Yoshua na Akusaidie Wewe Umtumikie Yehova kwa Uhodari!
“ULIMWENGUNI mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.” Huenda ukawa unatambua kwamba maneno hayo yalisemwa na mwanamume ambaye jina lake aliitwa Yesu. Hata hivyo, kama ungejua Kiebrania, jina Yoshua lingekuja akilini mwako, kwa maana Yesu ni namna ya Kigiriki ya jina la Kiebrania Yoshua.—Yohana 16:33.
Kwa kufaa, kuwa hodari (kujipa moyo) pia ni wazo kuu katika kitabu cha Biblia kilichoandikwa na mtangulizi wa Yesu, Yoshua mwana wa Nuni. Lakini huenda ukauliza, sisi binafsi tunaweza kufaidikaje na kitabu cha Yoshua? Ebu tuanze na wazo hilo la kuwa hodari.
Mwanamume Mwenye Uhodari
Musa alipokuwa akifikia mwisho wa maisha yake, Yehova alichagua Yoshua awe mrithi wake, ambaye kwa hakika hakuwa mtu asiye na ujuzi wala kijana ambaye hajazoezwa. Yoshua alikuwa amezaliwa akiwa mtumwa katika Misri, lakini baada ya Kutoka alijipa sifa kuwa kiongozi shujaa kwa kusukumia mbali shambulio lisilo na sababu la Waamaleki. (Kutoka 17:8-16) Yoshua alithibitisha ushujaa wake na imani yake wakati, kati ya wale wanaume 12 waliopelekwa wakaipeleleze nchi ya Kanaani, ni yeye na Kalebu tu walioripoti bila woga kwamba kwa msaada wa Yehova Wakanaani wasio na adili wangefagiliwa mbali kisha Nchi ya Ahadi itwaliwe.—Hesabu 13:1–14:9.
Kwa kuwa Musa hakuruhusiwa aingie katika Nchi ya Ahadi, alimwambia Yoshua hivi: “Uwe hodari na moyo wa ushujaa, maana utakwenda pamoja na watu hawa hata nchi [Yehova] aliyowaapia baba zao, ya kwamba atawapa; nawe utawarithisha.”—Kumbukumbu la Torati 31:7, 23.
Basi, unaweza kuona ni kwa sababu gani tunaweza kutazamia kujifunza kwa kitabu cha Yoshua jinsi alivyokuwa hodari na jinsi sisi tunavyoweza kuwa hodari. Kwa kweli, zaidi ya nusu ya mara ambazo maneno “hodari” na “ushujaa” yanaonekana pamoja katika mstari wa Biblia ni katika kitabu cha Yoshua au katika maelezo yanayomhusu yeye. Kwa mfano, tunapoanza kusoma kitabu hicho tunaona shauri ambalo Yehova anampa Yoshua: “Uwe hodari tu na ushujaa mwingi, uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu; usiiache, kwenda mkono wa kuume, au wa kushoto, upate kufanikiwa sana kila uendako.” (Yoshua 1:7) Ebu tuangalie baadhi ya visa ambavyo Yoshua alionyesha ushuhuda wa kuwa na uhodari wa ndani wa imani na pia uhodari wa nje wa tendo. Halafu tutaweza kuona ni masomo gani ambayo sisi binafsi tunaweza kujifunza kwa mambo hayo.
Imani na Vitendo vya Uhodari
Mara baada ya Yehova kumsihi Yoshua awe “hodari tu na ushujaa mwingi,” alianza matayarisho ya kuongoza Israeli wavuke Yordani na kuingia nchi ya Kanaani. Yoshua alielekeza hivi: “Fanyeni tayari vyakula; kwa maana baada ya siku tatu mtavuka mto huu wa Yordani, ili kuingia na kuimiliki nchi awapayo [Yehova], Mungu wenu.” (Yoshua 1:11) Kwa hiyo imani yenye uhodari haikumwongoza Yoshua awe na maoni kwamba wangeweza kujikalia tu na kungojea Yehova afanye kila jambo. Jitihada ya kibinafsi ilihitajiwa. Hali moja na hiyo, tunahitaji imani na uhodari kufuata shauri la Yesu la kumtumaini Mungu atusaidie tupate chakula na mavazi ya kutosha. Lakini ahadi ya kupewa msaada huo haimaanishi kwamba tunaweza kujikalia tu bila kufanya lo lote kujitegemeza wenyewe.—Mathayo 6:25-33.
Tatizo lililokuwa hapo mbele tu ya Yoshua lilikuwa kuvuka Mto Yordani wakati wa masika maji yalipokuwa yamefurika na kuvuka kulikuwa hatari sana. (Yoshua 5:10) Yoshua hakuwaza hivi, ‘Huenda ikawa vizuri kungojea mpaka katikati ya kiangazi wakati kina cha maji kinaposhuka.’ Mungu alisema atende, na Yoshua alifanya hivyo kwa uhodari. Je! wewe unaona somo katika jambo hilo? Inapokuwa ni wakati wa sisi kufanya jambo lo lote kuhusiana na ibada ya kweli, tunahitaji kutenda kwa uhodari, badala ya kuwa na maelekeo ya kukawia mpaka mambo yaonekane kuwa mazuri zaidi au yenye kufaa zaidi. Ndiyo, tenda, kama alivyofanya Yoshua.—Mhubiri 11:4; Yakobo 4:13, 14.
Akionyesha kwamba Yeye alikuwa pamoja na Yoshua, Mungu alimwelekeza aambie makuhani wabebe sanduku la agano mpaka kwenye mto huo uliofurika. Walipokanyaga ndani ya maji, mto ukatengana. Halafu taifa likaweza kuvuka kama kwamba ni juu ya nchi kavu., Badala ya yeye binafsi kujitwalia sifa kwa ajili ya jambo hilo, Yoshua alifuata uelekezo wa Yehova akajenga katika Gilgali (salama ng’ambo ya magharibi) ukumbusho wa mawe yaliyotwaliwa kwenye sakafu ya mto. Jambo hilo lilikuwa la kukazia kwamba ‘mkono wa Yehova ni wenye uweza, ili wamche milele.’ (Yoshua 3:5-4:24) Ingawa sisi binafsi hatuwezi kuona ukumbusho huo wa mawe, mambo ambayo Yehova alifanya kupitia Yoshua yapasa kusitawisha uhakika wetu katika uweza wa Mungu wa kutenda kwa ajili ya watu wake. Umaana wa ukumbusho huo hakika ungekuwa wenye kusudi kwa Waisraeli waliokuwa wakikabili mji wenye ngome wa Kikanaani wa Yeriko.
Je! Yoshua, akiwa amiri-jeshi asiyeogopa, angeongoza Waisraeli washambulie kwa wingi mji huo uliozungushwa kuta? Huenda ukajua kwamba badala ya kufanya hivyo Yoshua alifuata maelekezo ya Mungu. Maelekezo ya kufanya nini? Kuamuru wanaume wake wenye silaha wapige hatua wakiwa kimya kila siku kuuzunguka mji huo wakifuatwa na makuhani, wengine wakipiga tarumbeta na wengine wakibeba lile Sanduku. Katika siku ya saba walipiga hatua mara saba, kisha “watu waliposikia sauti ya tarumbeta hao watu wakapiga kelele kwa sauti kuu sana, na ule ukuta [wa Yeriko] ukaanguka nchi kabisa.” Hilo likawezesha wanaume wa Yoshua washambulie ndani ya mji na kuuharibu. Ndiyo, ulikuwa ushindi kamili!—Yoshua 6:20.
Kwa Uhodari Walio Thabiti, Lakini Wenye Kiasi
Tunaweza kuthamini sehemu nyingine ya uhodari wa Yoshua kwa matukio mawili yaliyotokea halafu. La kwanza lilihusu mji wa Ai uliokuwa jirani. Waisraeli walipoushambulia, walifukuzwa mbio-mbio. Kwa sababu gani? Kwa sababu, kinyume cha amri ya Mungu, Akani alikuwa ametwaa nyara kutoka Yeriko. Huenda watu wengine wakaona aliyofanya yalikuwa sawa kwa kuwa vitu alivyochukua vilikuwa vyenye mafaa na haikuonekana kwamba kwa yeye kufanya hivyo angemuumiza mtu ye yote. Huenda ukawa umekwisha kusikia kuwaza kwa namna hiyo kuhusiana na wivi mdogo-mdogo wa kumwibia tajiri wa kazi au ukosaji mwingine “mdogo-mdogo.” Yoshua alitendaje?
Kwa msaada wa kimungu Yoshua alimtambua mkosaji na kuthibitisha uhalifu huo kwa kuvipata vitu vilivyoibwa. Vitu hivyo vilionekana kuwa visivyo na thamani kama nini! Lakini Yoshua alifukua kiini cha jambo hilo, akamwambia Akani hivi: “Mbona umetufadhaisha hivi? [Yehova] atakufadhaisha wewe leo.” (Yoshua 7:25) Yoshua, akiwa thabiti kwa ajili ya uadilifu, aliamuru mtenda-dhambi huyo auawe, na hivyo akafungua njia ya Ai kuweza kushindwa. Tukiwa tunakumbuka kushughulika kwa Yoshua na kesi ya Akani, huenda tukakifiria hivi, ‘Je! mimi ninakata maneno hivyo wakati washirika kazini pangu au shuleni wanapochukua vyepesi vitendo vilivyo haramu au visivyo vya uadilifu?’
Sasa fikiria tukio la pili, ambalo lilihusu wakaaji Wakanaani wa Gibeoni. Waliposikia juu ya ushindi wa Yoshua juu ya Yeriko na Ai, kwa ujanja walituma wanaume wenye kuonekana kama wasafiri kutoka nchi ya mbali ambao walitaka kufanya agano la amani na Israeli. Nao walifanya hivyo. Ndipo ikajulikana kwamba kwa kweli wanaume hao walikuwa wametoka katika Gibeoni uliokuwa karibu, na Waisraeli wengi wakaanza kulalamika juu ya namna jambo hilo lilivyokuwa limeshughulikiwa. Je! Yoshua angekasirika sana kwa ajili ya ujanja huo aagize Gibeoni uharibiwe?
Agano lilikuwa limefanywa, na Yoshua aliliheshimu. Alielekeza kwamba Wagibeoni kuanzia wakati huo wapewe mgawo wa kuteka maji na kukusanya kuni kwa ajili ya nyumba ya Mungu. Wagibeoni walikubali kufuata mpango huo, na matukio baada ya muda mfupi yakaonyesha kwamba Yoshua, pia, angeufuata. Jinsi gani? Wafalme watano Wakanaani kutoka eneo hilo waliungana na kupiga hatua kuja kushambulia Gibeoni. Yoshua alitenda haraka, na, baada ya kupiga hatua usiku kucha, akashambulia muungano huo. Yehova alisaidia kwa kunyesha mvua ya mawe yenye kuua juu ya jeshi la Wakanaani hao halafu kwa muujiza akafanya jua lisisonge kwa siku moja ili Waisraeli wawamalize kabisa. Kwa kukumbuka Wagibeoni, tukifanya mapatano au kuahidi jambo fulani lisilopingana na kanuni za Mungu, je, tutakuwa hodari kwa uthabiti kama Yoshua? Je! tunatimiza ahadi yetu hata ikiwa ni ngumu au haitufai?—Zaburi 15:4.
Jambo lenye maana ni kwamba baada ya kupigana huko kulikotoka kutajwa tu, na wakati ambao wafalme hao maadui watano walikuwa wauawe, Yoshua aliwasihi watu wake hivi: “Msiche, wala msifadhaike; iweni hodari, na wa mioyo ya ushujaa; kwa kuwa ndivyo [Yehova] atakavyowafanyia adui zenu zote, ambao mwapigana nao.” (Yoshua 10:25) Kuwa hodari na wenye mioyo ya ushujaa kungewafaa Waisraeli walipokuwa wakiendesha ushindi ambao Mungu aliagiza kwanza upande wa kusini halafu kaskazini ambako mfalme wa Hazori pia alifanya muungano usiofaa kitu wa kupigana na Israeli. Ingawa hawakuwa wameendelea kiufundi kama Wakanaani, ambao walikuwa wamekwisha kufanya miji yao kuwa ngome na wenye magari ya silaha, Waisraeli walitekeleza mapenzi ya Yehova kwa uhodari.
Masomo Mengine Kutokana na Yoshua
Tumechunguza hasa masomo yaliyomo katika kitabu cha Yoshua yanayohusiana na uhodari wake. Lakini unapokisoma kitabu chote huenda ukaona masomo mengine yanayofaa.
Kwa mfano, wanawake wengi wamevutiwa na nia ya Rahabu, ambaye alilinda Waisraeli wawili waliokuja kupeleleza Yeriko. Wakanaani walio wengi, waliposikia matendo makuu ya Mungu kwa ajili ya Israeli, wakawa wenye kujikinga na wenye kupinga Israeli kwa woga. Lakini si Rahabu. Yeye alikuwa na nia ya kwenda kinyume cha watu wake mwenyewe na kuhatirisha maisha yake ili apate fadhili za upendo za Yehova. Pia alifanya aliyoweza ili asaidie watu wake wa ukoo wajifunze waliyohitaji kufanya ili maisha yao yalindwe. Hakika tungeweza kutumia masimulizi hayo kusaidia wanawake leo waone umaana mkubwa wa ibada ya kweli kuliko uhusiano wao na jirani zao au hata taifa lao.—Yoshua 2:8-14.
Utaona somo zuri kuhusu Yoshua juu ya kutohukumu vibaya makusudi ya wengine. Linahusu wakati ule, baada ya sehemu kubwa ya Kanaani kutiishwa, Yoshua alipogawanya nchi hiyo kulingana na urithi wa kikabila. Wanaume kutoka makabila mawili na nusu walikuwa wakirudi kwenye eneo lao upande wa mashariki wa Yordani. Walipokuwa wakirudi, walijenga madhabahu. Yale makabila mengine yakafanya haraka kukata maneno—wakakata maneno vibaya—kuhusu maana ya madhabahu hiyo. Kukawa hatari ya vita vya kikabila kutokea. Unaposoma masimulizi katika Yoshua sura ya 22, uangalie somo hilo la kuwa waangalifu kutotungia wengine nia mbaya kwa matendo yao. Na pia, angalia jambo ambalo ingekuwa vizuri kufanya ikiwa una maoni ya kwamba mwingine amekudharau au kutenda isivyofaa.
Hakuna uchunguzi wo wote wa kitabu cha Yoshua unaopasa kukosa kukazia juu ya kujifunza na kushikamana na ibada ya kweli ambayo msingi wake ni Neno la Mungu. Mungu alimshauri Yoshua asome Neno lake kwa ukawaida wala asiache kufuata njia yalo. (Yoshua 1:8) Baada ya ushindi katika Ai, Yoshua aliongoza taifa lote kuelekea kaskazini kwenye eneo la Shekemu, katika Mlima Ebali na Mlima Gerizimu. Huko akajenga madhabahu kwa ajili ya kutoa dhabihu, halafu “akaandika huko juu ya mawe hayo nakala ya torati ya Musa.” (Yoshua 8:32) Zaidi ya hilo, akawasomea watu torati. “Hapakuwa na hata neno moja katika hayo aliyoamuru Musa, ambalo Yoshua hakulisoma mbele ya kusanyiko lote la Israeli, na mbele ya wanawake, na watoto, na wageni waliokaa nao.”—Yoshua 8:35.
Baadaye, Yoshua akiwa ameishi kwa muda fulani katika mji ambao kwa kiasi alikuwa ameomba kuwa urithi, aliwakusanya watu tena, na kusema: “Mimi ni mzee, nami nimekwendelea sana katika miaka yangu; nanyi mmeona mambo yote ambayo [Yehova], Mungu wenu, amewatenda mataifa haya yote kwa ajili yenu; kwa maana [Yehova], Mungu wenu, ndiye aliyewapigania ninyi.” Kwa hiyo akawasihi hivi: “Iweni mashujaa sana, kuyashika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha torati ya Musa, na kuyatenda, msiyaache kwa kugeukia upande wa kuume wala upande wa kushoto . . . bali shikamaneni na [Yehova].” Ili kiwe kichocheo cha kufanya hivyo, aliwakumbusha hivi: “Mnajua mioyoni mwenu . . . ya kuwa halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu, katika habari zenu; yote yametimia kwenu, hapana neno lo lote mlilopungukiwa.”—Yoshua 23:2-8, 14.
Mwishowe, kwa mara nyingine akawaita watu wakusanyike awape maonyo ya mwisho na kuwasihi hivi: “Chagueni hivi leo mtakayemtumikia;... lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia [Yehova].” Wao, pia, walipomhakikishia wangefanya hivyo, yeye alifanya agano pamoja nao. Maandishi ya kimungu yanasema: “Ikawa, baada ya hayo, Yoshua, mwana wa Nuni, mtumishi wa [Yehova], akafa, mwenye umri wa miaka mia na kumi.” Hakika mwabudu huyo wa Yehova aliye mshikamanifu anatupa sisi, pia, kichocheo chenye nguvu tuwe hodari na wenye moyo wa ushujaa ‘tunapomcha Yehova na kumtumikia kwa unyofu wa moyo na kwa kweli.’—Yoshua 24:14, 15, 29.