Kusaidia Familia Yangu Iwe na Ufanisi wa Kiroho
Kama ilivyosimuliwa na Josephat Busane
Sitasahau kamwe safari ya garimoshi kwenda Johannesburg, Afrika Kusini, mnamo Januari 1941. Rafiki yangu wa tangu utotoni Elias Kunene na mimi tulikuwa tukirudi mahali petu pa kazi baada ya kuwa likizoni katika Zululand.
NDANI ya garimoshi pamoja nasi, palikuwa na mwanamume mmoja kijana aliyekuwa na muti, dawa ya uganga, ambayo kwa kawaida hupatikana kwa mchawi. Mtu huyo alipaka muti hiyo kwenye unyushi wake akiamini kwamba ingemsaidia apate kibali kutoka kwa mwajiri wake mzungu. Tulipokuwa tukishuka kutoka garimoshi, Elias alisema hivi: “Muti hiyo ndiyo mungu wake.” Maneno hayo yalinichoma moyo kama kisu kwa sababu mfukoni mwangu nilikuwa na muti yangu mwenyewe niliyokuwa nimeitayarisha kulingana na maelekezo ya mchawi mmoja.
Elias, nami, tulikuwa tukijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, na hivyo nikang’amua kwamba yeye alikuwa amefanya maendeleo makubwa zaidi ya kiroho kunishinda. Mara hiyo nikatupa muti hiyo ndani ya pipa la takataka na baada ya hapo nikajiunga na Elias kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa ukawaida.
Elias, nami, tulikuwa tumeoa. Kwa hiyo kwa nini tulifanya kazi katika jiji lililo umbali wa kilometa 400 kutoka nyumbani? Maisha ya jijini yalilinganaje na maisha ya mashambani katika Zululand? Na je, ushirika wetu na Mashahidi wa Yehova ulileta manufaa kwa familia zetu kule nyumbani?
Maisha Katika Zululand
Nilizaliwa katika Zululand, Afrika Kusini, katika 1908. Familia yetu iliishi katika wilaya ya Msinga, eneo la nyanda za nyasi, vilima, na michongoma. Hapa, katika vuli, maua machonge ya mti wa aloe hufunika ardhi kwa mng’aro mwekundu. Ng’ombe na mbuzi hulisha kwenye miteremko ya vilima kati ya miti. Maboma (mkusanyiko wa vibanda) na mashamba ya mahindi yametawanyika katika nyanda, mahindi yakiwa chakula cha msingi cha Wazulu.
Boma letu, kama yale mengine, lilitia ndani kibanda cha wazazi wangu, kimoja cha dada yangu, na kimoja changu na ndugu yangu. Kibanda kingine kilitumika kuwa mahali pa jikoni pa familia, na kulikuwa kingine cha kuhifadhia vitu. Kila kibanda kilikuwa na umbo la mzinga wa nyuki, chenye ukuta wa tope wa meta moja kwenda juu na kuba iliyoezekwa nyasi juu. Kati ya vibanda hivyo kuku huchakura ardhi, wakidonoa chakula, na hapo karibu kulikuwa na zizi la ng’ombe. Familia yetu iliridhika na maisha hayo sahili ya mashambani. Tulikuwa na chakula na makao, na baba yangu hakuhitaji kuajiriwa na mtu.
Lakini, mara nyingi hali ya usalama ya Zululand imeharibiwa. Vilima na mito hii mizuri imerowanishwa kwa damu ya wanadamu. Mwanzoni mwa karne ya 19, Zululand ilikaliwa na makabila kadhaa yaliyo huru. Ndipo akatokea shujaa wa Zulu aliyeitwa Shaka. Jeshi lake lilishambulia makabila yote yaliyo karibu. Waokokaji walitoroka au wakafyonzwa katika taifa la Zulu.
Baadaye, vita vilitokea kati ya Wazulu na Waholanzi walowezi. Mojawapo ilipiganwa kwenye mto ulio karibu na nyumbani kwetu. Damu nyingi sana ilimwagika mtoni hivi kwamba maji yaligeuka yakawa rangi nyekundu, hivyo ulipewa jina Blood River (Mto wa Damu). Kisha yakaja majeshi ya Uingereza. Kwenye kilima kiitwacho Isandlwana, kilicho karibu na nyumbani kwetu, maelfu ya watu walichinjwa katika mojawapo vita vingi vikali kati ya askari-jeshi wa Uingereza na Wazulu. Kwa kusikitisha, amani ya kudumu haijapata kupatikana katika sehemu yetu ya Zululand. Mara kwa mara, uhasama wa zamani wa kikabila hutokea.
Jitihada ya Kutafuta Ufanisi wa Kimwili
Mama yangu alikufa nilipokuwa na miaka mitano. Baba yangu na dada yangu mkubwa, Bertina, walinitunza na kunisaidia kusoma kwa miaka sita shuleni. Kisha, nilipokuwa na miaka 19, nilianza kazi ya kusaidia kuuza dukani katika mji wa karibu wa Dundee.
Nilisikia kwamba vijana wengi walikuwa wakichuma pesa nyingi zaidi katika jiji la Johannesburg, kitovu cha biashara ya uchimbaji migodi ya dhahabu cha Afrika Kusini. Kwa hiyo, mwaka uliofuata, nilihamia Johannesburg na kufanya kazi kwa miaka mingi nikibandika vibandiko vya matangazo katika sehemu za umma.
Katika Johannesburg, nilisisimuliwa sana na mambo ya kuvutia na fursa nyingi, lakini upesi nikang’amua kwamba maisha ya jijini yaliharibu maadili ya kidesturi ya watu wetu. Hata hivyo, ingawa vijana wengi walisahau familia zao zilizoishi mashambani, mimi sikusahau yangu kamwe na kwa kawaida niliwapelekea pesa nyumbani.
Baba yangu alikufa katika 1938. Nikiwa mwanae mkubwa zaidi, nilishurutika na desturi zetu za Kizulu “kufufua” boma letu la familia. Kwa hiyo, mwaka uliofuata, nilioa msichana kutoka Zululand, aitwae Claudina Madondo. Ingawa sasa nilikuwa na mke, bado niliendelea kufanya kazi umbali wa kilometa 400 katika Johannesburg. Wengi wa marika zangu walifanya vivyo hivyo. Ingawa ilinitia uchungu kutengwa na familia yangu kwa vipindi virefu, nilihisi nikiwa na daraka la kuwasaidia wafurahie maisha ya hali ya juu zaidi.
Ufanisi wa Kimwili au wa Kiroho?
Mama ndiye aliyekuwa mwenda-kanisani pekee katika familia yetu, na Biblia yake ndicho kilichokuwa kitabu pekee nyumbani mwetu. Muda fulani baada ya kifo chake, nikajua kusoma na mara hiyo nikaanza kuisoma. Lakini mafundisho na mazoea ya makanisa yalianza kunisumbua. Mathalani, washiriki waliendelea kupata kibali hata ingawa walikuwa wakifanya uasherati. Niliwauliza wahubiri juu ya kutopatana huko, lakini hakuna yule aliyenipa maelezo yenye kuridhisha.
Nilipokuwa Johannesburg, Elias Kunene, nami, tuliamua kutafuta dini ya kweli. Tulizuru makanisa katika ujirani wetu lakini hatukuridhishwa na yoyote kati yayo. Kisha Elias akakutana na Mashahidi wa Yehova. Alipojaribu kunielezea yale aliyojifunza kutoka kwao, nilimwambia kwamba alikuwa amedanganywa. Lakini baada ya kusikiliza mazungumzo yake na viongozi wa kanisa na kuona kushindwa kwao kumwonyesha kuwa amekosea, nilianza kusoma vichapo vya Watch Tower Society ambavyo Elias alinipa. Ni wakati huu ndipo nilipokuwa katika ile safari ya garimoshi isiyoweza kusahaulika wakati Elias aliponisaidia kutambua hatari ya kutumaini muti.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Mithali 3:5, 6.
Kisha nikajiunga na Elias katika kushiriki kwa ukawaida na kutaniko la kwanza la weusi la Mashahidi wa Yehova katika Johannesburg. Katika 1942, baada ya kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova, nilibatizwa katika Orlando, Soweto. Katika safari zangu za kwenda nyumbani Zululand, nilikuwa nikijaribu kushiriki imani yangu na Claudina, lakini yeye alijitia sana katika shughuli za kanisa.
Hata hivyo, yeye alianza kulinganisha fasihi yetu na Biblia yake, na hatua kwa hatua kweli ya Neno la Mungu ilifikia moyo wake. Yeye alibatizwa katika 1945. Akawa mhudumu Mkristo mwenye bidii, akishiriki kweli ya Biblia na majirani zake na kuikaza mioyoni ya watoto wetu.
Wakati huohuo, katika Johannesburg, nilikuwa na pendeleo la kusaidia watu fulani kuja katika ujuzi wa kweli ya Biblia. Kufikia 1945 kulikuwa na makutaniko manne ya weusi katika ujirani wa Johannesburg, na nilitumikia nikiwa mwangalizi msimamizi wa Kutaniko la Small Market. Baada ya muda mwelekezo wa Kimaandiko ulitolewa ili wanaume waliooa waliofanya kazi mbali na nyumbani kwao warudi kwa familia zao na kutoa uangalifu mwingi zaidi kwa madaraka yao wakiwa vichwa vya familia.—Waefeso 5:28-31; 6:4.
Elias alikuwa wa kwanza kuondoka Johannesburg, asiweze kuacha familia yake tena kamwe. Kama tokeo, mke wake na watoto wake wote watano wakawa Mashahidi wa Yehova walio watendaji. Elias pia alilea wapwa wanne wa kike na wa kiume wasio na wazazi, ambao walikuja kuwa Mashahidi waliojiweka wakfu. Alikufa katika 1983, akiwa ameweka kielelezo kizuri katika kufuata kwa uaminifu mielekezo ambayo Yehova hutoa kupitia Neno lake na tengenezo lake la kidunia.
Katika 1949, niliacha kazi yangu katika Johannesburg ili kutunza familia yangu katika njia ya Yehova. Huko nyumbani niliajiriwa na mkaguzi wa mifugo nikiwa msaidizi kwenye maogesho. Ilikuwa vigumu kutegemeza familia ya watoto sita kwa mshahara mdogo niliopata. Kwa hiyo ili kugharimia matumizi, niliuza pia mboga na mahindi tuliyokuza nyumbani.
Baraka za Thamani Kubwa Zaidi
Ingawa familia yetu haikuwa na ufanisi wa kimwili, tulikuwa na hazina za kiroho kwa sababu ya kufuata mielekezo ya Yesu: “Msijiwekee hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi.”—Mathayo 6:19, 20.
Kupata hazina hizo za kiroho hutaka kazi ngumu, kama vile ambavyo kuchimbua dhahabu kwenye migodi katika Johannesburg. Kila jioni nilikuwa nikishiriki andiko la Biblia pamoja na watoto wangu na kuwataka kila mmoja wao aniambie kile alichojifunza. Kwenye miisho-juma nilikuwa nikiwachukua, kwa zamu, katika kazi ya kuhubiri. Tulipokuwa tukitembea kutoka boma moja hadi nyingine, nilikuwa nikizungumzia mambo ya Kimaandiko na kujaribu kukaza viwango vya Biblia vya hali ya juu mioyoni mwao.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.
Kwa kielelezo, ili kuhakikisha kwamba watoto wetu hawakuiba, nilihakikisha kwamba kitu chochote walicholeta nyumbani hakikuwa kimeibwa. (Waefeso 4:28) Vivyo hivyo, mmoja wao aliposema uwongo, sikujizuia kutumia fimbo ya nidhamu. (Mithali 22:15) Pia nilitaka kwamba waonyeshe staha inayofaa kwa watu wa umri mkubwa zaidi.—Mambo ya Walawi 19:32.
Nikiwa kichwa cha familia, niliweka kielelezo kwa kutokosa mikutano, na nilitaka watoto waihudhurie pia. Nilihakikisha kwamba kila mtoto alikuwa na kitabu cha nyimbo, Biblia, na kichapo kingine chochote kilichotumiwa kwenye mikutano. Pia tulitayarisha kwa ajili ya mikutano yetu pamoja, na ikiwa mtoto hakutoa maelezo, nilikuwa nikijaribu kumsaidia afanye hivyo kwenye mkutano unaofuata.
Kwa miaka mingi familia yetu ndiyo iliyokuwa katika hali ya kuweza kuandaa ukaribishaji kwa waangalizi wasafirio. Wawakilishi hao wa Watch Tower Society walikuwa na uvutano mzuri juu ya watoto wetu na walijenga ndani yao tamaa ya kuwa mapainia, au waeneza evanjeli wa wakati wote. Mke wangu nami tulifurahi wakati mwana wetu mkubwa zaidi, aitwaye Africa, alipoanza kupainia baada ya kumaliza miaka kumi ya masomo. Hatimaye yeye alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye, na baadaye alialikwa kwenye ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ya Afrika Kusini, ambako alifanya kazi akiwa mtafsiri. Sasa yeye ameoa na ana watoto wake mwenyewe. Yeye anatumikia akiwa mzee katika kutaniko moja katika Zululand, na pia ana pendeleo la kusaidia tawi la Afrika Kusini na matatizo ya kisheria yanayozuka mara kwa mara kwa sababu ya masuala yanayohusu ibada ya kweli.
Wote pamoja, tulikuwa na wavulana watano na msichana mmoja. Watoto wote sita sasa wamekua na ni wenye nguvu kiroho. Hilo limejaza mioyo yetu furaha nyingi—uradhi mwingi usioweza kununuliwa kwa vitu vya kimwili. Wanne kati ya wana wangu watumikia wakiwa wazee katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova wanayoshirikiana nayo. Mmoja wao, Theophilus, sasa afurahia pendeleo la utumishi wa Betheli kwenye tawi la Afrika Kusini.
Kueneza Kweli Katika Zululand
Niliporejea hatimaye ili kuishi na familia yangu katika Zululand katika 1949, kulikuwako wahubiri wa Ufalme watatu tu katika Kutaniko letu la Collessie. Baada ya muda, kutaniko hilo lilikua, na kutaniko la pili lilianzishwa umbali wa kilometa 30 kutoka hapo katika kijiji cha Pomeroy.
Kwa muda wa miaka, nyakati nyingine kazi yetu ya kuhubiri ingekatizwa kwa sababu ya vita vya kikabila katika jumuiya. Waenda-kanisani hujitia ndani katika vita hivyo vya kikabila. Ni Mashahidi wa Yehova peke yao wanaojulikana kwa sababu ya kutokuwamo kwao. Wakati mmoja, vita vilizuka kati ya makabila ya Mabaso na maBomvu katika eneo nililoogeshea ng’ombe. Watu wa eneo hilo walikuwa wa kabila la Mabaso na kwa kawaida wangeniua kwa sababu walijua kwamba nilitoka kwa kabila la maBomvu. Hata hivyo, wao walijua pia kwamba nilikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na hivyo hawakunidhuru.
Wakati wa miaka ya 1970, visa vya mapigano ya kikabila vilichacha, na wilaya ya Msinga ikawa hatari kabisa. Tukiwa pamoja na wengine, niliamua kuhamisha familia yangu kwenye sehemu yenye amani zaidi katika Zululand. Katika 1978 tulihamia mji wa Nongoma, ambako tulianza kushiriki na Kutaniko la Lindizwe. Mwaka uliofuata, mke wangu mpendwa, Claudina, alikufa. Kumpoteza yeye kulinishtua sana, na afya yangu ilidhoofika vibaya.
Lakini, kwa fadhili zisizostahilika za Yehova, nilipata nafuu vya kutosha kuweza kuanza utumishi wa painia miaka miwili baadaye. Nina shukrani kama nini kwa Yehova kwamba afya yangu hasa imeboreka kwa kuwa na utendaji huu wa kuhubiri ulioongezeka! Sasa nina miaka 85 na bado huweza kufikia wastani wa saa 90 katika kazi ya kuhubiri kila mwezi. Katika Januari 1992, nilihama na mwanangu Nicholas hadi Muden, sehemu ya Zululand ambako kuna uhitaji wa wapiga mbiu ya Ufalme zaidi.
Jinsi nilivyo na shukrani kwa ajili ya mwelekezo kutoka kwa tengenezo la Yehova uliotutia moyo tutoe uangalifu bora zaidi kwa mahitaji ya kiroho ya familia zetu! Baraka ambazo tumepata ni nyingi zaidi ya chochote ambacho fedha zaweza kununua. (Mithali 10:22) Ninamsifu Yehova kwa yote hayo na kuomba kwa ajili ya wakati ambapo Ufalme wake utabadili dunia hii kuwa paradiso. Ndipo maisha katika vilima na nyanda hizi nzuri za Zululand yatakapokuwa yenye amani milele wakati ambapo wenyeji “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.