Tamaa ya Joshua
MNAMO Machi 6, 1992, familia ya Wood walitambua kwamba mshiriki wao mdogo zaidi, Joshua mwenye umri wa miaka saba, alikuwa anaugua ugonjwa wa leukemia (aina ya kansa) ambao huua. Kakaye Joshua, mwenye umri wa miaka 16, na dada yake, mwenye umri wa miaka 19, ni wahudumu wa wakati wote (mapainia) wa Mashahidi wa Yehova, kama ilivyo pia na baba yake. Ndugu mwingine wa Joshua ana umri wa miaka kumi.
Utibabu wenye bidii wa kutumia kemikali ulianzishwa mara hiyo ili kutibu ugonjwa wa Joshua. Dhara moja la matibabu lilikuwa kupoteza hamu ya chakula, kwa hiyo kila mara ilikuwa jitihada kumfanya Joshua ale. Katika Julai, familia nzima iliamua kuhudhuria pamoja mkusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova katika Lafayette, Louisiana, U.S.A., ambao haukuwa mbali na nyumbani kwao katika Winnfield. Alipokuwa huko, hali ya Joshua ikawa mbaya zaidi, na Jumamosi asubuhi alipelekwa kwenye chumba kimoja cha dharura cha hospitali. Baada ya mkusanyiko, wazazi wake walimpeleka katika hospitali moja katika New Orleans, ambako yeye hupata matibabu mara kwa mara.
Familia yao ilipokuwa New Orleans, mfanyakazi wa jamii alimweleza mama ya Joshua, April, juu ya programu ya kutimiza tamaa za watoto ambao ni wagonjwa mahututi. April aliachiwa fomu ya maombi ya programu hiyo, naye na mume wake, Paul waliijaza. Joshua aliporudishwa New Orleans mwishoni mwa mwezi wa Agosti kwa ajili ya uchunguzi wake wa kila mwezi, Jim, mtu anayewakilisha ile programu alikuja aseme na Joshua juu ya tamaa yake.
“Ninataka kwenda New York,” Joshua akasema.
Na kwa sababu mara nyingi watoto hutaka kutembelea sehemu zenye kufurahisha, Jim akauliza ni kwa nini Joshua alitaka kwenda New York. “Nataka kuona Watchtower Society,” akajibu Joshua.
“Hiyo ni nini?” Jim akauliza.
“Wajua, huko ndiko wanakotengeneza magazeti, Biblia, vitabu, na trakti.”
April akaelezea Jim zaidi juu ya makao makuu ya Mashahidi wa Yehova na kazi ya kuchapa inayoendelea huko. “Ndugu yangu anazuru huko sasa hivi,” akasema Joshua, “na ningependa niende na familia yetu yote.”
Baada ya kujua kwamba kuna watu sita katika familia hiyo, Jim alimwuliza Joshua kama angependelea kwenda Disney World (mahali pa kujifurahisha) katika Florida badala ya huko. Joshua alikuwa na uhakika wa kutaka kwenda New York. Jim akaeleza kwamba hakujua kama ombi hilo lingeweza kutimizwa lakini angelifuatilia. Jim akamwuliza Joshua chaguo lake la pili.
“Kompyuta ya IBM,” akajibu Joshua.
“Mbona IBM?” Jim alitaka kujua.
Joshua akasema kwamba ili aweze kupata Biblia katika disketi kutoka kwa Watch Tower Society. (Joshua alijua kwamba disketi hiyo ya Biblia ni ya kompyuta za IBM.) Kisha Jim akauliza tena: “Una uhakika hutaki kwenda Disney World?”
“Nina uhakika,” akasema Joshua.
Siku chache baadaye, Jim alirudi kumweleza Joshua kwamba tamaa yake ya kwenda New York pamoja na familia yao ilikubaliwa. “Josh ni aina ya mtoto ambaye huwa mtulivu sana kwa mambo ambayo husisimua watu wengi,” mama yake akaeleza, “lakini nilichachawa!”
Mnamo Septemba 30, familia ya akina Wood ilienda kwa ndege kutoka New Orleans hadi Jiji la New York. Hakuna mmoja wao aliyekuwa amepata kuzuru vifaa vya Watchtower, ila Buddy, mwana wao mkubwa, ambaye alikuwa amekuwa huko majuma machache tu yaliyokuwa yamepita. Wote sita walikaa katika hoteli ya Ramada Inn katika Manhattan, New York, na walipewa gari la kuwasafirisha hadi kwenye majengo ya usafirishaji, uchapaji, ofisi, na makao kwa kuvuka Mto East katika Brooklyn.
Wakati wa siku mbili walizokuwa huko, familia hiyo ilitembezwa kwenye vifaa vya makao makuu. Siku moja walitembelea majengo ya ofisi na lile jengo kubwa la kiwanda lenye orofa tano. Siku iliyofuata walizuru jengo lenye upana wa meta za mraba tisini-elfu ambamo mna shughuli za usafirishaji, urudufishaji wa kanda, na utendaji mwingine mbalimbali, na vilevile wakatembelea baadhi ya majengo 21 ya makao yenye kukaliwa na wale wafanyakazi wenye kujitolea zaidi ya elfu tatu. Wakati familia hiyo ilipokaa huko, mipango ya pekee ili-fanywa ili wafurahie milo mitatu pamoja na wafanyakazi wa makao makuu, na wale chakula katika chumba kimoja kati ya vile vyumba kumi vya mlo.
Mnamo Oktoba 3, familia ilikodi gari na kwenda kilometa 160 kaskazini ili kuzuru Watchtower Farms. Walitembelea jengo kubwa la kuchapa huko na pia wakaona mahali chakula kingi cha wafanyakazi wa makao makuu hukuzwa. Katika alasiri, familia hiyo ilizuru Watchtower Educational Center iliyokuwa bado inajengwa, iliyoko karibu na Patterson, New York, karibu mwendo wa saa moja kwa gari kutoka Watchtower Farms, na kisha ikarudi New York usiku.
Siku iliyofuata walipelekwa kwa gari kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kennedy kilichoko New York kwa safari yao ya kurudi New Orleans. Tamaa ya Joshua ya kuona “wanakotengeneza magazeti, Biblia, vitabu, na trakti” ilikuwa imetimizwa. Familia ya Wood inashukuru sana kwa programu hiyo ya kutimiza tamaa ya watoto wagonjwa kwa kugharimia kila kitu katika safari yao yenye kujenga kiroho.
Majuma kadhaa baadaye, katikati ya Novemba, akiwa kwenye hospitali ya New Orleans kwa ajili ya utibabu wake wa kila mwezi, Joshua alialikwa awe mgeni wa mwimbaji maarufu wa nyimbo za utaratibu na za tamaduni za magharibi Garth Brooks kwenye moja ya maonyesho yake katika Monroe, Louisiana. Baadaye, Joshua na baba yake walipoalikwa na Bwana Brooks waende nyuma ya jukwaa, Joshua alimpatia nakala ya kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani cha kusaidia kujifunza Biblia. Joshua alipomwuliza Bwana Brooks hali ya mtoto wake (ana binti mchanga), huyo alivutiwa sana na kupendezwa kwa Joshua.
Kwa kweli inafariji wakati mtoto anapohangaikia mapendezi ya wengine, hasa ikiwa mambo anayochagua yaonyesha kupendezwa na mambo ya kiroho! Kama ungeulizwa tamaa yako, je, ungechagua jambo ambalo lingekufaidi wewe na wengine kiroho?
[Picha katika ukurasa wa 16, 17]
Walikozuru Joshua na familia yao
Kulia: Watchtower Educational Center
Chini: Jengo la ofisi za Watchtower
Kushoto: Jengo la 360 Furman, lenye Idara ya Usafirishaji
Chini: Jengo la kiwanda
Kushoto: Watchtower Farms na jengo la kuchapia