Kuthamini Wazazi Wanaomwogopa Mungu
Wazazi wanaofanya bidii kulea watoto wao wawe watu wazima wenye kujali madaraka na wenye kumhofu Mungu wanafurahi wakati jitihada zao zinapofanikiwa. Wao wanafurahi vilevile wakati watoto wao wanapoonyesha uthamini kwa ajili ya utunzaji huo mzuri.
Inayofuata hapa ni barua iliyopelekwa na mwana mmoja na mke wake kwa wazazi wa mwana huyo baada ya arusi yao:
“Mama na Baba Wapendwa:
“Ah, tuanzie wapi? Acha tuanze kwa kusema jinsi tulivyothamini upendo, utegemezo, na ukarimu wenu katika siku yetu ya arusi. Kwa kweli hiyo ilikuwa ni siku ya pekee, na kuwapo kwenu kulikuwa kwa maana sana. Na zaidi, kama kwamba hayo hayakutosha, mlitusaidia katika kuifanya fungate yetu ifurahishe sana. Mambo hayo ambayo tumetaja ni uthibitisho zaidi wa kuwa kwenu wazazi wenye kutokeza, wenye upendo, wenye kiasi, na wenye kupenda furaha na nyakati zote mmekuwa hivyo!
“Je! mmepata kujiuliza ni kwa nini nimeweza kubaki katika njia iliyonyooka na iliyo nyembamba? Ni kwa sababu, mbali na upendo wangu kwa Yehova Mungu, sikuzote nimekuwa na staha kubwa sana kwa nyinyi wawili. Staha hiyo imekuwa yenye nguvu sana hivi kwamba ikiwa pamoja na nidhamu yenu, sikuzote imenifanya nifikirie kwa uzito wakati ninapofanya vitu na kufanya maamuzi. Mafanikio katika maisha yangu katika kufanya mapenzi ya Mungu kwa kweli yanatokana kwa sehemu kubwa na upendo wenu na nidhamu yenu yenye kudumu kwangu na ujitoaji wenu mkubwa kwa Yehova na tengenezo lake.
“Kama ningechukua kumbukumbu zangu zote za utotoni kuhusu nyinyi wawili na kuziweka pamoja, zingesema kwamba ingawa siwezi kukumbuka kila kitu mlichosema, ninakumbuka mwenendo wenu mzuri, hasa upendo wenu kwa wengine na kwa Yehova.
“Tunawapenda sana, sana.
“Mwana na binti-mkwe wenu,
“L. na W.”