Je, Nafsi Hufa?
HUENDA swali hilo liliingia akilini mwa mtu aliyesoma gazeti Time la Julai 30, 1990. Likizungumzia juu ya ongezeko kubwa la magari barabarani katika Ujerumani Mashariki kabla ya muungano wa zile Jerumani mbili katika Oktoba 3, 1990, gazeti hilo liliripoti katika makala yake “Kuendesha Kwa Kasi Kwenye Miinuko ya Barabara”: “Vifo vya barabarani katika Mashariki vilipanda kwa asilimia 60 katika miezi sita ya kwanza ya 1990, vikichukua nafsi 1,078.”
Makala hiyo kwa wazi ilimaanisha kwamba watu 1,078 waliuawa katika aksidenti za magari; walikufa. Lakini je, nafsi 1,078 zilikufa? Je, gazeti Time lilikosea kwa kutumia usemi “nafsi” kwa ajili ya watu wa nyama na damu? Nafsi ni nini?
Katika muda wote wa historia, kumekuwa na mawazo mbalimbali kuhusu nafsi. Watu wengi wa kale waliamini kwamba nafsi isiyokuwa na mwili iliendelea kuishi baada ya kifo, kwamba kifo kilikuwa, kama tokeo, mlango wa maisha mengine. Watawala fulani wa nyakati za kale hata walilazimisha kuuawa kwa watumishi wao katika wakati wa kifo chao wenyewe katika imani kwamba nafsi za watu hawa zingeendelea kuwatumikia.
Ingawa wengi leo pia wanaamini kwamba nafsi inamaanisha sehemu ya mtu isiyo ya kimwili, au roho, ambayo huokoka kifo cha mwili halisi, Biblia haifundishi hivyo. Kwa hakika, katika Hesabu 6:6, inazungumza juu ya “nafsi yoyote iliyokufa,”NW. La, nafsi siyo kitu fulani kisicho cha kimwili kilicho ndani yako. Wewe ni nafsi. Nafsi yaweza kufa, kama vile gazeti Time lilivyoripoti.
The Jewish Encyclopedia (1910) yasema hivi: “Ile imani kwamba nafsi huendelea kuwako baada ya kifo cha kimwili ni jambo la kufikiriwa tu au ni kisio la kitheolojia badala ya kuwa la imani sahihi, na kwa kupatana halikufunzwa kwa udhahiri katika Maandiko Matakatifu.”—Buku 6, ukurasa 564.