Mungu vizuri zaidi. Kupitia funzo la Biblia, amekuja kuthamini “kwamba Yehova anaweza kutegemeza analosema. Anapoahidi jambo, havunji ahadi yake; hasemi uongo.”—Tito 1:2.

Thawabu kwa Juhudi Yako

Kujifunza Biblia kunahusisha jitihada na kudhabihu mwingine wa wakati wako wa starehe. Kuanza kwaweza kuwa kugumu na hata kunaweza kuleta dhihaka kutoka kwa familia na rafiki. Lakini tazama thawabu mbalimbali. Kujifunza Biblia kikawaida kumemsaidia Paula. Alisema, nilisitawisha “uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, ndugu zangu wa Kikristo, na familia yangu.” Sandy asema ilimsaidia “kujenga dhamiri” ambayo inafanya kazi hata kwa mambo madogo madogo. Asema: “Ninaweza kufikiria maandiko au kanuni za Biblia ambazo zinaweza kunisaidia kukata kauli nitakachotazama katika TV.” Na wamkumbuka Ken aliyetajwa mwanzoni? Alianza kusoma Biblia mara nyingi zaidi na asema hivi: “Kwa kadiri nilivyoendelea kusoma, ndivyo nilivyopendezwa zaidi, na nikaelewa zaidi.” Ken alichochewa kuwa mtumishi wa Mungu aliyebatizwa.

Kwa nini usianze funzo la maana la Biblia? Lione jambo hilo kuwa mwito wa ushindani. Uliza wazazi wako au mshiriki mmoja wa kundi la kwenu la Mashahidi wa Yehova akusaidie uanze. Piga moyo konde kutoacha. Tumia unachojifunza. Na ukumbuke: ‘Anayeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri [mwenye furaha, NW] katika kutenda kwake.’—Yakobo 1:25.

[Blabu katika ukurasa wa 26]

Je! ‘umefahamu upana, na urefu, na kimo, na kina’ cha kweli za Biblia au ujuzi wako ni wa kijuujuu tu?

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mzazi au mshiriki mwingine wa kundi la Kikristo waweza kukusaidia uanze mradi wa kusoma Biblia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki