Maoni ya Biblia
Michango ya Kutoa Misaada—Wajibu wa Kikristo?
MUDA unaopungua miaka kumi iliyopita, Kilabu cha PTL (“Praise the Lord,” yaani, Bwana Asifiwe), chenye makao makuu katika kusini-mashariki mwa United States, kiliomba-omba michango kikiwa kikundi cha kidini cha kutoa misaada. Kikitumia mfumo wa TV-satelaiti na barua, kilipata mamia ya mamilioni ya dola, zilizokuwa zikimwagika kwa makasha yacho—eti ili kueneza evanjeli.
Ebu wazia jinsi walivyohisi maelfu ya watu ambao walikuwa wamepelekea Kilabu cha PTL fedha wakati waliposoma ripoti za habari kama ile ya shirika la habari la Associated Press iliyosema kwamba Jim Bakker, aliyekuwa msimamizi wa PTL, pamoja na mke wake, Tammy, “inaripotiwa kuwa walilipwa mshahara na fedha za ziada zinazofikia dola milioni 1.6 [za U.S.] katika 1986.” Na kwa ubaya zaidi, ripoti hiyo iliongeza hivi: “Malipo hayo yalitolewa hata ingawa chama hicho kina deni lisilopungua dola [za U.S.] milioni 50 . . . Sehemu ya fedha za PTL, dola [za U.S.] 265,000, zimewekwa kando kwa ajili ya [Jessica] Hahn ili kuhakikisha kwamba amenyamaza juu ya kisa chake [cha kingono] na Bakker.”
Kabla ya kuhukumu Bakker kwa sababu ya kupunja wafuasi wake fedha, hakimu aliyesimamia kesi yake alisema hivi: “Wale miongoni mwetu ambao wana dini wamechukizwa kuwa vitu vya kunyonywa na wahubiri na makasisi wenye kutafuta fedha sana.”
Si dini pekee inayovutia hisia za watu wenye kutoa michango na kisha kula sehemu kubwa ya fedha hizo. Ni jambo la kawaida kwa wengine wanaotafuta michango kuweka zaidi ya asilimia 90 ya michango wanayoomba.
Basi, ishangaze kwamba watu wamechoshwa na mashirika kama hayo ya kutoa misaada? Hata hivyo, Wakristo wafanye nini? Je! wana wajibu wa kutoa michango kwa mashirika hayo ya kutoa misaada? Biblia inatoa miongozo gani ili kuhakikisha kwamba fedha zinatumiwa kwa hekima wakati wa kuwasaidia wengine? Ni njia gani iliyo bora zaidi na yenye kufaa zaidi ya kuwasaidia wengine?
Kutoa Michango—Ndiyo na La
Kwa hakika, shauri la Biblia ni kuwa mwenye fadhili na mkarimu kwa wale wenye uhitaji. Kutokea nyakati za kale watu wa Mungu wametiwa moyo “wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo.” (1 Timotheo 6:18; Kumbukumbu la Torati 15:7, 10, 11) Kwa kweli, Wakristo wanaambiwa hivi katika 1 Yohana 3:17: “Mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?”
Ndiyo, toa; lakini jihadhari! Sisi huvamiwa kila mara na mashirika ya kutoa misaada, dini, na kampeni za utumishi za kila mwaka; mengi zaidi huomba kwa njia ya kushurutisha. Hata hivyo, katika kuyacha-nganua ni vizuri kukumbuka ile mithali ya Biblia: “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” (Mithali 14:15) Katika maneno mengine, jihadhari usiamini tu madai au ahadi zote za mashirika ya kutoa misaada. Fedha zilizokusanywa zinatumiwaje kwa kweli? Je! mashirika hayo yanayopokea fedha ni yale ambayo Mkristo anapaswa kuunga mkono? Je! utendaji wayo ni wa kisiasa, wa kutukuza taifa, au unahusika na dini bandia? Je! makusudi ya fedha hizo yanafaa na hayapingi kanuni za Kimaandiko?
Baadhi ya mashirika ya kutoa misaada yanasaidia sana watu wenye uhitaji. Wakristo wenyewe mara nyingi wamepokea misaada kutoka kwa mashirika kama hayo wakati wanapokumbwa na mikasa ya kiasili au ugonjwa unaoua. Ingawa hivyo, mashirika mengine ya kutoa misaada yana gharama za juu sana za kujiendesha au yanaomba fedha nyingi mno, hiyo ikimaanisha kwamba ni sehemu kidogo tu ya fedha zinazokusanywa inayotumiwa hasa kwa kusudi linalotajwa. Kwa mfano, uchunguzi wa karibuni wa mashirika 117 makubwa zaidi katika United States ambayo si ya kibiashara, kutia ndani mashirika ya kutoa misaada, uligundua kwamba zaidi ya robo ya mashirika hayo huwalipa maofisa wayo wa juu mshahara unaofikia dola za U.S. 200,000 au zaidi kila mwaka. Ukaguzi wa fedha mara nyingi hufunua matumizi ya fedha kwa vitu vya anasa na kwa kulipia maisha yenye utajiri mwingi. Hata jina la shirika liwe nini, haielekei kwamba kutoa michango kwa miradi kama hiyo kutatimiza amri ya Biblia ya kuwasaidia wale wenye uhitaji.
Maoni Yanayosawazika
Ingawa hakuna mtu anayetaka kutumia vibaya fedha zake—au kwa ubaya zaidi, kuona fedha zake zikitumiwa na watu wenye kujitumikia—kuna uhitaji pia wa kujilinda ili usidharau kutoa upaji. Usichukue jambo la kwamba “mashirika mengine ya kutoa misaada” hayafanyi kazi vizuri au hayafuatii mambo ya haki kuwa udhuru wa kutowasaidia wenye uhitaji au kuzuia hisi zako za huruma. Mithali 3:27, 28 lashauri hivi: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda. Usimwambie jirani yako, Nenda, urudi halafu, na kesho nitakupa; nawe unacho kitu kile karibu nawe.” (Linganisha 1 Yohana 3:18.) Usidhanie kwamba mashirika yote ya kutoa misaada ni ama yenye kutumia fedha vibaya ama yenye kupunja. Chunguza mambo ya hakika, kisha uamue binafsi kama utatoa upaji au la.
Wengi hupendelea kusaidia binafsi kwa kutoa zawadi moja kwa moja kwa watu mmoja mmoja na familia zenye uhitaji. Hivyo, watoaji wana uhakika wa utumizi unaofaa wa mara hiyo wa michango yao. Tendo hilo pia laandaa fursa ya kujenga na kuonyesha fadhili kwa maneno na kwa matendo vilevile. Hata kama huna mengi ya kutoa kimwili, waweza bado kuwa na shangwe ya kutoa. Wakati mwingine utakaposikia uhitaji wa kweli wa msaada kama huo, toa uwezacho kwa roho ya 2 Wakorintho 8:12: “Kama nia ipo, hukubaliwa kwa kadiri ya alivyo navyo mtu, si kwa kadiri ya asivyo navyo.”
Kumbuka pia kwamba nyakati nyingine kitu kiwezacho kufanya mema zaidi chaweza kuwa si fedha. Yesu aliwaambia wafuasi wake ‘waenende wakihubiri, wakisema, Ufalme wa mbinguni umekaribia. Mmepata bure, toeni bure.’ (Mathayo 10:7, 8) Vivyo hivyo leo, Wakristo wanatambua kwamba wakati, nishati, na fedha zinazotumiwa ili kutegemeza utoaji ushahidi kwa ajili ya Ufalme—kazi inayofanyia maendeleo maisha za watu na kutoa tumaini—ni utoaji wa misaada ulio bora zaidi.
Basi, maoni ya Biblia ni kuwa mwenye fadhili, mkarimu, na mwenye kutoa kwa hali inayofaa. Inatukumbusha kwamba mara nyingi kuna uhitaji wa kimwili, na uhitaji huo haupaswi kupuuzwa. Lakini usijihisi umeshurutishwa kutoa michango kwa yeyote na wote wanaoweza kukuomba fedha. Fikiria njia bora zaidi ya kutumia fedha zako ili kumpendeza Mungu na kutoa kwa njia ifaayo zaidi kwa familia yako mwenyewe na kwa binadamu mwenzako. (1 Timotheo 5:8; Yakobo 2:15, 16) Mwige Yesu kwa kuwa mwenye kuona na kuitikia mahitaji ya wengine—kiroho na kimwili. Kwa maneno ya Waebrania 13:16: “Msisahau kutenda mema na kushirikiana; maana sadaka kama hizo ndizo zimpendezazo Mungu.”