“Siku ya Mashahidi wa Yehova”
MASHAHIDI WA YEHOVA hufurahia kukusanyika pamoja kwa idadi kubwa-kubwa mara kadhaa mwakani. Wao hukusanyika ili wajifunze juu ya Mungu na kanuni zake adilifu. Mikutano hiyo pia ni fursa nzuri sana za kutiana moyo pamoja na Wakristo wenzi.—Waebrania 10:24, 25.
Vikundi hivi vikubwa vya wageni Mashahidi vina athari gani kwa majiji yaliyoteuliwa kwa ajili ya makusanyiko? Bila shaka, kuna faida kwa uchumi wa wenyeji. Lakini pia kuna athari kwa “kielelezo chao cha wakfu wa kiroho na mapambo ya kibinafsi,” kama ilivyosemwa katika tangazo lililotolewa na meya wa jiji la Gainesville, Georgia, Marekani.
Hati hii rasmi ilisema hivi kwa sehemu: “KWA MAANA, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakikutana Georgia Mountains Center kwa wastani wa miisho-juma 14 kila mwaka kwa miaka 11 iliyopita, kukiwa na hudhurio katika kila pindi la wastani wa watu 2,200; na . . . ‘wingu kubwa hili la Mashahidi’ kwa hakika limetoa ushuhuda wenye kusisimua wa imani na wakfu kwa wote ambao wameona hilo:
“KWA HIYO, SASA, MIMI, Emily D. Lawson, Meya wa Gainesville City, natangaza Jumamosi, Novemba 23, 1991, kuwa ‘SIKU YA MASHAHIDI WA YEHOVA’ katika Gainesville; nikiomba wakazi wote waitambue na wakaribishe wageni hawa kwa moyo mkunjufu, nao wajaribu kuiga kielelezo chao cha wakfu wa kiroho na mapambo ya kibinafsi, katika kila fursa mwisho-juma huu na wakati ujao.”